📌Pia kuwekeza kwenye miundombinu ya usafirishaji umeme nchini
📌Waialika Tanzania kushiriki mkutano wa Tisa wa maendeleo kati ya Japan na Afrika
📌 Waupongeza mpango mahsusi wa Nishati wa Taifa kuwa bora na wa mfano kwa nchi za Afrika
Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati, anayeshughulikia umeme na nishati jadidifu Dkt Khatibu Kazungu, leo amekutana na kuzungumza na ujumbe wa wawekezaji kutoka nchini Japan kupitia kampuni ya Toyota Tshusho Cooperation, uliolenga kufanya mazungumzo kuhusu uwekezaji wa miradi mbalimbali kwenye sekta ya umeme hususan umeme wa jua, upepo na njia za kusafirisha umeme pamoja na ujenzi wa vituo vya kupoza umeme chini ya mpango mahsusi wa Nishati wa Taifa ujulikanao kama Energy Compact.
Kupitia serikali ya Japan chini ya Japan International Banking Corporation, Japan imeonesha nia yake ya kuwekeza kwenye maeneo hayo na kwa sasa wapo kwenye mazungumzo na Serikali ya Tanzania ili kuainisha maeneo hayo ya uwekezaji.
Dkt Kazungu amesema Japan imeonesha nia hiyo ya kuwekeza chini ya mpango huo mahsusi kutokana na Tanzania kuwa na mpango mzuri wa ajenda ya Compact ambao umekuwa wa mfano kwa nchi za Afrika hususan kwenye mafanikio kuunganisha umeme kwa wateja, na nchi nyingi za Afrika zimekuwa zikijifunza kutoka mpango wa Tanzania.
Mpango mahususi wa Nishati wa Taifa ulibuniwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Benki ya Dunia kwa lengo la kuzisaidia nchi za Afrika kutekeleza miradi mbalimbali ya nishati wakati wa mkutano wa wakuu wa nchi uliofanyika jijini Dar es salaam wa Mission 300 uliobeba ajenda ya kuhakikisha waafrika milioni 300 wanafikiwa na umeme ifikapo mwaka 2030.
Katika hatua nyingine Serikali ya Japan imeialika Tanzania kushiriki kwenye mkutano wa tisa wa masuala ya maendeleo kwa nchi za Afrika utakaofanyika nchini Japan mwezi Agosti, 2025 kwa lengo la kuzikutanisha nchi za Afrika kujadili masuala ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali.
EmoticonEmoticon