SIMBA YAJIPELEKA MIKONONI MWA YANGA NUSU FAINALI KOMBE LA MAPINDUZI,JUMANNE SAA MBILI USIKU ZANZIBAR KUTIKISIKA

January 09, 2017
ngoma-vs-juuko
Na.Alex Mathias.
Ushindi wa tatu wa Simba katika Michuano ya Kombe la Mapinduzi Zanzibar yameifanya ifikishe jumla ya pointi 10 na kuongoza kundi A na sasa itakutana na watani wao jadi Yanga Mchezo wa Nusu Fainali itakayopigwa siku ya Jumanne kwenye uwanja wa Amaan baada ya kuwatandika Jang’ombe boys magoli 2-0.
Simba waliuanza mchezo kwa kasi ya 4G huku Shiva Kichuya akiwatesa mabeki wa Jang’ombe boys na katika dakika ya 11 Laudit Mavugo aliwanyanyua mashabiki waliokuwa wamefurika akimalizia kazi nzuri ya Kichuya na mashabiki kulipuka shangwe kwa kusema kuwa tunaitaka Yanga Nusu fainali.
Hadi mwamuzi Mfaume Nassoro anapuliza kipyenga cha Mapumziko Simba walikuwa mbele kwa ushindi wa bao hilo moja la mshambuliaji Raia wa Burundi ambaye amekuwa kwenye wakati mgumu kutokana na kushindwa kuonesha kiwango cha hali ya juu kwa mashabiki wa Simba.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kufanya mabadiliko hata hivyo Simba waliendelea kuumiliki mchezo huo na kuweza kupata bao la pili dakika ya 53 kupitia kwa Laudit Mavugo aliyeachia bonge la shuti na kujaa moja kwa moja golini huku shangwe za mashabiki wa Simba zikisema kiama kwa Yanga siku ya Jumanne ya Januari 10.
Hadi dakika 90 za mwamuzi Mfaume Nassoro ubao ulikuwa ukisomeka Simba 2-0 dhidi ya Jang’ombe boys iliyokuwa chini ya Mchezaji wa zamani wa Yanga Abdi Kassim na kuwafanya Jang’ombe wayaage mashindano hayo wakiwa na pointi zao 6.
Kwa matokeo hayo Simba itacheza na Yanga siku ya Jumanne saa mbili usiku mchezo wa Nusu Fainali  ambao unategemewa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na historia ya ikumbukwe mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania bara timu hizo zilitoka sare ya kufungana 1-1.
Yanga wanaingia Nusu Fainali na kumbukumbu ya kuunganisha kifurushi cha 4G toka kwa matajiri wa jij la Dar es salaam timu ya Azam FC ambao waliwadhalilisha kwa kipigo cha magoli 4-0 na tayari kamati ya mashindano imetaja viingilio vya mechi hiyo huku kiingilio cha chini kabisa ni cha sh elfu tatu na cha juu elfu kumi.
Mchezo wa pili utachezwa saa mbili na robo kati ya Taifa Jang’ombe dhidi ya Mabingwa watetezi URA toka Uganda na mshindi wa hapa atakutana na Azam FC Nusu Fainali ya kombe la Mapinduzi.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »