Kamishna wa Sensa ya Watu na
Makazi ya mwaka 2012 Hajjat Amina Mrisho Said akizungumza na waandishi
wa habari leo kuhusu nia yake ya kugombea nafasi ya Ubunge wa Jimbo la
Kiteto lililoko mkoani Manyara kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kamishna wa Sensa ya Watu na
Makazi ya mwaka 2012 Hajjat Amina Mrisho Said akisisitiza jambo wakati
akizungumza na waandishi wa habari leo kuhusu nia yake ya kugombea
nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Kiteto lililoko mkoani Manyara kwa tiketi
ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Kulia kwake ni mume wake Alhajj Abeid
Omary Khamis.
………………………………….
Na. Mwandishi wetu Dar es Salaam
Kamishna wa Sensa ya Watu na
Makazi ya mwaka 2012 Hajjat Amina Mrisho Said ametangaza nia ya kugombea
nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Kiteto lililoko mkoani Manyara kwa tiketi
ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam
Hajjat Amina Mrisho Said amesema iwapo atateuliwa na CCM kuwa mgombea wa
Jimbo la Kiteto, atahakikisha anatoa ushirikiano wa hali ya juu ili
kuleta maendeleo ya wananchi wa jimbo hilo.
Ametaja vipaumbele vyake kuwa ni kufuatilia kwa ukaribu
utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2015 – 2020 na kufanikisha ujenzi
wa Chuo cha VETA jimboni ili vijana waweze kupata elimu ya stadi za kazi
na hatimaye waweze kujiajiri.
Kuhusu suala zima la ufugaji, Hajjat Amina amesema atahamasisha
uendelezaji wa ufugaji wenye tija kwa kuifuatilia Serikali ili iweke
miundombinu katika maeneo yote ya wafugaji jimboni.
Vipaumbele vingine ni pamoja na kuhamasisha ujenzi wa Soko la
Kimataifa la Mazao hasa mahindi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya
matumizi ya stakabadhi ya mazao gharani na kuwashirikisha wananchi wote
katika kujiletea maendeleo kwenye maeneo yao.
Hajjat Amina Mrisho Said kitaaluma ana Shahada ya Uzamili wa
Mifumo ya Kompyuta na amewahi kuwa Mkuu wa mkoa wa Iringa na Pwani
ambapo kwa sasa ni Kamishna wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012.