UKOSEFU WA UZALENDO WASABABISHA KUTEKETEA KWA MSITU WA BOMBO WEST

May 05, 2014







Viongozi wa vijiji vya Bombo majimoto, Bombo Mtoni,Kijungumoto na Kwetonge vilivyopo kata ya Mashewa wamelalamikiwa kukosa uzalendo na kutuhumiwa kushirikiana na raia
  wanaosadikiwa kutoka nchi jirani ya Kenya kuvuna msitu wa asili wa miti ya Mkarambati unaozunguka vijiji hivyo kwa ajili ya kuchongea vinyago ambavyo huuzwa kwa Watalii  nchini Kenya.
Hayo yamebainishwa juzi na baadhi ya Wananchi wa vijiji hivyo waliokutwa katika msitu huo wakikusanya kuni wakati wa operesheni maalum iliyolenga kuwakamata waharibifu wa  msitu huo ambayo  iliendeshwa na kamati ya ulinzi na Usalama ya wilaya ya Korogwe kwa kushirikiana na wakala wa huduma za misitu Tanzania (TFS) na Halmashauri ya wilaya ya Korogwe.
Akizungumza na kamati ya ulinzi na usalama mkazi wa Bombo majimoto Shaban Said alisema kuwa mara nyingi wameshajaribu kutoa taarifa kuhusu uhalifu unaoendelea katika msitu huo ngazi ya kijiji lakini wamekuwa wakidhihakiwa kuwa wana vyeo gani serikalini hata walisemee suala hilo na hivyo imekuwa ngumu kwao kama Wananchi kukomesha ujangili huo wa msitu.
“Ili mhakikishe kuwa wanashirikiana ndiyo maana hata hawatembelei msitu mara kwa mara kwani wangeshachukua hatua kabla ya nyie kuja kutokana na uharibifu mkubwa uliofanyika humu ndani ya msitu, lakini sisi tukipeleka taarifa tunaulizwa tuna vyeo gani.” Alisema  Said.
 Kwa upande wake diwani wa kata ya Mashewa inayozungukwa na msitu huo Seif Hillaly,   alisema yeye binafsi na uongozi wa kata walishafanya doria katika msitu huo na kufanikiwa  kuwakamata wahalifu lakini hata hivyo  waliachiwa huru baada ya kulipa faini  kulingana na sheria za nchi,hivyo  alitoa rai kwa watunga Sheria kutunga Sheria kali zenye adhabu itakayowatofautisha wazawa na wageni ili kukomesha kabisa tabia ya raia wa nchi nyingine kuingia Tanzania na kuharibu misitu.
Mkuu wa wilaya ya Korogwe Mrisho Gambo ambaye ndiye mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya aliwaeleza waandishi wa habari kwamba wanafanya juhudi kama Serikali kwa ushirikiano na idara ya uhamiaji kuwatia nguvuni watu hao wanaosadikiwa kuingia nchini kinyemela na kufamya uhalifu huo na kwamba atatumia vyombo vya dola kuchunguza na kuwabaini viongozi wanaoshirikiana nao,pia  alitoa wito kwa Watanzania kuwa Wazalendo na kulinda nchi yao wao wenyewe kwani msitu huo unawafaidisha Watanzania hivyo kuathirika kwake ni hasara kwa Watanzania huku wakenya wakibaki salama na nchi yao.
Awali akitoa taswira ya uharibifu wa msitu huo, Afisa Misitu Msaidizi wa TFS Mbwelwa Kimweri alisema msitu huo wenye ukubwa wa hekta 3500 umekwishaharibiwa kwa asilimia 90 na sababu kubwa ikiwa ni ukosefu wa uzalendo kwani TFS na Halmashauri wameshatoa elimu ya kutosha kwa wanajamii hao kuhusu umuhimu wa msitu huo na jinsi ya kuuhifadhi huku wakiendelea kufaidika nao.
Operesheni hiyo ilifanikisha kukamatwa kwa mtu mmoja anayedhaniwa kuwa  raia wa Kenya ambaye alifikishwa katika kituo cha polisi wilayani Korogwe na hatua za awali za kufunguliwa mashtaka zimekwishafanyika. 
Kamati ya Ulinzi na Usalama ikijipanga katika makundi kuingia Msituni kusaka waharibifu wa Msitu.
 
Safari kuelekea Msituni
Kikosi kazi kilipovamia kambi ya Majangili hao wa Msitu na kukuta wametoroka,hata hivyo kikosi hicho kilimpata mmoja wao ambaye anashikiliwa na jeshi la Polisi wilayani Korogwe
Mgambo wakitoka na Shehena ya vinyago Msituni vilivyokuwa vikiendelea na matengenezo kabla ya msitu kuvamiwa na Kamati ya Ulinzi.
Kamati ya Ulinzi na Usalama ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Korogwe(mwenye shati jekundu) ikiwahoji baadhi ya Watanzania waliokutwa  msituni kuhusu uharibifu unaoendelea katika msitu huo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »