WAFUGAJI KILINDI WACHOSHWA NA MATUKIO YA KIKATILI YA MIFUGO YAO

November 29, 2013
Na Elizabeth Kilindi,Kilindi.

MVUTANO   unaoashiria mapigano na mauaji kwa mara nyingine tena unafukuta baina ya wakulima na wafugaji  Wilayani Kilindi Mkoani Tanga baada ya wafugaji kuchoshwa na  matukio ya  kikatili ya mifugo yao kuuawa  kwa kuwekewa  sumu kwenye malisho na  kufia porini.


Tukio hilo la kusikitisha lilitokea  juzi katika kitongoji cha Kipaluke, Kijiji cha Kigwama, Kata ya Msanja Tarafa ya Mswaki Wilayani Kilindi  ambako ng'ombe nane  walifia porini  kati ya 14 waliyodaiwa  kula majani yenye sumu.



Wakizungumzia  tukio hilo la kinyama, jamii ya wafugaji walilalamikia kuchoshwa na maisha ya kunyanyaswa na kufanyiwa vitendo vya ukiukwaji wa haki  na wakulima ambao wanalindwa na kupewa baraka  na baadhi ya viongozi.

Wilaya ya Kilindi imekuwa ikikabiliwa na machafuko ya mara kwa mara na kusababisha vifo na majeruhi kwa kile kilichokuwa kikielezwa kuwa ni viongozi kutokuwa na tahadhari ya kushughulikia migogoro mapema hadi yanapotokea maafa.

  

Wakizungumza katika mkutano wa dharula wa wafugaji hao wa jamii ya kimasai uliyofanyika jana katika kitongoji cha Kipaluke,wafugaji hao wakiongozwa na Philipo  Ngakuru mwenyekiti wa serikali ya  kitongoji cha Kipaluke na Marko  Issaya kiongozi wa  kijadi  wa jamii hiyo (Raigwanani), walisema hali ilipofikia watalazimika kuingia msituni kufanya vita.


katika mkutano huo viongozi hao walichukua jukumu la kuzuia machafuko hayo wakiaahidi  jamii hiyo kwamba watafuatilia  ngazi za juu za serikali ili  kupatiwa ufumbuzi wa matukio hayo na hatimaye haki itendeke  kwa njia ya amani  ambayo ni utamaduni wa  taifa letu.


Wakati  wakizungumza kwenye mkutano huo walidai kuwa tatizo lao na wakulima linastawishwa na vyombo husika kushindwa kusimamia makubaliano ya kisheria juu ya matumizi halali ya eneo lenye mgogoro na kwamba hata pale wanapoomba serikali kuingilia kati hakuna kinachotendeka.


Naye Thomas Tinno aliitaka serikali kutokaa kimya na badala yake itoe tamko kuhusiana na kitendo cha kumwagwa sugu kwenye malisho ya wanyama na kusababisha vifo  na kueleza kuwa kufanya hivyo kutazuia  maamuzi ya hasira  ya kulipa kisasi yanayoweza kuchukuliwa na wahanga.


“Mimi naiomba serikali kupitia nyinyi waandishi wa habari ichukue hatua kwani waliyohusika na tukio hili wanafahamika isingoje wahanga wachukue hatua, kwani kukaa kimya itakuwa imebariki machafuko” alisema Tinno.


Abraham Ngakuru  alisema kuwa kutokana na tukio hili, jamii ya wafugaji imetangaza mgogoro na kwamba kama si busara za viongozi wao wa kijadi amani ingetoweka tangu pale serikali ilipojidhihirisha kusimama na kutetea upande mmoja wa wakulima hao.


Aidha Paulo Sinion  alidai kuwa siku ya tukio majira ya saa tisa  jioni  walipata taarifa kutoka kwa mchungaji kuwa ng’ombe zinaanguka na walipofika walizikuta 14  zikigaagaa chini na kwamba sita zilinusurika kufa baada ya kupewa maziwa na sukari ambapo nane kati ya hizo zilikufa hapohapo.


Akitoa  tamko la mkutano huo, Philipo ambaye ni mwenyekiti wa serikali ya Kitongoji hicho, alisema kuwa tatizo la migogoro ya wakulima na wafugaji limekuwa sugu na kueleza bayana kuwa unachochewa na uongozi wa Kata na baadhi ya serikali za vijiji.


Kwamujibu wa Philipo ni kuwa  viongozi wa Kata kwa kushirikiana na wa vijiji wamekuwa na utamaduni wa kuwanyanyasa wafugaji kwa vitendo mbalimbali kama vile kuunda kikundi cha vijana  kwa ajili ya kuhujumu mifugo  yao.


Alisema kuwa  kutokana na hali ilivyo ni lazima serikali ya Wilaya na Mkoa iingilie kati kukomesha unyanyasaji huo unaofanywa kwa lengo la kuwanufaisha wachache ili kuzuia vurugu zinazoweza kutokea katika maeneo hayo.


Alishangaa uongozi wa Kata kutolishughulikia tatizo hilo kwa madai kuwa lipo wazi kwani sehemu yenye mgogoro inayotumiwa kwa ufugaji  ilitengwa na serikali tangu mwaka 1998  kuwa eneo la malisho na kuhoji sababu za  kutoheshimiwa.


Kiongozi wa jamii hiyo, Raigwanani Issaya yeye alikitaka Chama cha Mapinduzim CCM kuingilia kati mgogoro huo kwani wafugaji hao  wananyanyashwa na  watendaji wake  na hawapati haki licha ya kuwa ni wafuasi wa Chama hicho.


Aidha alienda mbali zaidi kwa kukitaka Chama hicho kumshauri Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya ya Kilindi kumuondoa afisa mtendaji wa Kata ya Msanja akieleza kuwa ni mzigo na chanzo cha unyanyasaji ndani ya Kata hiyo.


Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, Seleman Liwowa  alidai hakuwa na taarifa ya tukio hilo na kuahidi kufuatilia ili kubaini na kuchukua hatua zinazostahili na kwamba ni kosa la jinai kwa mtu kutumia vibaya madaraka yake jambo ambalo pia ni kinyume na uwepo wa kiongozi husika.


“Hapana  Mimi sina taarifa hizo ndiyo unanambia sasa hivi, japo kuwa sipo Wilayani, nipo Mtwara…..nitawasiliana na (OCD) Mkuu wa polisi Wilaya afuatilie kwa kuwa wewe unanieleza tofauti na taarifa nilizokuwa nazo” Liwowa alisema.


Share this

Related Posts

Previous
Next Post »