KAMATI YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA YAPONGEZA UJENZI WA HOSPITALI YA WILAYA YA KILOLO

January 28, 2018
image1
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa ikiwasili katika Hospital ya Kilolo kukagua ujenzi wa Hospital ya Wilaya.
image2
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa ikipokea Taarifa ya Ujenzi wa Hospital ya Wilaya ya Kilolo ilipofanya ziara ya Ukaguzi wa Katika Mradi huo!
image3
Huu ndio muonekano wa  Sehemu ya Jengo la Hospital ya Wilaya ya Kilolo inayoendelea kujengwa.
image4
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Josephat Kakunda(Pili Kushoto) akijadili jambo na Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikalinza Mitaa wakati wa Ziara katika Mradi wa Ujenzi wa Hospital ya Wilaya ya Kilolo.
………………
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imepongeza  ujenzi wa majengo mbalimbali ya kutolea huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Kilolo Mkoani Iringa.
Kamati hiyo imetoa Pongezi hizo wakati walipotembelea Kilolo na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Hospitali hiyo.
Wabunge wamepongeza kazi inayofanywa na wakandarasi kwani ipo katika ubora mzuri na kiwango cha kuridhisha.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati Mhe. Mwanne Mchemba aliyeongoza Waheshimiwa hao amesema “naipongeza sana Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, uongozi na watumishi kwa ujumla kwa usimamizi mzuri wa ujenzi wa Hospitali ya Wilaya, ujenzi ni wa kiwango cha juu na thamani ya fedha inaonekana”.
Kamati imeagiza Halmashauri kuhakikisha inakamilisha majengo yote kwa wakati ili huduma ianze kutolewa mara moja.
Ameongeza kuwa ni vizuri kipindi hiki ambacho ujenzi unaendelea Halmashauri ijipange kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba, vitendanishi na dawa pamoja na kuajiri watumishi.
Naye Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI Mhe. Josephat Kandege ameziagiza Halmashauri zote nchini ambazo hazina Hospitali za Wilaya zianze taratibu za ujenzi mara moja ili kuimarisha utoaji wa huduma za afya nchini.
Hadi sasa ujenzi uliofanyika ni wa majengo matano ambayo ni jengo la wagonjwa wa nje; jengo la maabara; jengo la huduma ya mionzi; jengo la huduma ya afya ya uzazi na mtoto; na jengo la wagonjwa wa ndani. Ujenzi wa majengo haya hadi kukamilika unatarajia kutumia kiasi cha fedha shilingi bilioni  4.4.
Aidha, mradi mzima wa Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kilolo utagharimu Tsh. Bil 12.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »