Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

WAZIRI NDEJEMBI ATOA ONYO KWA MKANDARASI ANAYETEKELEZA MRADI WA SONGEA–TUNDURU–MASASI

July 22, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu - Tunduru, Ruvuma


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameonesha kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Masasi kupitia Tunduru na kuagiza mkandarasi kuongeza juhudi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya mradi huo leo Julai 22, 2026, Mhe. Ndejembi amesema Serikali haitakuwa tayari kuona miradi ya kimkakati inayogusa maisha ya wananchi ikicheleweshwa bila sababu za msingi.


Amesema mradi huo ni miongoni mwa miradi muhimu ya Sekta ya Nishati inayopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutokana na mchango wake katika kuimarisha upatikanaji wa umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Kusini.


“Maendeleo ya mradi huu hayaridhishi ukilinganisha na muda uliopita tangu utekelezaji wake uanze. Serikali inatarajia kuona kasi kubwa zaidi ya utekelezaji katika kipindi kilichobaki. Nimemuagiza Katibu Mkuu kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo haya na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa iwapo hakutakuwa na maboresho yanayoonekana,” amesema Mhe. Ndejembi.


Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nyasa, Mhe. Boniface Magiri, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, amesema Mkoa utaendelea kushirikiana na Serikali Kuu katika kufuatilia utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati.


Naye Mhe. Sikudhani Chikambo kwa niaba ya wabunge wa Mkoa wa Ruvuma, viongozi hao wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya umeme ambayo itachochea ukuaji wa uchumi, uwekezaji na kuboresha huduma za kijamii katika maeneo ya Kusini mwa Tanzania.


Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea kupitia Tunduru hadi Masasi unatekelezwa na Mkandarasi Kalpataru Power kutoka India. Mradi huo unatarajiwa kuiunganisha Mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye Gridi ya Taifa pamoja na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Wilaya ya Tunduru na maeneo jirani.



WANAHABARI NI WASHIRIKA MUHIMU WA KUHAMASISHA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

July 15, 2026 Add Comment




Naibu Waziri wa Nishati amesema vyombo vya habari na maafisa mawasiliano Serikalini ni washirika muhimu wa maendeleo ya Taifa kutokana na nafasi yao ya kufikisha taarifa sahihi kwa wananchi na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia kupitia habari, vipindi vya redio na televisheni pamoja na majukwaa ya kidijitali.


Hayo ameyabainisha leo Julai 14, 2026 wakati akifungua Warsha ya Kuwajengea Uwezo Waandishi wa Habari na Maafisa Mawasiliano Serikalini kutoka katika Wizara na Taasisi  kuhusu Uandishi na Uhamasishaji wa Masuala ya Nishati Safi ya Kupikia, inayofanyika katika ukumbi wa Morena hoteli mkoani Morogoro.

Amesema vyombo vya habari si wasambazaji wa taarifa pekee bali ni washirika muhimu wa maendeleo ya Taifa kwa kutoa taarifa sahihi huku akibainisha kuwa kupitia habari, vipindi vya redio na televisheni, makala pamoja na maudhui ya kidijitali, wanahabari wana nafasi kubwa ya kujenga uelewa wa wananchi, kuondoa dhana potofu na kuhamasisha mabadiliko chanya ya tabia kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia  kwani katika zama za mawasiliano ya kidijitali, taarifa moja sahihi inaweza kuwafikia mamilioni ya wananchi ndani ya muda mfupi na kuleta mabadiliko makubwa katika jamii.

Amefafanua kuwa, taarifa zisizo sahihi zinaweza kusababisha upotoshaji na kuchelewesha utekelezaji wa ajenda muhimu za maendeleo akimnukuu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) uliofanyika jijini Arusha, amesema watu wanaweza kushiriki kubomoa Tanzania, lakini hawawezi kusaidia kuijenga hivyo amesisitiza kuwa wanahabari wana wajibu wa kutumia kalamu na keybord zao kuandika habari zenye ukweli, zenye kujenga matumaini na kuunga mkono juhudi za maendeleo ya Taifa badala ya taarifa zinazoweza kupotosha wananchi.

Aidha Mhe. Salome ameeleza kuwa, matarajio ya Serikali ni kuwa mafunzo hayo yatawaongezea washiriki maarifa na ujuzi wa kuandaa habari zenye usahihi, ushahidi na weledi wa hali ya juu, pamoja na kuandaa maudhui yanayoonesha mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia, ubunifu wa sekta binafsi na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa sekta hiyo.

Ameongeza kuwa warsha hiyo itawajengea uwezo washiriki kuhusu sera, mikakati na mwelekeo wa Serikali katika sekta ya nishati safi ya kupikia, matumizi sahihi ya takwimu pamoja na namna bora ya kuripoti kuhusu teknolojia mbalimbali zinazopatikana nchini ili kuandaa taarifa zenye ubora na zinazojenga uelewa wa wananchi.


Aidha, amewataka washiriki kutumia kikamilifu fursa ya mafunzo hayo kujenga ushirikiano kati ya Wizara ya Nishati, Idara ya Habari MAELEZO, washirika wa maendeleo, sekta binafsi na vyombo vya habari, akisisitiza kuwa mawasiliano sahihi ni nguzo muhimu ya kufanikisha ajenda ya nishati safi ya kupikia na kufikia lengo la asilimia 80 ya matumizi ifikapo mwaka 2034.



NAIBU WAZIRI SALOME AWASILI MOROGORO KUFUNGUA WARSHA YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

July 15, 2026 Add Comment

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Mussa Kilakala, akiwasili katika Ukumbi wa Morena Hotel mkoani Morogoro kwa ajili ya kufungua warsha ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari pamoja na Maafisa Mawasiliano wa Serikali kuhusu uandishi na uhamasishaji wa masuala ya Nishati Safi ya Kupikia.

Warsha hiyo imeandaliwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF), kupitia Mradi wa CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya.

Katika ziara hiyo, Naibu Waziri Salome ameambatana na Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia wa Wizara ya Nishati, Bw. Nolasco Mlay, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Nishati, Bi. Nteghenjwa Hosseah na Meneja wa Mradi wa CookFund – UNCDF, Bw. Imanuel Muro.




LINDI KUENEZA ELIMU YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KWA WOTE

July 15, 2026 Add Comment







📌 Majiko banifu 5,776 kusambazwa mkoani Lindi




Katibu Tawala wa Mkoa wa Lindi, Bi. Zuwena Omary, amesema Mkoa wa Lindi umeanza kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ikiwa ni sehemu ya juhudi za kufikia lengo la kitaifa la kuhakikisha zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Bi. Omary amesema hayo leo, Julai 15, 2026, alipokutana na Afisa Mshauri Mwandamizi wa Masuala ya Kiufundi kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Deusdedit Malulu, aliyeambatana na uongozi wa Kampuni ya Tango Energy Limited, inayotekeleza usambazaji wa majiko banifu mkoani Lindi.

“Nawapongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia. Tunamuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, na tutaendelea kutoa elimu ili iwafikie wananchi wote,” amesema Bi. Omary.

Kwa upande wake, Mha. Malulu amesema jumla ya majiko banifu 5,776 yameanza kusambazwa na Kampuni ya Tango Energy Limited katika maeneo ya Lindi, Ruangwa, Nachingwea, Liwale na Kilwa.

Mha. Malulu amewataka wananchi katika maeneo hayo kuchangamkia fursa ya kupata majiko banifu kwa bei nafuu ya ruzuku ya shilingi 7,600 tu kwa jiko.

Naye, Meneja wa Mauzo wa Tango Energy Limited, Bw. Emmanuel Ibrahim, amesema mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kiasi kidogo cha kuni na mkaa, hatua inayolenga kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati pamoja na athari za moshi unaotokana na matumizi ya majiko ya kawaida.

Kupitia mradi huo, Tango Energy Limited itasambaza jumla ya majiko banifu 5,776 kwa wananchi kwa bei ya ruzuku. Bei halisi ya jiko moja ni TZS 50,847.46, lakini Serikali imetoa ruzuku ya asilimia 85, hivyo mwananchi atanunua jiko kwa TZS 7,600 tu.


















RAIS MWINYI ATEMBELEA BANDA LA NISHATI SABASABA

July 13, 2026 Add Comment

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, akisalimiana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba mara baada ya kufika  katika Banda la Wizara ya Nishati katika kilele cha  Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba), yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. 

Kushoto kwa Katibu Mkuu ni Mkurugezi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania ( TANESCO), Lazaro Twange.




MHANDISI MRAMBA AVUTIWA NA KASI YA REA KUSAMBAZA UMEME KWENYE VITONGOJI

July 13, 2026 Add Comment

Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu) Mha. Felchesmi Mramba ameipongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini pamoja na mafanikio ya usambazaji umeme kwenye vitongoji.

Mha. Mramba amesema hayo leo Julai 13, 2026 alipotembelea banda la REA kwenye Kilele cha  maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba)