NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII AFANYA ZIARA KATIKA HIFADHI YA SAADANI

December 30, 2017

1
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga  (katikati) akioneshwa   ramani ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani na  Mwakilishi wa Mkuu wa Hifadhi za Taifa, Vitalis Kuluka huku akishirikiana kuonesha  eneo hilo na  Katibu Tawala wa Wilaya ya Bagamoyo,Erica Yigella ( wa pili kulia)    mahali kilipo Kitongoji cha Uvinje ambapo wakazi wa eneo hilo wamegoma kuhama ndani ya  hifadhi hiyo na wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea hifadhi hiyo jana. Wa kwanza kulia ni  Afisa Wanyamapori, Godfrey Maro na  Wa kwanza kushoto ni Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Stephano Msumi na pande wa kulia nyuma ya Katibu Tawala ni Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa,  Fredrick Mofulu   
2a
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga  ( wa pili kulia )  akizungumza na Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya  Saadani , Stephano Msumi ( katikati)  wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea hifadhi hiyo jana kwa ajili ya kujionea changamoto mbalimbali zinazoikabili . Wa kwanza kulia ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Bagamoyo, Erica Yigella, Wa kwanza kushoto ni  Mwakilishi wa Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Vitalis Kuluka, wa tatu  kushoto ni Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa,   Fredrick Mofulu  
3
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga  akizungumza jana  na  Wananchi wa  Kitongoji cha Uvinje ambao wamegoma kuhama ndani ya  hifadhi hiyo,  wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea kwa ajili ya kuzungumza nao ili kujua ukubwa tatizo  la mgogoro huo uliodumu kwa zaidi ya miaka 10 sasa .
4
Bango lililopo katika geti la Gama   linalokuelekeza sheria na taratibu  ukiwa unaingia katika Hifadhi ya Taifa ya Saadani iliyopo wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.
5
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga  ( kushoto )  akipatiwa maelezo na  Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya  Saadani , Stephano Msumi ( katikati)  wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea hifadhi hiyo jana kwa ajili ya kujionea changamoto mbalimbali zinazoikabili .Wa kwanza kulia ni  Mwakilishi wa Mkuu wa Hifadhi ya Taifa, Vitalis Kuluka, nyuma ya Mhifadhi  wa Saadani ni Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa,   Fredrick Mofulu
6
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga  ( mbele ) akiwa na baadhi ya viongozi wa Hifadhi za Taifa  pamoja  kamati ya ulinzi na usalama  kutoka Wilayani Bagamoyo  akiongoza kwenda kuangalia sehemu kunakofanyika utalii wa boti katika  Hifadhi ya Taifa ya  Saadani  wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea hifadhi hiyo jana kwa ajili ya kujionea changamoto mbalimbali zinazoikabili .
7
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (wa pili kulia)   akipatiwa maelezo na Msaidizi wa Mkurugenzi Mkuu wa Hifadhi za Taifa,   Fredrick Mofulu ( wali kushoto) kuhusiana na sehemu kunakofanyika utalii wa boti katika  Hifadhi ya Taifa ya  Saadani .  Wengine ni   baadhi ya viongozi wa Hifadhi za Taifa pamoja na kamati ya ulinzi  kutoka Wilayani Bagamoyo . 
Picha na Lusungu Helela
……………
Wananchi wa Kitongoji  cha Uvinje  kilichomo ndani Hifadhi ya Taifa ya Saadani iliyopo wilayani Bagamoyo Mkoani wa Pwani wamesema  hawapo tayari kuhama wala kulipwa fidia  ili kupisha hifadhi hiyo.
Kitongoji hicho, ambacho ni kati ya vitongoji nane vya Kijiji cha Saadani, kilitakiwa kiondolewe tangu mwaka 2005 baada ya hifadhi hiyo kupandishwa daraja kutoka pori la akiba na kuwa hifadhi kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Namba 281 la Septemba 16, 2005.
Akizungumza mbele ya kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya  ya Bagamoyo, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga wakati  alipofanya ziara jana  katika  kijiji hicho aliwambia wananchi hao kuwa lengo la ziara yake ni kutaka kuwasikiliza juu mgogoro huo na sio kuwahamisha.
‘Mimi ni mgeni kidogo kwenye Wizara hii, Nimekuja kuangalia   sio kuwahamisha kwa kuwa sijui eneo hili lina ukubwa kiasi na lina kaya ngapi  lakini nimekuja kutembelea hifadhi na maeneo yote yenye changamoto. ‘’ alisema
Alisema   amefika kwa ajili ya    kuwasikiliza ili aweze kujua jinsi mgogoro ulivyo kwa sababu hakutaka  kusikia upande mmoja wa TANAPA pekee.
Naye , Kaimu Mwenyekiti wa  Kitongoji hicho, Hassan Akida alisema  wakazi wa eneo hilo hawapo tayari kuhama na wala kulipwa fidia kwa vile  ni ardhi yao tokea enzi za mababu zao.’
‘Tumesema hapa ndo kwetu mnataka kutuhamisha mtupeleke wapi wakati sisi tumezoea maisha yetu hapa’’ alisema Akida.
Aliongeza  kuwa kitongoji hicho kimekuwapo kwa muda mrefu na waliishi bila shida  hadi pale  pori hilo lilipobadilishwa na kuwa Hifadhi ya Taifa
“Wakati hili ni pori la akiba tuliishi vizuri tu na wazazi wetu walikuwa ni wafanyakazi wa pori. Lakini tangu iwe hifadhi   imekuwa taabu. Sasa tunafukuzwa wakati tumezaliwa hapa na wazazi wetu wamezikwa hapa hapa,” anasema Hassan Akida.  
Kwa upande wa  Mwenyekiti wa Kijiji cha Saadani,  Adam Mwandosi  alisema  mgogoro huo umedumu kwa muda mrefu  na umekuwa ukileta chuki kati ya Serikali na wananchi.
Amesema  wananchi wa eneo hilo muda mwingine wamekuwa wakimuona hata yeye  Mwenyekiti wao kama anawasaliti   kwa vile tokea mgogoro huo ulipoanza  viongozi wengi wamekuwa wakifika hapo lakini wamekuwa hawana majibu ya kumaliza mgogoro huo.
Mhifadhi Mkuu wa Saadani, Stepahano Msumi amesisitiza kuwa kitongoji hicho kimo ndani ya hifadhi kinyume cha sheria.
Alisisitiza kuwa sheria za hifadhi za Taifa haziruhusu makazi ya watu ndani yake.
“Kwa ufupi tu ukiangalia GN (Tangazo la Serikali) linaonyesha kuwa eneo lote la kitongoji cha Uvinje liko ndani ya hifadhi. Ni kweli lilikuwa eneo la watu ambao walikuwa watumishi wa pori la akiba tangu lilipoanzishwa mwaka 1968. Waliombwa kuondoka lakini waliendelea kuongezeka,” anasema.
Anasema katika makubaliano, iliamuliwa kuwa walipwe fidia kwa taratibu lakini hata  hivyo licha ya kutekeleza utaratibu wa fidia bado wamegoma kuipokea mbali ya wachache kujitokeza.
Ikumbukwe kuwa, Saadani ni hifadhi pekee ya Taifa nchini na Afrika Mashariki yenye fukwe za bahari na inayotazamana na Bahari ya Hindi na fukwe zake zinakutana na uoto wa asili wa nchi kavu.
Inapatikana katika mikoa ya Tanga na Pwani. Uwepo wake ni matokeo ya pori la akiba la Saadani, ranchi ya Mkwaja na sehemu ya kaskazini, sambamba na akiba ya msitu wa asili wa Zaraninge.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »