Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

TANESCO YATUNUKIWA TUZO KUTAMBUA MCHANGO WA UBUNIFU NA MAENDELEO YA NISHATI

September 07, 2026 Add Comment

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limekabidhiwa tuzo ya kwa kutambua mchango wa kipekee katika ubunifu na maendeleo ya sekta ya Nishati nchini  ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wa Shirika katika kuendeleza sekta hiyo.


Tuzo hiyo imekabidhiwa kwa Shirika la Umeme Tanzania TANESCO katika hafla ya tuzo za ujenzi wa miundombinu na uchimbaji madini kwa mwaka 2026, iliyofanyika Septemba 4, 2026 jijini Dar es Salaam.


Akikabidhi tuzo hiyo Mkurugenzi wa Usajili wa Wakandarasi Wizara ya Ujenzi Mhandisi Rhoben Nkori kwa Niaba ya Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega amelipongeza Shirika kwa kuendelea kuimalisha upatikanaji wa Umeme katika Maeneo mbalimbali hapa nchini Hali ambayo imekuwa Chachu ya kuchochea Maendeleo katika sekta mbalimbali hapa nchini.


Tuzo hiyo imetolewa na Chama cha Ujenzi na Miundombinu cha Tanzania (CCIT), ikiwa ni utambuzi wa mchango wa TANESCO katika ubunifu na maendeleo ya nishati nchini.

KILWA YATAKA UWEKEZAJI ZAIDI KATIKA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

September 06, 2026 Add Comment




Kilwa, Lindi.


Katibu Tawala wa Wilaya ya Kilwa, Yusuph Mwinyi, amesisitiza umuhimu wa Serikali kuendelea kuwekeza katika nishati safi ya kupikia ili kuongeza upatikanaji wa nishati hiyo kwa wananchi na kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya Taifa ya nishati safi ya kupikia.


Mwinyi alitoa kauli hiyo wakati wa ziara ya ujumbe wa Wizara ya Nishati uliotembelea mradi wa nishati safi ya kupikia unaotumia teknolojia ya haidrojeni ya kijani katika Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi.


Amesema uwekezaji katika nishati safi ya kupikia ni muhimu kutokana na nafasi ya nishati hiyo katika maisha ya kila siku ya wananchi, akieleza kuwa Serikali inapaswa kuendelea kuweka mazingira yatakayowezesha teknolojia mbalimbali za nishati safi kupatikana na kutumika kwa upana zaidi.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia wa Wizara ya Nishati, Nolasco Mlay, amesema Serikali inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuendeleza teknolojia za nishati safi ya kupikia, ikiwemo teknolojia bunifu kama haidrojeni ya kijani, ili kuongeza wigo wa chaguo la nishati kwa wananchi.


Mlay amesema kuendelezwa kwa teknolojia hizo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi ya kupikia inayokidhi mahitaji yao, huku akisisitiza umuhimu wa ubunifu, uwekezaji na ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha azma hiyo.


Amesema teknolojia ya haidrojeni ya kijani inaonesha fursa katika safari ya Taifa ya kuelekea kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia, hivyo ni muhimu kuendelea kufanya tathmini na kutoa elimu kwa jamii kuhusu matumizi yake salama na yenye ufanisi.


Mlay amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi, wataalamu na wananchi ni muhimu katika kuongeza kasi ya upatikanaji na matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini, sambamba na kufikia lengo la asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

UMEME WA UHAKIKA MIGODINI WACHANGIA ZAIDI YA SHILINGI BILIONilI 340 KWA MWAKA

September 06, 2026 Add Comment



Dodoma, Septemba 3, 2026.


Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Hashimu Komba, amesema upatikanaji wa umeme wa uhakika katika migodi una mchango mkubwa kwa uchumi wa Taifa, ambapo sekta hiyo huchangia zaidi ya Shilingi bilioni 340 kwa mwaka kupitia mrabaha, kodi na tozo mbalimbali.


Mhe. Komba ameyasema hayo Septemba 3, 2026, jijini Dodoma, katika hafla ya utiaji saini mkataba wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya Mpomvu–GGM yenye msongo wa kilovoti 220 (220kV), pamoja na Kituo cha Kupoza Umeme katika eneo la GGM, mkoani Geita. Hafla hiyo ilihudhuriwa na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ambaye alikuwa Mgeni Rasmi.


Ameipongeza Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa juhudi za kuhakikisha umeme unafikishwa katika maeneo ya shughuli za madini, ikiwemo migodi mikubwa kama Geita Gold Mining (GGM), hatua inayosaidia kuongeza uzalishaji na kuchochea ukuaji wa sekta ya madini nchini.

“Tunawapongeza TANESCO kwa kuhakikisha umeme unafika katika maeneo ya migodi mikubwa kama GGM. Umeme wa uhakika ni muhimu katika kuhakikisha shughuli za uzalishaji zinaendelea bila vikwazo na hivyo kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa Taifa,” amesema.


Aidha, Mhe. Komba amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi za kuendelea kusogeza huduma ya umeme kwa wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.


Amesema Mkoa wa Geita umefikia hatua ya vijiji vyote 474 kuwa na umeme, huku mkandarasi Central Electrical Installation akiendelea na kazi ya kupeleka umeme katika vitongoji 528 vya mkoa huo.


Katika hatua nyingine, Mhe. Komba amewaalika Watanzania, wachimbaji wadogo, wa kati na wakubwa pamoja na wawekezaji kushiriki katika maonesho ya madini yanayotarajiwa kufanyika Septemba 23, 2026, mkoani Geita.


Amesema maonesho hayo yatatoa fursa kwa wananchi na wadau mbalimbali kujionea fursa zinazotokana na rasilimali za madini zilizopo mkoani Geita na nchini kwa ujumla.


Mhe. Komba pia ameahidi kuwa uongozi wa Mkoa na Wilaya ya Geita utatoa ushirikiano wa karibu kwa mkandarasi pamoja na watumishi wa TANESCO ili kuhakikisha utekelezaji wa mradi wa Mpomvu–GGM unafanyika kwa wakati na bila vikwazo visivyo vya lazima.


Amesema ushirikiano huo ni muhimu katika kuhakikisha mradi unakamilika kwa ufanisi na kuchangia upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa shughuli za uchimbaji na uzalishaji katika sekta ya madini.

TANESCO YABORESHA MAISHA YA WAFANYAKAZI NYUMBA YA MUNGU

September 05, 2026 Add Comment



*📌 Nyumba za wafanyakazi zakarabatiwa, kuboresha utendaji wa kazi*


*📌 Mtambo wa kisasa wa kuchakata maji wazinduliwa*


📍 MWANGA, KILIMANJARO | Septemba 2, 2026

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limezindua na kukabidhi nyumba zilizokarabatiwa kwa wafanyakazi wa Kituo cha Kuzalisha Umeme kwa Maji cha Nyumba ya Mungu, Wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro.


Nyumba hizo, zilizojengwa tangu mwaka 1969, wakati Kituo cha Nyumba ya Mungu kilipoanza kufanya kazi, zimefanyiwa ukarabati mkubwa hatua inayolenga kuboresha mazingira ya makazi na ustawi wa wafanyakazi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi na makabidhiano hayo, Afisa Rasilimali Watu wa Kituo cha Nyumba ya Mungu, Bi. Neema Mwaisaka, amewataka wafanyakazi waliokabidhiwa nyumba hizo kuzitunza ili ziendelee kuwa na thamani na kutumika kwa muda mrefu.


“Natoa rai kwa wafanyakazi ambao tumewakabidhi nyumba hizi wazitunze, kwani Shirika limetumia fedha nyingi katika kuzikarabati,” amesema Bi. Neema.

Kwa upande wao, wafanyakazi waliokabidhiwa nyumba hizo, kupitia mwakilishi wao Masasi Maduka, wameipongeza Menejimenti ya TANESCO kwa kuboresha mazingira yao ya kuishi, wakieleza kuwa mazingira bora ya makazi yataongeza morali, ufanisi na kujituma katika kutekeleza majukumu yao.


“Kuboresha mazingira yetu ya kuishi kutatuongezea morali ya kufanya kazi na kutuwezesha kujituma zaidi katika kutekeleza majukumu yetu,” amesema Masasi.

Katika hatua nyingine, Kituo cha Nyumba ya Mungu kimezindua mtambo wa kisasa wa kuchakata maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu pamoja na matumizi katika mitambo ya kituo.


Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mtambo huo, Mkuu wa Kitengo wa Kituo cha Nyumba ya Mungu, Mha. Andrea Shio, amesema TANESCO imefanya ukarabati na uboreshaji wa mtambo huo ili kuufanya kuwa wa kisasa na kuongeza ufanisi wake.


“Naipongeza Menejimenti ya Shirika kwa ukarabati wa mtambo huu. Maji haya yanatumika kwa matumizi ya binadamu pamoja na kwenye mitambo,” amesema Mha. Shio.


Ukarabati wa nyumba za wafanyakazi pamoja na kuboresha miundombinu muhimu kama mtambo wa kuchakata maji ni sehemu ya jitihada za TANESCO za kuimarisha mazingira ya kazi na makazi, kuongeza ufanisi na kuhakikisha huduma za uzalishaji umeme zinaendelea kutolewa kwa uhakika.

MRADI WA UMEME MPOMVU – GGM KUIMARISHA UPATIKANAJI WA UMEME NA KUCHOCHEA SHUGHULI ZA KIUCHUMI GEITA – MHE. SALOME

September 04, 2026 Add Comment

 


Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme nchini kupitia utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Mpomvu hadi kituo cha kupokea na kupoza umeme cha GGM, wenye urefu wa takribani kilomita 6.7.


Akizungumza Septemba 3, 2026, jijini Dodoma, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi huo, Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema kukamilika kwa mradi huo kutaimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na kuchochea shughuli za kiuchumi, ikiwemo uzalishaji, ajira, ongezeko la mapato na uwekezaji.




Amesema Serikali itaendelea kushirikiana na TANESCO na wadau wa sekta ya nishati kuhakikisha miundombinu ya umeme inaendana na kasi ya ukuaji wa mahitaji.


“Serikali itaendelea kushirikiana na TANESCO na wadau wote wa sekta ya nishati kuhakikisha miundombinu ya umeme inaendana na kasi ya ukuaji wa mahitaji. Tunataka kuona umeme unaozalishwa nchini ukitumika kikamilifu kuchochea uzalishaji, kuongeza ajira, kuongeza mapato na kuvutia uwekezaji zaidi. Mradi huu ni kielelezo cha falsafa hiyo,” amesema Mhe. Salome.




Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema mradi huo unatekelezwa kwa miezi 18 kutoka tarehe ya utiaji saini mkataba ukilenga kukidhi ongezeko la mahitaji ya umeme kwa GGM.

“Mradi huu unagharimu takribani Shilingi bilioni 63.19 za Kitanzania na kutokana na kuwa GGM ni miongoni mwa wateja wetu wakubwa wenye kuchangia kiasi kikubwa cha mapato kwa Shirika, tutahakikisha mradi huu unafanikiwa kama inavyotarajiwa kukidhi ongezeko la mahitaji yao kwa manufaa ya pande zote mbili na pato la Taifa kwa ujumla,” amesema Bw. Twange.



Aidha, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya TANESCO, Mhe. Balozi Zuhura Bundala, amesema utiaji saini wa mkataba huo ni sehemu ya hatua za kimkakati za kujenga uwezo wa TANESCO kukidhi mahitaji ya wateja na kufungua fursa za uwekezaji na ajira.

“Utiaji saini huu ni sehemu ya kimkakati kujenga uwezo wa TANESCO kukidhi mahitaji ya wateja na kufungua fursa za uwekezaji na ajira. Bodi tutaendelea kuisimamia TANESCO kukidhi ongezeko la hitaji la umeme kwa kuimarisha na kuwekeza kwenye ujenzi wa miundombinu ya umeme,” amesema Mhe. Bundala.


Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO kwa namna inavyosimamia Shirika katika ujenzi wa uchumi wa kisasa kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


“Niipongeze Bodi ya Wakurugenzi TANESCO kwa namna mnavyosimamia Shirika hili kujenga uchumi wa kisasa kuelekea Dira 2050. Utekelezaji wa mradi huu unatupa nguvu zaidi kwa sababu sekta zote, nishati na madini, zipo chini yetu,” amesema Mhe. Mgalu.


Naye Mkuu wa Wilaya ya Geita, Mhe. Hashimu Komba, akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa huo amesema Uongozi wa Mkoa umejipanga kushirikiana na mkandarasi wa mradi huo kuhakikisha utekelezaji wake haupati kikwazo, akisisitiza umuhimu wa nishati ya umeme katika kuchochea maendeleo ya sekta mbalimbali.


“Ni dhahiri, nishati ya umeme inachagiza maendeleo ya sekta zote. Tunampongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyosukuma kwa dhati agenda ya nishati ya umeme kuwafikia wananchi. Mamlaka ya Mkoa imejipanga kushirikiana na Mkandarasi wa mradi wa umeme wa Mpomvu–GGM kuhakikisha mradi haupati kikwazo,” amesisitiza Mhe. Komba.


Kukamilika kwa mradi huo, kutatoa fursa ya njia ya awali ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoto 33 iliyokuwa ikipelekea umeme GGM, kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika Mkoa wa Geita na maeneo ya pembezoni , vilevile kuwezesha wananchi kuendesha shughuli zao za uzalishaji kwa ufanisi, pamoja na kuweka mazingira wezeshi kwa uwekezaji mpya ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha na kuongeza uwezo wa mfumo wa usafirishaji na usambazaji wa umeme kukidhi mahitaji ya sasa na yajayo.




NISHATI YA JUA YAZIDI KUIMARISHA GRIDI YA TAIFA

September 03, 2026 Add Comment




Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema Serikali inaendelea kuongeza matumizi ya nishati jadidifu, hususan nishati ya jua, katika uzalishaji wa umeme nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza uwezo wa uzalishaji na kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na endelevu.


Mhe. Makamba ameyasema hayo leo, Septemba 3, 2026, wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana, kuhusu mpango wa Serikali kutumia nishati ya jua ili kupunguza changamoto zinazowakabili wanawake wa Mkoa wa Njombe.


Amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kuzalisha umeme kutoka katika vyanzo vya nishati jadidifu, ikiwemo jua, sambamba na utekelezaji wa mkakati wa kuchanganya vyanzo vya uzalishaji umeme nchini (Generation Mix).


“Kwa sasa, umeme unaozalishwa kutokana na nishati ya jua unachangia jumla ya Megawati 65 katika Gridi ya Taifa, ambapo wazalishaji wadogo wa umeme (SPPs) wanachangia Megawati 15 kutoka katika vyanzo vya jua,” amesema Mhe. Makamba.


Ameongeza kuwa Serikali inatarajia kuongeza MW 100 baada ya kukamilika kwa Mradi wa Umeme wa Jua wa Shinyanga Awamu ya Pili, pamoja na MW 22 zitakazozalishwa kupitia miradi mitatu ya wazalishaji wadogo wa umeme (SPPs) ambayo ipo katika hatua za mwisho za ujenzi.


Mhe. Makamba amesema uwekezaji huo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuongeza mchango wa nishati jadidifu katika uzalishaji wa umeme, kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika na endelevu, pamoja na kupunguza utegemezi wa chanzo kimoja cha uzalishaji wa umeme nchini.