RC TANGA AONGOZA KUTUNDIKA MIZINGA YA NYUKI KOROGWE.

May 01, 2014




Mkuu wa mkoa wa Tanga Luteni Mstaafu Chiku Gallawa jana aliongoza mamia ya wakaazi wa kijiji cha Kwamzindawa kilichopo kata ya Mnyuzi, Korogwe vijijini kutundika mizinga ya nyuki pembezoni mwa milima inayopakana na hifadhi ya asili ya Amani katika
kuadhimisha siku ya kutundika mizinga nchini ambapo kitaifa shughuli hiyo ilifanyika mkoani Katavi .
Maadhimisho hayo ya kimkoa yaliyoratibiwa na Wakala wa misitu Tanzania (TFC) kwa ushirikiano na Halmashauri ya wilaya ya Korogwe yalifanikisha utundikaji wa mizinga 45 iliyotolewa na TFC shughuli iliyofanywa kwa umakini na viongozi mbalimbali kwa ushirikiano na Wananchi wakiongozwa na Mkuu wa mkoa.
Katika hotuba yake mara baada ya zoezi hilo Mkuu wa mkoa alikipongeza kikundi cha ufugaji nyuki cha Malkia cha kijijini hapo ambacho ndiyo kimekuwa chachu ya kuendeleza ufugaji nyuki  waliouanzisha kwa jitihada zao binafsi na baadaye kupatiwa msaada wa vifaa vya kufugia na kurinia asali ikiwemo mizinga hiyo.
Gallawa aliongeza kuwa ni vyema kikundi hicho kikajenga mtandao wa ulinzi na utunzaji wa mazingira ili kuwavutia zaidi nyuki kuingia katika mizinga hiyo na kumwagiza Mkurugenzi Mtendaji kuwaandalia mafunzo ya kitaalamu wafugaji hao ili ufugaji huo ukue na kufikisha mizinga 100 hatimaye uweze kuwa na tija kwenye uchumi endelevu.
“Agizo la mkoa ni kila kikundi cha ufugaji nyuki kuwa na mizinga 100 hapo ndipo mnaweza kuona tija ya ufugaji nyuki ambao mtaji na uwekezaji wake ni mdogo,lakini faida ni kubwa.” Aliongeza Gallawa.
Kadhalika aliwashauri wafugaji hao kulima zao la alizeti ambalo huvutia nyuki hivyo itapelekea kupata faida mara zaidi hatimaye kufanikisha kipaumbele cha mkoa cha kumfanya mkazi wa Tanga kuongeza pato hadi kufikia  Tsh ml 1.5 kwa mwaka.
Awali katika risala yao iliyosomwa na Fatuma Kipara, kikundi cha ufugaji nyuki cha Malkia walimweleza Mkuu wa mkoa kuwa wanakabiliwa na changamoto ya uhaba wa wataalamu wa sekta ya nyuki jambo linalowaathiri kwa kuwa hawatembelewi mara kwa mara.
Naye Afisa nyuki wa wilaya Vicent Mhezi, akisoma taarifa ya ufugaji nyuki alisema Wilaya ina vikundi vya ufugaji wa nyuki 38,vyenye wanachama 602, vikundi  vilivyosajiliwa ni 13 na kuongeza kuwa Korogwe imefanikiwa kuanzisha  ofisi ya usindikaji wa Mazao ya Nyuki iliyopo Bungu,ambapo kwa mwaka 2013,wamefanikiwa kusindika asali lita 500 yenye thamani ya Tshs 5,000,000/-
Diwani wa kata ya Mnyuzi Rajab Muhidin akitoa maelezo ya awali kuhusu kata yake kwa  Mkuu wa Mkoa.

Afisa Nyuki wilaya Vicent Mhezi akieleza teknolojia iliyotumika kutengeneza mizinga hiyo kwa Mkuu wa Mkoa

 Shughuli ya kutundika mizinga ikiendelea mara baada ya Mkuu wa Mkoa kuzindua zoezi hilo.
 Mkuu wa Magereza Mkoa wa Tanga  Edith Mallya akiungana na Mkuu wa Mkoa katika kutundika mizinga
 Baada ya "tundikatundika" , tuliacha eneo hilo likionekana namna hii
 Mkuu wa Mkoa wa Tanga Luten Mstaafu Chiku Gallawa akizungumza na Wananchi wa kijiji cha Mzindawa
 Wananchi wa Mzindawa walioshiriki tukio hilo wakimsikiliza Mh.Mkuu wa Mkoa
  Mwisho Mkuu wa Mkoa alihitimisha shughuli hiyo kwa kutembelea banda la maonesho la kikundi cha Malkia kujionea  mazao yatokanayo na Nyuki

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »