*MASHINDANO YA SHIMIWI YAFIKIA HATUA YA NUSU FAINALI MJINI MOROGORO

October 09, 2014


 Timu ya kuvuta kamba ya wanawake ya Ikulu wakiwavuta timu ya Wizara ya Kilimo, Ushirika na Chakula (hawapo pichani) wakati wa mashindano ya kuingia hatua ya nusu fainali mashindano ya SHIMIWI  leo mjini Morogoro ambapo Ikulu imefuzu kucheza hatua hiyo.
 Timu ya kuvuta kamba ya wanaume ya Ikulu wakiwavuta timu ya Wakala wa Hifadhi ya Chakula ya Taifa (NFRA- hawapo pichani) wakati wa mashindano ya kuingia hatua ya nusu fainali mashindano ya SHIMIWI leo mjini Morogoro ambapo Ikulu imefuzu kucheza hatua hiyo.
 Mshindi wa kwanza wa mchezo wa drafti wanaume Salumu Simba (kushoto) kutoka RAS Dodoma akichuana na mshindi wa tatu wa mchezo huo Ramadhani Mtenga (kulia)kutoka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wakati wa mashindano ya SHIMIWI leo mjini Morogoro.
 Mshindi wa kwanza wa mchezo wa drafti wanaume Salumu Simba (kulia) kutoka RAS Dodoma akichuana na mshindi wa tatu wa mchezo huo Dkt. Idris Lukindo (kushoto) wakati wa mashindano ya SHIMIWI leo mjini Morogoro.
 Baadhi ya watumishi wanaoshabikia mchezo wa drafti wakishuhudia pambano la kuwatafuta  washindi wa mcheo huo  leo katika kiwanja cha Jamhuri mjini Morogoro.
 Mchezaji wa timu ya mpira wa pete Ikulu Mwadawa Twalibu (GA) akimiliki mpira wakati wa mchezo wa robo fainali kati ya timu ya Ikulu na Bunge wa kumsaka mshindi atakayecheza nusu fainali, timu ya Ikulu imefuzu kwa kuwashinda timu ya Bunge kwa magoli 67 kwa 24.
 Wachezaji wa timu ya mpira wa miguu ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo (waliovalia sare ya bluu) wakisalimiana na wachezaji wa mchezo huo kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (waliovalia sare ya rangi ya machungwa) kabla ya mchezo wa robo fainali ambapo timu ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wameibuka washindi na kuingia nusu fainali katika mshindano ya SHIMIWI kwa kuifunga timu ya Ofisi ya Waziri Mkuu 1- 0.
 Timu ya mpira wa miguu ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo (kushoto) na timu ya Ofisi ya Waziri Mkuu (kulia) wakiomba dua kabla ya mchezo wa hatua ya robo fainali leo mjini Morogoro.
Baadhi ya watumishi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wakishangilia ushindi wa timu yao wa kuifunga timu ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa goli 1- 0 leo mjini Morogoro. Picha zote na Eleuteri Mangi- MAELEZO
**************************************
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Michuano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) imefikia hatua ya nusu fainali kwa michezo ya kuvuta kamba, mpira wa miguu na mpira wa pete kwenye mashindano yanayoendelea mjini Morogoro.

Katika mchezo wa kuvuta kamba timu za wanaume zilizoingia hatua hiyo ni Ikulu, Uchukuzi, Hazina na Mahakama wakati kwa upande wa wanawake timu zilizoingia hatua hiyo ni  Ikulu, Uchukuzi, Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na RAS Iringa.
Kwa upande wa mpira wa pete timu zilizofuzu ni Ikulu, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Wizara ya Uchukuzi na timu ya Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma.
Wakati huo huo, timu zilizokata tiketi ya kucheza hatua ya nusu fainali kwa mpira wa miguu ni Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Wizara ya Uchukuzi, Idara ya Mahakama na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Aidha, mchezo wa drafti umefikia ukingoni ambapo kwa wanaume bingwa wa mchezo huo imedchukuliwa na Salumu Simba kutoka timu ya RAS Dodoma, nafasi ya pili imekwenda kwa Dkt. Idris Lukindo kutoka Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) na nafasi ya tatu  imekwenda kwa Ramadhani Mtenga kutoka Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.

Kwa upande wa wanawake, Leocadia Mwang’ombe kutoka RAS Morogoro ameibuka bingwa kwa mchezo wa drafti huku nafasi ya pili imekwenda kwa Sophia Mpema kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na nafasi ya tatu imeenda kwa Madaraka Kabaka kutoka RAS Mwanza.

Mashindano hayo yanatarajiwa kufikia tamati siku ya Jumamosi Oktoba 11 mwaka huu na kuhusisha fainali za michezo mbalimbali ambazo zitachezwa kuhitimisha mashindano hayo ambapo yatafungwa rasmi kwa maandamano ya wanamichezo yatakayopokewa na Mgeni Rasmi atakayefunga michezo hiyo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »