Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo akitoa maelekezo kwa watendaji wa Halmashauri ya Rombo
Ujenzi wa jengo la upasuaji linaloendelea katika Kituo cha Afya Karume wilayani Rombo
Nyumba ya daktari inayojengwa katika Kituo cha Afya Karume wilayani Rombo
Jengo la wodi ya wazazi inayojengwa katika kituo cha Afya Karume.
…………………………………………………………………………………………….
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,
TAMISEMI Mhe. Selemani Jafo ameonyesha kukerwa na kutoridhishwa na kasi
ya utendaji kazi wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Rombo na
watendaji wake wa chini kwa kushindwa kwenda sambamba na kasi anayoitaka
katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Hali hiyo ilijitokeza leo wakati Jafo alipokuwa katika ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo iliyopo mkoani Kilimanjaro.
Amesema Halmashauri ya wilaya ya
Rombo ni miongoni mwa Halmashauri zilizopokea fedha za awamu ya kwanza
ya uboreshaji vituo vya afya lakini licha ya kupokea fedha hizo tokea
mwezi Agosti mwaka 2017 bado wapo nyuma ukilinganisha na halmashauri
zingine zilizopata fedha kwa wakati mmoja.
Akikagua kituo cha afya Karume ,
Waziri Jafo amemtaka mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kufanya kazi kwa
weledi na kuwapa ushirikiano wa kutosha watendaji walio chini yake ili
waweze kumaliza kazi hiyo kabla Februari 25, mwaka huu.
Kadhalika, Jafo amewapongeza Mkuu
wa wilaya ya Rombo Agness Hokololo na Katibu Tawala wake wa wilaya
Asenga kwa kazi kubwa wanayofanya ya kusimamia maendeleo ya wilaya hiyo.