DAWASCO KUGHARAMIA GHARAMA ZA UUNGANISHAJI KWA WATEJA WAPYA.

May 10, 2016
Mhandisi Cyprian Luhemeja.
Katika kutekeleza agizo la serikali la kuwafikia wateja laki 4 (400,000) ifikapo June 2016 ,Shirika la Majisafi na Majitaka jijini Dar es salaam (Dawasco) ,linaendelea na zoezi  la uunganishaji wa huduma ya Maji kwa wananchi wote wa jiji la Dar es salaam pamoja na miji ya Bagamoyo na Kibaha mkoani Pwani huku ikigharamia gharama zote za uunganishaji ambazo awali zilikuwa zikilipwa na mteja.


Akiongea na waandishi wa habari hivi Afisa mtendaji mkuu wa Dawasco, Mhandisi Cyprian Luhemeja ameeleza kuwa kwenye awamu hii ya zoezi la uunganishaji wateja wapya shirika litagharamia gharama zote za maunganisho ambazo ni gharama za uunganishaji, mabomba na vifaa vya uunganishaji ambapo mteja atawajibika kurudisha gharama hizo za maunganisho kidogo kidogo kila mwezi kwa kipindi cha miezi 12 baada ya kupata huduma ya Maji.

“Dawasco itamuunganishia huduma ya maji na kugharamia gharama zote uunganishaji ila mteja atawajibika kurudisha ile gharama kidogokidogo kila mwezi kwa kipindi cha miezi 12 baada ya kupata huduma ya Maji hii itasaidia hata wale ambao kipato chao ni cha chini kuweza kuunganishiwa huduma ya Maji” alisema Luhemeja.

Pia Mhandisi Cyprian Luhemeja ameleeza kuwa zoezi hili la uunganishia wateja wapya ni la kipindi cha miezi miwili tu cha Mei na Juni 2016 hivyo wananchi wote watumie fursa hii kwa kufika katika ofisi za Dawasco za kanda ili kupata huduma hiyo.


“Zoezi hili la kugharamia  gharama za uunganishaji huduma ya maji kwa wateja ni kwa kipindi maalum cha miezi miwili tu ambacho ni Mei na Juni hivyo wananchi watumie fursa hii kujitokeza iliwaweze kuunganishiwa na katika kipindi chote cha zoezi Ofisi za Dawasco zitakuwa wazi kuanzia jumatatu hadi jumapili” alisema Luhemeja.

Hata hivyo Dawasco imeeleza kuwa wananchi pamoja wateja wake wameweza kuwasiliana na kituo  cha huduma kwa wateja kupitia namba 022-2194800 au 0800110064 (bure) ili waweze kupata huduma na maelezo zaidi kuhusiana na zoezi hilo la uunganishaji huduma ya Maji.


Mapema mwaka huu serikali kupitia kwa waziri mwenye dhamana ya kusimamia Wizara ya Maji, Mh Mhandisi Gerson  iliagiza Shirika la Dawasco kuongeza idadi ya wananchi wanaopata huduma ya Majisafi kutoka 156,000 waliopo sasa kufikia wateja 400,000 (laki nne) ili kwenda sambamba na ongezeko la watu pamoja na mahitaji makubwa ya Maji yanayohitajika katika jiji la Dar es salaam.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »