NUNDU:AWAASA WAISLAM MKOANI TANGA KUENDELEA KUTENDA MEMA.

August 10, 2013

Na Oscar Assenga, Tanga.
MBUNGE wa Jimbo la Tanga, Omari Nundu amewataka waislamu mkoani kuendelea kudumisha amani iliyopo hapa nchini pamoja na kuilinda kwa kufanya mambo mema yanayompendeza mwenyezi mungu ikiwemo kuacha kufanya yale yote yaliyokatazwa.

Nundu alitoa kauli hiyo wakati akitoa hotuba yake kwenye baraza la Iddi lililofanyika ukumbi wa shule ya sekondari Jumuiya mkoani Tanga ambalo lilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa dini  akiwemo Meya wa Jiji la Tanga Omari Guledi ambapo alisema waislamu hawana budi kuendelea kutenda mema ili kuweza kupata dhawabu.

Alisema waislamu wanapaswa kuwa na tahadhari kwa kuepuka kuwa na vikundi ambavyo vinalenga kuleta chokochoko ya kidini kwenye jamii zinazowazunguka kwani kufanya hivyo kunapelekea uvunjifu wa amani badala yake waishi kwa kutii na kuheshimu sheria zilizopo hapa nchini.

Mbunge huyo alitumia nafasi hiyo kuwaasa waislamu kutilia mkazo elimu ya dunia kwa sababu ugunduzi mwingi unaotumika hivi sasa umeelemea sana kwenye maandiko yatokanayo na kuruhan hivyo kuwataka kuzingatia suala hilo kiumakini. 

  “Ndugu zangu waislamu wenzangu tumemaliza mwenye mtukufu wa ramadhani kwa amani,basi nawashauri tuendeleze sifa tulizokuwa nazo kwenye mwezi huo kwa kuacha kufanya maovu badala yake tuelekeze nguvu zetu kwenye kutenda mambo mema “Alisema Nundu.

Aidha aliwataka kuepuka mivurugano ambayo haina tija kwenye jamii zao kwa kuishi kwa amani ikiwamo kushirikiana  na watu wengine malengo yakiwa ni kutimiza nguzo kuu ya uislamu ya kufanya ibada mara kwa mara ili kuweza kuwa karibu na mwenyezi mungu.

Awali akizungumza katika baraza hilo,Sheikh wa Mkoa wa Tanga,Ally Juma Luwuchu alisisitiza suala la waislamu kuendelea kutenda mambo mema  ikiwemo kuendelea kuonyesha ustawi mzuri kwa jamii kitu kitakachopolekea kupata radhi za Mwenyezi Mungu na kujenga umoja ulio imara katika uislamu hapa nchini

Sheikh Luwuchu aliwaomba  waslam kuondoa tofauti zao za kiimani na wawe wamoja , wasikivu kwa viongozi wao  wakuu wa kidini hasa inapofikia wakati wa kupata tamko kutoka kwa viongozi hao kitu kitakachowapelekea kuonyesha umoja wetu na mshikamano katika maswala yote yanayohusu uislam.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »