Waziri Ummy awaonya watendaji wa sekta ya afya watakaozembea kutoa taarifa ya kipindupindu

February 08, 2016

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amewataka watendaji wa Serikali na Sekta ya Afya kuwajibika ipasavyo kwa  kutoa taarifa sahihi juu ya idadi ya wagonjwa wa kipindupindu nchini.
Akitoa tamko kuhusu mwenendo wa ugonjwa wa kipindupindu nchini pamoja na tahadhari ya ugonjwa wa Zika leo jijini Dar es salaam Mhe. Ummy amesema kuwa watendaji watakaoficha taarifa za wagonjwa katika maeneo yao watawajibishwa.
“Mojawapo wa changamoto katika mapambano ya kudhibiti mlipuko huu wa kipindupindu ni utoaji wa idadi pungufu au kutotoa kabisa taarifa za wagonjwa wa kipindupindu hivyo kupelekea kutokuwa na mafanikio katika mikakati iliyowekwa” alisema Waziri Ummy
 Aidha, ametoa wito kwa sekta nyingine kushirikiana na Wizara kupambana na ugonjwa huo ili kukabiliana  na baadhi ya changamoto zinazowakabili watoa huduma za afya na elimu walioko katika maeneo mbalimbali nchini.
“ Jukumu la kupambana na mlipuko wa ugonjwa huu si la Wizara ya Afya pekee  naomba sekta nyingine ikiwemo Maji, Miondombinu, Biashara Elimu na Mazingira tushirikiane kwa pamoja ili kuutokomeza ugonjwa huu”
Mbali na hayo Mhe. Ummy ameeeleza kuwa takwimu za kuanzia tarehe 1 hadi 7 februari mwaka huu zinaonyesha kuwa idadi ya wagonjwa wa kipindupindu imepungua kutoka 459 ya wiki iliyoisha tarehe 31 Januari hadi 258 ambapo ni sawa na punguzo la asilimia 44%.
Hata hivyo Wizara imewatoa hofu wananchi na kuwakumbusha kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Homa ya Zika pamoja na magonjwa mengine yanayoenezwa na Mbu.
Imeandaliwa na Beatrice Lyimo- Maelezo

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »