Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts

MSIGWA AIPONGEZA TBS KWA KUHAMASISHA MICHEZO MAENEO YA KAZI

September 15, 2024 Add Comment

 



NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM
KATIBU Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa amezitaka taasisi mbalimbali za serikali kushiriki na kufanya mabonanza ya michezo ambapo itasaidia kuimarisha afya za wafanyakazi na kuleta manufaa kwa taifa kwa kuongeza idadi ya wachezaji na wawakilishi katika mashindano ya kimataifa.


Rai hiyo imetolewa Septemba14,2024 Jijini Dar es salaam alipokuwa katika Bonanza la michezo la watumishi lililoandaliwa na Shirika la viwango Tanzania (TBS).


Msigwa ameipongeza TBS kwa kuunga juhudi za Serikali ya awamu ya sita kwa kuhamasisha michezo maeneo ya kazi kwa kutengeneza bajeti na kuruhusu wafanya kazi kushiriki katika michezo ili kuimarisha afya na kujenga mahusiano mazuri kazini jambo ambalo huoongeza ubunifu na ufanisi maeneo ya kazi.


Ameongeza kwa kuiasa Menejimenti ya TBS kutenga bajeti ya kujenga viwanja bora maeneo ya kazi ili kuwawekea wafanyakazi mazingira bora wakati wa kushiriki michezo mbali mbali.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi TBS Prof. Othman Chande amesema walianzisha Bonanza hilo miaka mitano iliyopita ambapo limelenga kuimarisha afya za wafanyakazi pamoja na kujenga umoja.


"Wachezaji wanacheza kama timu mbili tofauti lakini ni walewale wakishamaliza mchezo wanaenda pamoja inaongeza urafiki". Amesema


Aidha Prof.Chande ameeleza kuwa mashindano hayo ya mabonanza yatachangia kuwa na machaguo mengi ya wachezaji watakao wakilisha katika mashindano ya kimataifa.


Nae Mwenyekiti wa Michezo Shirika la viwango Tanzania (TBS) Nyabutwenza Methusela ameeleza faida za bonanza hilo ambapo amesema kuwa linasaidia watumishi kuondokana na changamoto ya afya ya akili kwa kujikita zaidi katika michezo ambayo inawaondolea msongo wa mawazo na kuongeza ufanisi wanaporudi kufanya kazi.


"Kupitia michezo afya ya akili na mwili inaboreshwa, wafanyakazi wanakuwa wachapakazi kwasababu wameboresha afya zao za akili pamoja na mwili". Nyabutwenza ameeleza.



WIZARA YA MALIASILI YAZIDI KUWA TISHIO KWENYE MICHEZO YA KIRAFIKI KUELEKEA SHIMIWI 2024

September 07, 2024 Add Comment

Na. Ashrack Miraji Matukio Daima - Dodoma
.
Wizara ya Maliasili na Utalii imeibuka mshindi kwenye michezo mitatu ya kirafiki iliyochezwa leo kwenye Viwanja vya Vijana vilivyopo Jijini Dodoma ikiwa ni maandalizi ya  kuelekea Mashindano ya SHIMIWI 2024 yanayotarajiwa kuanza  Septemba 18 mwaka huu  Mkoani Morogoro 

Katika michezo hiyo Wizara ya Maliasili imejinyakulia ushindi kwenye mchezo wa Kamba ( Ke) dhidi ya Timu ya Wizara ya Madini  kwa goli mbili kwa nunge, Kamba (Me) imeibuka  mshindi kwa goli mbili kwa moja dhidi ya Timu ya  Wizara ya Madini huku kwa upande wa Netboli (Ke) ikiichakaza Timu ya CRDB kwa goli 26 kwa 21

Akizungumza mara baada ya ushindi huo Mkurugenzi wa Idara  Sera na Mipango wa wizara hiyo  ambaye pia ni moja ya walezi wa Timu hiyo, Bw. Abdallah Mvungi ameipongeza Timu hiyo kwa kazi kubwa waliyofanya ya kuiletea Wizara ushindi huku akiitaka Timu hiyo kuongeza jitihada za kufanya  mazoezi ili kuiletea Wizara ushindi katika mashindano ya SHIMIWI 2024

"Wachezaji wetu, tunawapongeza sana kwa ushindi huu, Kila siku tunaona mabadiliko, mnacheza kwa moyo na ari kubwa sana, hongereni sana. Sisi tutaendelea kuwapa hamasa na kuwaunga mkono, endeleeni kupambana ili tutakapoenda kwenye mashindano tuiletee wizara Ushindi" Amesema Mvungi

Kwa upande wake Kocha wa Timu ya Kamba (Ke na  Me) wa Wizara hiyo , Bw. Abunu Issa  amewapongeza Wachezaji hao huku akiwasisitizia kuendelea kujitoa na kuhakikisha wanashinda michezo ya kirafiki itayofuata hapo kesho

Ameongeza kuwa, michezo ya kirafiki inayochezwa ni muhimu kwa Timu hizo kwani inawajengea ari ya kupambana lakini pia, inazisaidia timu hizo kujipima  kwa ajili ya maandalizi ya Mashindano ya SHIMIWI yanayotarajiwa kuanza  hivi karibuni

" Nanachoangalia katika michezo hii ya kirafiki ni hali ya wachezaji wetu  kama wanapokea kile ninachoelekeza na kufundisha, Hivyo, hii michezo ni kipimo tosha cha mimi kufahamu kama maelekezo yangu yanafuatwa  na kutekelezwa ipasavyo" Amesema Abunu

Kulekea Mashindano ya SHIMIWI 2024, Wizara ya Maliasili na Utalii inatarajiwa kushiriki michezo kadhaa ya kujipima uwezo,  ambapo hapo kesho Wizara inatarajiwa kuchezo Mchezo wa Kirafiki kwenye mchezo wa Netboli pamoja na Kamba (Me) dhidi ya Timu ya  Wizara ya Utamduni sanaa na Michezo


 

RIADHA TANGA KUMPA USHIRIKIANO MUANDAAJI WA MASHINDANO YA TANGA CITY MARATHON

August 27, 2024 Add Comment



Mwenyekiti wa Chama cha Riadha Mkoa wa Tanga Sophia Wakati akizungumza 



Na Oscar Assenga, Tanga.

CHAMA cha Riadhaa Mkoa wa Tanga (RT) kimesema kwamba kitampa ushirikiano wa kutosha muandaaji wa Mashindano ya Riadhaa ya Tanga City Marathon ili kuweza kuondoa changamoto zilizojitokeza msimu uliopita na yaweza kuwa na tija na mafanikio makubwa.

Hayo yalisemwa leo na Mwenyekiti wa Chama cha Riadha (RT) Mkoa wa Tanga Sophia Wakati alipokuwa akizungumza na vyombo bya habari kuhusu namna walivyojipanga kuhakikisha wanampa ushirikiano wa kutosha muadaaji huyo ili mashindano hayo yaweze kufanyika kwa ufanisi.

Alisema pia kuweza kufanyika vizuri kwa kufuata taratibu zote za Mashindano hayo kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kupitia Afisa Michezo Mkoa

“Mbio hizi za Tanga City Marathon ni mashindano muhimu kwa mchezo wa Riadha mkoani hapa na kwa sasa tumeyaingiza kwenye kalenda ya Mkoa na sasa yatakuwa yakifanyika kila mwaka na sisi RT kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga tutatoa ushirikiano wa kutosha kwa waandaaji”Alisema Sophia Wakati.

Mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika Septemba 22 mwaka huu ambapo yataanzia kwenye Hotel ya Tanga Beach Resort na kuzunguka maeneo mbalimbali Jijini Tanga na kuishia hapo huku yakishirikisha wakimbiaji katika makundi matatu ya Kilomita 21,10 na 5 za kujifurahisha.




HOME GUARD FC, SMALL PRISON ZAAGA MASHINDANO ULINZI CUP TANGA

August 21, 2024 Add Comment

Mratibu wa Mashindano ya Ulinzi Cup Sophia Wakati akisistiza jambo kwa wachezaji wa timu za Small Prison na Chote FC kabla ya kuanza mchezo wao wa Michuano hiyo

Na Oscar Assenga, TANGA.

TIMU za soka Small Prison na Home Guard zimeaga Mashindano ya Ulinzi Cup baada ya kila mmoja kufungwa katika mchezo wa hatua ya mtoano inayoendelea kwenye viwanja vya Ziwani Pongwe Jijini Tanga.

Mashindano hayo yanaratibiwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Tanga yakiwa na lengo la kutoa elimu kwa vijana kujiepusha na vitendo vya uhalifu katika jamii wanazoishi ikiwemo kuwa mabalozi wa amani kwenye maeneo yao

Katika mchezo wa awali wa ufunguzi wa mashindano hayo timu ya soka TFC waliigaragaza Home Guard bao 1-0 bao ambalo lilifungwa na Mohamed Saidi dakika ya 5 hya mchezo huo ambao ulikuwa na upinzani.


Huku mchezo wa pili uliochezwa Agosti 21 mwaka huu timu ya Chote FC waliweza kuwapigisha kwata maafande wa Jeshi la Magereza Small Prison bao 1-0 ambalo lilifungwa na Boniface Majere dakika ya 47.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mashindano hayo,Diwani wa Kata ya Pongwe (CCM) Mbaraka Sadi alilipongeza Jeshi la Polisi kwa kazi kubwa anayoifanya kwa kuhakikisha Jeshi la Polisi linakuwa karibu na Jamii jambo ambalo ni muhimu katika kuhakikisha kuimarisha ulinzi.

Mbaraka alisema kwamba kufanyika kwa mashindano hayo katika maeneo mbalimbali yanasaidia na kuwawezesha vijana kuweza kuyatumia kama njia muhimu ya ajira,kujenga afya pamoja na kusaidia kuwaondoa vijana kwenye masuala ya uhalifu na dawa za kulevya na wanaamini mashindan hayo yatakuwa chachu kubwa ya kuinua vipaji vya wachezaji.

Naye kwa upande wake Mratibu wa Mashindano hayo Sophia Wakati alivitaka vilabu vinavyoshiriki kwenye mashindano hayo kuhakikisha wanazingatia sheria 17 za mpira wa miguuu zilizowekwa ikiwemo kuacha kuwachukia waamuzi.

“Lengo la Mashindano hayo ni kujenga undugu baina ya Jeshi la Polisi na Jamii lengo kujenga urafiki msijengeane chuki hakikisheni mnacheza kwa kuzingatia nidhamu ambayo itakuwa chachu ya mafanikio kwenye jambo lolote lile lakini msiwachukie waamuzi kutokana na kwamba wakati mwengine kunakuwa na makosa ya kibinadamu”Alisema

DKT.BITEKO APONGEZA JITIHADA ZA CRDB BANK MARATHON KUSAIDIA WATOTO, WAKINA MAMA NA VIJANA

August 19, 2024 Add Comment

 

 
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko (katikati), akiwa ameongozana na Waziri wa Michezo, Dkt. Damas Ndumbaro (watatu kulia), Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila (wapili kulia), Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Benki ya CRDB, Dkt. Ally Laay (watatu kushoto), Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB Bank Foundation, Martin Warioba (kulia), Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela (wanne kushoto) pamoja na viongozi wengine wakianza mbio za kilometa tano katika kilele cha msimu wa tano wa CRDB Bank Marathon zilizofanyika viwanja vya farasi 'The Green Grounds' jijini Dar es salaam Agosti 18, 2024 na kuhudhuriwa na washiriki zaidi ya 8,000.
Tanzania 18 Agosti 2024 – Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Dotto Biteko ameipongeza taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kuendelea kuandaa mbio za CRDB Bank Marathon ambazo zimejielekeza katika kusaidia jitihada za serikali kuboresha sekta ya afya, kusaidia wenye uhitaji, pamoja na kukuza ustawi wa jamii.

Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo wakati wa kilele cha msimu wa tano wa CRDB Bank Marathon ambapo Shilingi Milioni 350 zimekusanywa kwa ajili ya kusaidia watoto wenye uhitaji wa upasuaji wa moyo Taasisi ya Jakaya Kikwete (JKCI), huduma za afya kwa wakinamama wenye ujauzito hatarishi hospitali ya CCBRT, na uwezeshaji wa vijana.
“Niwapongeze kwa kuendelea kusaidia matibabu ya wakinamama na watoto wetu. Wakinamama ndio wamebeba uchumi wa Taifa letu. Lakini pia wakinama ndio waangalizi wa familia zetu hususani watoto. Hivyo ukiimarisha afya ya mama na watoto umeimarisha afya ya Taifa,” amesema Dkt. Biteko huku akisema Serikali na Watanzania wanaona jitihada hizo zinazofanywa na Benki ya CRDB kupitia CRDB Bank Foundation.
Akizungumza Waziri wa Sanaa, Utamaduni, na Michezo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema CRDB Bank Marathon imesaidia kwa kiasi kikubwa kuchochea ari ya michezo nchini. Dkt. Ndumbaro amesema mbio hizo zimekuwa jukwaa muhimu kwa wanariadha nchini kuonyesha vipaji vyao katika jukwaa la kimataifa kwani mbio hizo zimesajiliwa kimataifa na Shirikisho la Upimaji Mbio Kimataifa (AIMS) na Shirikisho la Riadha Duniani (World Athletic).

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela amesema katika kiasi cha fedha kilichokusanywa; shilingi milioni 100 zitakwenda kusaidia watoto wenye uhitaji wa upasuaji wa moyo Taasisi ya Jakaya Kikwete (JKCI), Shilingi Milioni 100 kusaidia huduma za afya kwa wakinamama wenye ujauzito hatarishi hospitali ya CCBRT, na Shilingi Milioni 150 uwezeshaji wa vijana.
Katika mbio hizo zawadi za jumla ya Shilingi Milioni 98.7 zimetolewa kwa washindi 60 wa mbio za kilometa 42, 21, 10, 5, pamoja na mbio za baiskeli za kilometa 65. Mwenyekiti wa Bodi ya CRDB Bank Foundation, Martin Warioba amesema jumla ya washiriki waliojiandikisha mwaka huu ni 8,000 huku akisema lengo la mwaka kesho ni kupata washiriki 10,000 Tanzania, huku malengo ya washiriki Burundi na DRC wakiwa ni 3,000 kila nchi.

Mbio hizi zilizofanyika Dar es Salaam ni za tatu baada ya zile zilizofanyika nchini DRC, na Burundi. Nchini DRC mbio hizo zilifanyika tarehe 4 Agosti ambapo Dola za Marekani 50,000 zilikusanywa kusaidia kuboresha huduma za afya kwa watoto hospitali ya Jason Sendwe jijini Lubumbashi. Kwa upande wa nchini Burundi, mbio hizo zilifanyika tarehe 11 Agosti ambapo Faranga za Burundi Milioni 120 zilikusanywa kusaidia wahanga wa mafuriko mkoa wa Gatumba jijini Bujumbura.

Akizungumza wakati wa kutangaza matokeo ya mbio hizo Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa amewapongeza washindi wa mbio hizo, na kuwashukuru washirika wa mbio hizo wakiwemo kampuni za bima Sanlam na Alliance Life ambao ni washirika wakuu wa mbio hizo. “Tunawashukuru sana washirika wetu na wakimbiaji wote kwa kuungana nasi katika juhudi za kusambaza tabasamu kwa watoto walioathirika,” amesema Mwambapa.

Washindi wa mbio hizo Kilometa 42 upande wa wanawake ni Joyloyce Kemuma kutoka Kenya, upande wa wanaume mshindi ni Moses Nengichi kutoka Kenya. Kilometa 21 upande wa wanawake ni Sara Makera kutoka Tanzania, na upande wa wanaume ni Joseph Panga kutoka Tanzania. Kilometa 10 upande wa wanawake ni Hamida Nasor kutoka Tanzania, na upande wa wanaume ni Mao Hindo Ako kutoka Tanzania.
Sara Makera mshindi wa mbio za Kilometa 21 upande wa wanawake ameeleza furaha yake kushiriki katika mbio hizo na kusema kuwa ushindi wake ni sehemu ya kusaida matibabu ya watoto wenye matatizo ya moyo na  matibabu ya wakinamama wenye ujauzito hatarishi hospitali ya CCBRT.

 “Mimi kama mwanamke ninajisikia faraja kubwa kushiriki kusambaza tabasamu kwa watoto na wakinamama. Watu wanapaswa kufahamu kuwa afya bora ni haki ya kila mtoro na wakinamama pia hawastahili kupoteza maisha wakati wa kujifungua. Tunawashukuru CRDB Bank Foundation kwa kutuunganisha pamoja katika juhudi hizi,” amesema.