Maadhimisho ya Wiki ya Ukombozi wa Bara la Afrika Mei 25 hadi 29 mwaka huu.

May 20, 2015

images 
Na Lorietha Laurence-Maelezo
Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Kushirikiana na Shirika la Kimataifa linaloshughulikia Elimu,Sayansi na Utamaduni (UNESCO) itaadhimisha wiki ya Ukombozi wa Bara la Afrika Mei 25 hadi 29 mwaka huu. Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa Idara ya Habari –MAELEZO, Bw. Assah Mwambene ,amesema maadhimisho hayo yanatarajiwa kufunguliwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Mhe. Bernard Membe. katika ufunguzi huo, Mkurugenzi ameeleza kuwa maadhimisho hayo yatatanguliwa na uzinduzi wa Mradi wa Nyaraka za Urithi wa Tanzania (TAHAP) ikiambatana na maonyesho ya picha ya kumbukumbu mbalimbali zinazoelezea ukombozi wa bara hilo. “Mradi wa nyaraka za urithi wa Tanzania unatarajia kuweka na kutunza kumbukumbu mbalimbali zinazohusu ushiriki wa Tanzania katika harakati za zinazohusu ukombozi wa nchi za Bara la Afrika” alisema Bw.Mwambene. Naye Mshauri Mkuu wa masuala ya Uhifadhi wa Nyaraka kutoka UNESCO, Bw.Philippe Roisse ameeleza namna shirika hilo lilivyojidhatiti katika kuhakikisha kumbukumbu hizo zitakavyohifadhiwa kwa usahihi na manufaa ya kizazi kijacho. “UNESCO imeazimia kusimamia suala hili la uhifadhi wa nyaraka za kumbukumbu Barani Afrika kuhusu harakati za ukombozi na hasa ukizingatia shirika hili limefikisha miaka 17 katika kutoa huduma” Alisema Bw. Roisse. Kwa Upande wa Mshauri Mwelekezi wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Dkt. Dinah Mbaga ameeleza kuwa mchango wa Tanzania katika ukombozi wa Afrika ni muhimu sana kwa kizazi cha sasa, na kuongeza kuwa ni muhimu kukumbushana. Aidha, Mshauri kutoka UNESCO Bw. Daniel Ndagala, ameongeza kwa kueleza kuwa mradi wa uhifadhi wa kumbukumbu mbalimbali na nyaraka za urithi ni chombo muhimu sana katika utekelezaji wa utambuzi wa juhudi za Tanzania kwa nchi za Bara la Afrika. Wiki ya maadhimisho ya Ukombozi wa Bara la Afrika utaenda sambamba na midahalo mbalimbali ikiwemo, mdahalo wa mchango wa vyama vya siasa katika harakati za ukombozi, Mchango wa wanajeshi katika harakati za ukombozi Mingine ni mchango wa wanawake katika harakati za ukombozi, mchango wa wasanii na watunzi na mchango wa vyombo vya habari yote ikilenga suala zima la harakati za ukombozi wa Bara la Afrika.
Maadhimisho hayo yanatarajiwa kufungwa na mgeni rasmi ambaye ni Waziri wa Habari,Vijana,Utamaduni naMichezo, Mhe. Dkt. Fenella Mukangara.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »