Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

RC CHALAMILA AZINDUA " PROGRAMU KONEKT UMEME PIKA KWA UMEME"

October 10, 2025 Add Comment


📌Aipongeza TANESCO kwa  mpango wa ukopeshaji wa majiko wateja 

wanaounganishiwa umeme


📌Asema ni wazo la kibunifu kuongeza wateja wa umeme na watumiaji wa umeme kupikia

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es salaam


Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Albert Chalamila amezindua program ya Konekt Umeme Pika kwa Umeme ukiwa ni utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Nishati (Energy Compact), wenye lengo la kuunganisha wateja milioni 8.5 ifikapo mwaka 2030, sawa na takribani wateja milioni 1.7 wapya kila mwaka.

Akizungumza katika uzinduzi huo Oktoba 09.2025 katika viwanja vya Mwembeyanga Jijini Dar es salaam Mhe  Mhe. Chalamila ameipongeza ,Wizara ya Nishati, TANESCO na wadau wote wa maendeleo kwa kuja na wazo hili bunifu lenye lengo la kuongeza idadi ya wateja wanaounganishiwa umeme pamoja na upatikanaji wa nishati safi ya kupikia.

Pamoja na hayo Mhe. Chalamila amesema mabadiliko ya tabia nchi yamekuwa yakichangia changamoto ya ukame hivyo ameitaka jamii kuwa mstari wa mbele kuhakikisha inalinda mazingira na kutunza miundombinu ya umeme.


‘’Niwapongeze sana TANESCO kwa kuja na mpango huu, hakika mmeibeba ajenda ya Mhe. Rais Dkt.  Samia Suluhu Hassan na ninafurahi sana kwa jiji la Dar es salaam umeme umefika kila sehemu na tumeshuhudia maboresho ya miundombinu ya umeme. Ninaamini kwa jitihada hizi wananchi wengi watahamasika kutumia umeme kupikia,’’alisisitiza Mhe. Chalamila.


Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange amefafanua  kuwa mpango huu ni mwanzo wa zama mpya katika historia ya huduma za umeme nchini ambapo kwa hatua ya kuwaunganishia wateja wapya na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya umeme kupikia kunaifanya  jamii ya Kitanzania kuwa katika viwango bora vya maisha.


‘’Tumeamua kusogeza huduma zetu karibu na wateja, kwetu mteja ni zaidi ya neno lenyewe tumekuwa tukifanya jitihada za makusudi katika kumuhudumia na  kupitia ushirikiano na MECS, TANESCO imeandaa mpango wa kuhakikisha kila mteja mpya anae unganishiwa  umeme anapata jiko la umeme sanifu mara tu baada ya kufungiwa huduma ya umeme, ‘’,

 ameeleza Twange.


Naye Mwakilishi wa Mpango wa MECS ulio chini ya Serikali ya Uingereza Bw. Charles Barnabas ambao ndio wanadhamini wa mpango wa huduma za kisasa za kupikia (MECS) amesema kwa kushirikiana na TANESCO mpango huu utachagiza ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa umeme kwa wananchi.


Hafla ya uzinduzi huu umeenda sambamba na kauli mbiu isemayo Konekti umeme, pika kwa umeme ambapo wateja ambao wameunganishiwa umeme walikopeshwa majiko yanayotumia umeme kidogo kupikia na kukabidhiwa na Mgeni rasmi ambayo watayalipa kwa kipindi cha miezi sita hadi mwaka mmoja kupitia manunuzi ya umeme.

EACOP NI MRADI WA KUJIVUNIA DUNIANI – BALOZI SEFUE

October 10, 2025 Add Comment




Na Mwandishi Wetu, Tanga


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania TPDC Mhe Balozi Ombeni Sefue amesema kuwa Mradi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki EACOP ni miongoni mwa miradi bora zaidi duniani inayotekelezwa kwa kuzingatia utu haki za binadamu na uhifadhi wa mazingira.


Akizungumza Oktoba 9, 2025 jijini Tanga katika mkutano na waandishi wa habari Balozi Sefue amesema kuwa mradi huo unaotekelezwa kutoka Kabaale Uganda hadi Chongoleani Tanga umefikia hatua kubwa ya utekelezaji na unaendelea kwa kasi nzuri huku ukionyesha mfano wa kuigwa katika usimamizi wa miradi mikubwa ya kimkakati barani Afrika.


Amesema Serikali kupitia TPDC pamoja na wanahisa wenzake wamejipanga kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na unawanufaisha Watanzania kwa kuzingatia viwango vya kimataifa katika heshima ya haki usalama na utunzaji wa mazingira.

Utekelezaji wa mradi kwa ujumla umefikia asilimia 70 ambapo kazi ya uchomeleaji wa mabomba imekamilika kwa zaidi ya kilomita 946 sawa na asilimia 65.6% ya urefu wote wa bomba huku ujenzi wa bomba ukitarajiwa kukamilika Julai 2026 Serikali ya Tanzania imehakikisha hakuna ucheleweshaji unaosababishwa na changamoto za kifedha kwani fedha zote za utekelezaji zimeshapatikana kwa asilimia 100.


Katika hatua za utekelezaji wananchi 9869 kati ya 9927 waliopisha eneo la mradi wamelipwa fidia kwa jumla ya Shilingi Bilioni 35.06 ambapo mkoani Tanga pekee wananchi 1688 wamepokea fidia ya zaidi ya Shilingi Bilioni 10.49.


Aidha nyumba 340 za makazi mbadala zimejengwa kwa wananchi 294 kati yao 40 kutoka mkoa wa Tanga wamenufaika kwa nyumba 43 mpya.


Kuhusu ajira jumla ya ajira 9194 zimezalishwa ambapo Watanzania 6895 sawa na asilimia 75 wamenufaika moja kwa moja kupitia kazi zenye ujuzi wa kati na wa chini wakati ajira 2299 sawa na asilimia 25 zimenufaisha wataalamu wa ndani katika fani za uhandisi mazingira usalama na maendeleo ya jamii.



Serikali ya Tanzania imekusanya zaidi ya Shilingi Bilioni 70 kupitia vyanzo mbalimbali vya kodi na ushuru unaotokana na mradi huu na matarajio ni kukusanya zaidi ya Shilingi Trilioni 2 baada ya kuanza kwa shughuli rasmi za uendeshaji Katika Jiji la Tanga pekee Halmashauri imekusanya zaidi ya Shilingi Bilioni 2 kutokana na kodi na ada zinazotokana na wakandarasi wa mradi.


Zaidi ya kampuni 200 za Kitanzania zimepata zabuni zenye thamani ya shilingi trilioni 1.325 na fedha hizo zimechochea mzunguko wa uchumi wa ndani kupitia ununuzi wa bidhaa na huduma zinazozalishwa hapa nchini Kupitia utekelezaji wa EACOP barabara zenye jumla ya kilomita 304 zimeboreshwa hivyo kurahisisha shughuli za wananchi na wakandarasi.


Mradi unatekeleza ujenzi wa vituo vitano vya kupoozea umeme vinavyounganishwa na njia za umeme zenye jumla ya kilomita 313.13 hatua itakayowezesha vijiji vingi kuunganishwa na nishati ya umeme kwa mara ya kwanza Aidha mradi unatekelezwa kwa kuzingatia sheria za Tanzania na viwango vya kimataifa ukiweka kipaumbele katika usalama wa wafanyakazi na mazingira.


Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni pamoja na kutumia mifumo maalumu ya kuhifadhi joto ndani ya bomba ili kulinda uhai wa viumbe wa ardhini kuhifadhi na kurejesha tabaka la udongo wakati wa ujenzi ili kuruhusu uoto wa asili kurejea kutumia teknolojia ya Horizontal Drilling Direction kuvusha bomba chini ya mito kama Mto Sigi bila kuathiri maji wala bioanuwai kujenga Solar Farms kama chanzo mbadala cha nishati kwa ajili ya mitambo ya mradi.


Mradi wa EACOP pia unashirikiana na taasisi za uhifadhi wa mazingira kama TANAPA NEMC TAWA na TFS kuhakikisha shughuli zote katika hifadhi mbuga na misitu zinafanyika kwa uangalizi mkubwa ili kulinda mazingira.


Katika upande wa jamii mradi umeendelea kujenga uhusiano mzuri na wananchi katika maeneo unakopita ambapo miradi kadhaa ya kijamii inatekelezwa ikiwemo ujenzi wa mtandao wa mabomba ya maji wenye gharama ya shilingi bilioni 4.4 unaowanufaisha zaidi ya wananchi 26000 ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Chongoleani upandaji wa miti milioni 2 ya minazi ujenzi wa uwanja na kituo cha michezo cha timu ya Coastal Union pamoja na mafunzo kwa vijana 800 katika fani za ujenzi mekanika na umeme wa viwandani.


Balozi Sefue amesema licha ya changamoto zilizojitokeza wanahisa wa EACOP wakiwemo TPDC wanaendelea na utekelezaji wa mradi kwa nia ya dhati hadi ukamilike ifikapo mwaka 2026 akisisitiza kuwa EACOP ni mradi wa kielelezo unaoonyesha usimamizi bora wa miradi mikubwa nchini.


Amesema mradi huu ni wa kizazi hiki na vizazi vijavyo kwani unahakikisha Watanzania wananufaika kwa kulipwa fidia kwa haki kujengewa nyumba bora kupewa mafunzo ya kilimo ufugaji na stadi za kazi pamoja na kulindwa mazingira na haki zao za msingi.


Bodi ya TPDC imesisitiza itaendelea kusimamia Menejimenti ya Shirika kuhakikisha ujenzi wa bomba unakamilika kwa wakati na kwa ubora wa hali ya juu huku ikihakikisha Watanzania wanaona matokeo ya moja kwa moja ya uwekezaji huu katika maisha yao ya kila siku.





















SHULE ZINAZOTUMIA KUNI KAMA NISHATI YA DHARURA ZAELEKEZWA KUTUMIA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

October 09, 2025 Add Comment


📌 *Mkurugenzi Nishati Safi ya Kupikia apongeza jitihada za Shule zilizohamia kwenye nishati salama na rafiki kwa afya na Mazingira.*


📌 *Atoa wito kwa Wadau kuwekeza katika uzalishaji wa kuni/mkaa mbadala kutokana na kuhitajika kwake*

Mkurugenzi wa Nishati safi  ya kupikia, Wizara ya Nishati, Bw. Nolasco Mlay, ametoa wito kwa shule zote nchini  kuhakikisha zinaachana na matumizi ya kuni na badala yake kuhamia kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia, ikiwemo gesi, majiko banifu, na mkaa mbadala.

Akizungumza wakati wa kuhitimisha  ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya nishati safi ya kupikia inayotekelezwa chini ya mpango wa CookFund katika Mkoa wa Mwanza, Mlay amesema kuwa shule nyingi bado zinategemea kuni kama nishati ya dharura, hali inayochangia uharibifu wa mazingira na madhara kwa afya ya watumiaji.

“Katika ziara hii nimebaini Shule nyingi zinatumia kuni kama nishati ya dharura hivyo nitoe wito kwa uongozi wa shule mkishirikiana na Afisa Elimu kuanza kutumia mkaa mbadala ambao ni rafiki kwa mazingira na unachangia katika kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa." Amesema Mlay

Aidha, Bw. Mlay amepongeza baadhi ya shule ambazo tayari zimeanza kutumia nishati safi, ambazo hazifadhiliwi na mradi wa Cookfund ikiwemo shule ya Sekondari ya wavulana Musabe pamoja na Shule ya Msingi Buhongwa A akizitaja kuwa mfano bora kwa taasisi nyingine nchini.

Amesema matumizi ya nishati safi huchangia kwa kiasi kikubwa kulinda afya ya wanafunzi na walimu dhidi ya magonjwa ya mfumo wa upumuaji, yanayosababishwa na moshi kutoka kwa kuni na mkaa wa kawaida.

“Tunapongeza juhudi za shule zinazohamia kwenye nishati safi ya kupikia kwani hii hatua ni kubwa katika kulinda afya, mazingira na hata kuongeza ufanisi wa shughuli za kila siku shuleni hivyo nitoe wito kwa shule zote ambazo bado hazijaanza kutumia nishati safi ya kupikia, kuanza kutumia nishati safi kwani ni nafuu na zinaokoa muda." Ameongeza Bw. Mlay

vilevile, Mlay amehimiza Serikali za Mitaa, Wakuu wa Shule na wadau wa elimu kushirikiana kwa karibu katika kuhakikisha taasisi za elimu zinapata vifaa vya kisasa vya kupikia kwa kutumia nishati safi.

 Amesisitiza kuwa mradi wa CookFund na mipango mingine ya kitaifa iko tayari kusaidia shule zinazotaka kuhamia kwenye mfumo huo wa kisasa wa kupikia ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati  wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia 2024 - 2034 ambao unalenga kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034, asilimia 80 ya wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia.

Mlay  ametoa wito kwa wawekezaji mbalimbali kujitokeza kuwekeza katika uzalishaji wa kuni na mkaa mbadala ili kufanikisha azma ya nchi kuhamia kwenye nishati safi na kulinda mazingira.


“Ni muhimu kuwekeza kwa dhati katika uzalishaji wa kuni na mkaa mbadala, hasa kwa ajili ya taasisi kwani kukosekana kwa wazalishaji hawa kunaweza kusababisha athari kubwa kiuchumi, kijamii na kimazingira hapo baadaye hivyo tunahimiza wadau wote kujitokeza, kushirikiana, na kuwekeza katika mabadiliko haya yenye tija kwa taifa na vizazi vijavyo”. Amesisitiza Bw. Mlay


Naye Afisa Elimu Taaluma Halmashauri ya Jiji la Mwanza Bw. Rodrick Kazinduki ameeleza kuwa  kupitia mkakati wa Nishati Safi ya kupikia, Tanzania itaondokana na changamoto za uharibifu wa mazingira na afya zinazotokana na matumizi ya nishati zisizo safi huku akieleza kuwa  kupitia ushirikiano wa Serikali, Mashirika ya Kimataifa na jamii kwa ujumla, kuna matumaini kuwa shule nyingi zaidi zitaweza kuhama kutoka kwenye kuni na mkaa wa kawaida, na kuingia katika zama mpya za nishati safi, salama na endelevu.

TANESCO KUWAUNGANISHIA WATEJA UMEME NDANI YA SIKU MOJA

October 08, 2025 Add Comment


📌Ni katika maadhimisho ya wiki ya huduma kwa Wateja yanayofanyika katika viwanja vya Mwembe yanga.


📌RC Chalamila kuzindua utekelezaji mpango wa kuwakopesha majiko ya umeme wateja wapya watakaounganishiwa umeme na kulipa kupitia manunuzi ya umeme


Na Josephine Maxime, Dar es saaam


Katika kuadhimisha Wiki ya Huduma kwa Wateja, TANESCO imekuja na program maalumu ya kuwahudumia wateja wao Kwa kuwaunganishia wateja wapya huduma ya umeme ndani ya siku moja, ikiwa ni sehemu ya kusogeza huduma karibu na wateja wao.


Akizungumza katika maadhimisho hayo yanayofanyika katika viwanja vya mwembe yanga jijini Dar es salaam Bi. Gowelle ameeleza kuwa TANESCO imekuja na program hiyo ya TANESCO Mtaani kwako kwa lengo la kuwahudumia wananchi wa mkoa wa Dar es salaam ambapo wafanyakazi muhimu wa vitengo mbalimbali vya shirika wameweka kambi kwenye viwaja hivyo kwa siku tatu kuanzia leo Oktoba 08 ili  kutoa huduma kwa wananchi.

Vilevile amesema kwa siku ya alhamisi wanatarajia kuwa na hafla ya uzinduzi wa  mpango maalum wa kuwaunganishia umeme wateja wapya na kuwakopesha majiko ya umeme kwa wale watakaopenda kutumia nishati ya umeme kwenye kupika na kwamba watayalipa kidogo kidogo kupitia manunuzi yao ya umeme kwa mkataba wa miezi sita hadi mwaka mmoja.

Mpango huo ni sehemu ya utekelezaji wa malengo ya mradi wa Shirika unaofadhiliwa na Taasisi ya Mecs ambao umedhamini majiko ya umeme mapya elfu moja kwa majaribio ya awali ya mpango huo.

‘’ TANESCO tumeona tuadhimishe wiki ya huduma kwa mteja kwa kusogeza huduma kwa jamii, tumekuja na  program ya TANESCO Mtaani kwako kwa lengo la kuwahudumia wananchi wa mkoa wa Dar es salaam, ni fursa ya pekee kwa wananchi kufika katika viwanja hivi vya mwembe yanga kupata elimu na mambo mbalimbali yahusuyo Shirika,’’alisisitiza Bi Gowelle 

Aidha, amebainisha kuwa wananchi watapata fursa ya kushuhudia maandalizi ya vyakula mbalimbali kwa kutumia majiko yanayotumia umeme kidogo pamoja na kupata elimu kuhusu matumizi bora ya umeme,usalama ,ulinzi wa miundombinu na operesheni inayoendelea ya ukaguzi wa mita

Bi. Gowelle pia amewakaribisha wananchi kushiriki katika uzinduzi rasmi  utakaofanyika Oktoba 09. 2025 katika viwanja vya Mwembe Yanga, jijini Dar es Salaam, ambapo Mgeni Rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mheshimiwa Albert Chalamila.

Maadhimisho haya yanafanyika chini ya kaulimbiu isemayo: “Mpango Umewezekana”, ikilenga kuonesha mafanikio ya huduma za TANESCO na dhamira ya Shirika hilo katika kuwahudumia Watanzania kwa haraka, ufanisi na ubunifu.

WANUFAIKA WA MITAJI YA COOKFUND WAHIMIZWA KUWEKEZA KATIKA MITUNGI MIDOGO YA GESI

October 08, 2025 Add Comment


📌 *Ni mitungi ya kilo tatu au chini ya kilo tatu*


📌 *Lengo ni kuwezesha wananchi wa kipato cha chini kumudu gharama*


📌 *Wasisitizwa matumizi ya Mita janja (smart meters) ili kuwezesha wananchi kununua gesi kama LUKU.*


Wanufaika wa mitaji kupitia mradi wa CookFund ambao upo chini ya mpango wa kimataifa wa Integrated Approach to Sustainable Clean Cooking Solution unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF)  kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU)  wamehimizwa kuelekeza uwekezaji wao katika uzalishaji na usambazaji wa mitungi midogo ya gesi ya kilo tatu au chini ya kilo tatu ili kuwawezesha wananchi wa kipato cha chini kuhamia kwenye matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa urahisi zaidi.




 Mkurugenzi wa Nishati safi ya Kupikia Wizara ya Nishati,  Nolasco Mlay ameyasema hayo wakati akiendelea na ziara yake jijini Mwanza kwa lengo la kukagua miradi ya Nishati Safi ya Kupikia inayofadhiliwa na Cookfund

ambayo inalenga kuchochea maendeleo ya nishati safi ya kupikia nchini.


Akiwa jijini Mwanza Mlay aliwatembelea wafanyabiashara wa kuuza gesi walioongezewa mtaji kupitia mradi huo wa CookFund ili kuhakikisha Wananchi wanafikiwa na huduma ya gesi kwa ukaribu zaidi kupitia uinuaji wa wafanyabiashara wadogo na wa kati kwenye sekta ya nishati safi ya kupikia.


Amesema kupitia Cookfund wafanyabiashara wadogo wanapewa  mitaji na msaada wa kiufundi ili kuongeza wigo wa usambazaji wa majiko bora ya gesi na mitungi ya gesi.


Mlay amewapongeza wanufaika hao wanaouza mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku kwa kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma hiyo kwa wakati na urahisi zaidi huku akizidi kusisitiza kuhusu kuuza pia mitungi ya gesi ya kilo moja hadi tatu.



“Tunahitaji kuona wanufaika wa CookFund wakiwekeza kwenye teknolojia zinazogusa maisha ya wananchi moja kwa moja. Mitungi midogo ni suluhisho linalowezesha watu wengi zaidi kutumia gesi badala ya kuni au mkaa”. Amesema Mlay

Sambamba na hilo,  Mlay ametoa wito kwa wadau wote wa nishati safi ya kupikia kuleta teknolojia ya mita janja (smart meter) kwa baadhi ya maeneo ambayo bado hawana ili kurahisisha ununuzi wa gesi kwa njia ya kidigitali, na kuondoa changamoto za kujaza mitungi kwa gharama kubwa au umbali mrefu.

“Lazima tuhakikishe nishati safi ya kupikia inapatikana kwa bei nafuu, kwa njia rahisi, na kwa vifaa vinavyomfaa kila Mtanzania kwani kupitia teknolojia hii wananchi wataweza kununua nishati hiyo kama wanavyonunua umeme kwa njia ya LUKU ambapo itasaidia kuondoa changamoto za upatikanaji wa gesi hasa wakati wa kujaza mitungi kwa wananchi wa kipato cha chini”. Amesisitiza Bw.Mlay.


Vilevile amewataka wananchi kuendelea kuchukua hatua za kubadilika na kutumia nishati safi za kupikia ikiwemo gesi, umeme, mkaa mbadala na bayogesi kwa ajili ya afya bora na mazingira salama.


Kwa upande wao,  Wafanyabiashara wanaouza mitungi ya gesi wamesema kuwa mwitikio kutoka kwa wananchi umekuwa mkubwa  huku baadhi ya wananchi wakikopeshwa mitungi na wengine wakijitokeza kuwekeza kwa kulipa fedha kidogokidogo ili kuweza kupata mitungi hiyo ya gesi  ili kuachana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa afya na mazingira.