Want create site? Find Free WordPress Themes and plugins.
Beki
wa timu ya Taifa ya Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’ Kelvin Yondani
ataukosa mchezo dhidi ya Rwanda utakaofanyika kesho Jumamosi Desemba 9,
2017 kwenye Uwanja wa Kenyatta, Machakos Kenya.
Yondani amepewa mapumziko ya siku tatu baada ya kupata majeraha ya kifundo cha mguu kwenye mchezo wa jana dhidi ya Zanzibar.
Hivyo atakosa mchezo huo wa kesho ukiwa ni miongoni mwa mechi mechi
za michuano ya kuwania Kombe la Afrika Mashariki maarufu kama Cecafa
Senior Challenge inayofanyika hapa Kenya.
Jopo la Madaktari wa Kilimanjaro Stars linaloundwa na Dk. Richard
Yomba na Dk Gilbert Kigadye limethibitisha kuwa majeraha aliyoyapata
Yondani sio makubwa na yanahitaji apumzike kwa saa 72 ambazo ni sawa na
siku tatu.
Vipimo vilivyochukuliwa vinaonesha kuwa hakuna mfupa wowote
ulioathirika zaidi ya kupata mshtuko kiasi kwa hiyo wamempa siku tatu za
mapumziko wakiendelea kumtazama maendeleo yake kwa ukaribu.
Kwa upande wa Mbaraka Yusuph ambaye alipata majeraha ya misuli kwenye
mchezo wa kwanza dhidi ya Libya, amepona na anatarajia kuingia kwenye
program ya utimamu wa mwili.
Hata hivyo Mbaraka hataweza kucheza kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Rwanda.
Wakati huo huo, leo kikosi cha Kilimanjaro Stars kimefanya mazoezi
kwenye Uwanja wa Machakos Academy licha ya mvua zinazoendelea kunyesha
hapa County ya Machakos.
Kilimanjaro inajiandaa na mchezo wa kesho dhidi ya Rwanda utakaochezwa saa 8 mchana kwenye Uwanja wa Kenyatta, Machakos.
Mchezo huo wa kundi A una umuhimu mkubwa kwa Kilimanjaro Stars katika
harakati zake za kuitafuta tiketi ya kucheza hatua ya nusu fainali.
Kilimanjaro Stars ina pointi moja mpaka sasa baada ya kutoka sare na
Libya kwenye mchezo wa kwanza kabla ya kufungwa na Zanzibar kwenye
mchezo wake wa pili.
Kundi A linaongozwa na Zanzibar wenye pointi sita (6) wakifuatiwa na
Uganda wenye pointi (4) wakati Libya yenyewe ina pointi (3) ikikamata
nafasi ya tatu ikifuatiwa na Kilimanjaro Stars na Rwanda wenye pointi
(1) kila mmoja.