YONDANI KUIKOSA RWANDA, MBARAKA NAFUU

December 08, 2017
Want create site? Find Free WordPress Themes and plugins.
Beki wa timu ya Taifa ya Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’ Kelvin Yondani ataukosa mchezo dhidi ya Rwanda utakaofanyika kesho Jumamosi Desemba 9, 2017 kwenye Uwanja wa Kenyatta, Machakos Kenya.
Yondani amepewa mapumziko ya siku tatu baada ya kupata majeraha ya kifundo cha mguu kwenye mchezo wa jana dhidi ya Zanzibar.
Hivyo atakosa mchezo huo wa kesho ukiwa ni miongoni mwa mechi mechi za michuano ya kuwania Kombe la Afrika Mashariki maarufu kama Cecafa Senior Challenge inayofanyika hapa Kenya.
Jopo la Madaktari wa Kilimanjaro Stars linaloundwa na Dk. Richard Yomba na Dk Gilbert Kigadye limethibitisha kuwa majeraha aliyoyapata Yondani sio makubwa na yanahitaji apumzike kwa saa 72 ambazo ni sawa na siku tatu.
Vipimo vilivyochukuliwa vinaonesha kuwa hakuna mfupa wowote ulioathirika zaidi ya kupata mshtuko kiasi kwa hiyo wamempa siku tatu za mapumziko wakiendelea kumtazama maendeleo yake kwa ukaribu.
Kwa upande wa Mbaraka Yusuph ambaye alipata majeraha ya misuli kwenye mchezo wa kwanza dhidi ya Libya, amepona na anatarajia kuingia kwenye program ya utimamu wa mwili.
Hata hivyo Mbaraka hataweza kucheza kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Rwanda.

Wakati huo huo, leo kikosi cha Kilimanjaro Stars kimefanya mazoezi kwenye Uwanja wa Machakos Academy licha ya mvua zinazoendelea kunyesha hapa County ya Machakos.
Kilimanjaro inajiandaa na mchezo wa kesho dhidi ya Rwanda utakaochezwa saa 8 mchana kwenye Uwanja wa Kenyatta, Machakos.
Mchezo huo wa kundi A una umuhimu mkubwa kwa Kilimanjaro Stars katika harakati zake za  kuitafuta tiketi ya kucheza hatua ya nusu fainali.
Kilimanjaro Stars ina pointi moja mpaka sasa baada ya kutoka sare na Libya kwenye mchezo wa kwanza kabla ya kufungwa na Zanzibar kwenye mchezo wake wa pili.
Kundi A linaongozwa na  Zanzibar wenye pointi sita (6) wakifuatiwa na Uganda wenye pointi (4) wakati Libya yenyewe ina pointi (3) ikikamata nafasi ya tatu ikifuatiwa na Kilimanjaro Stars na Rwanda wenye pointi (1) kila mmoja.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »