MELI ILIYOBEBA MAGARI 300 YATUA BANDARI YA TANGA NA KUWEKA REKODI YA AINA YAKE

July 30, 2024



Na Bashiru Hamis, TANGA

HISTORIA mpya imeandikwa katika Bandari ya Tanga baada ya leo Meli iliyobeba magari 300 ya MV Annegrit kupitia kampuni ya kubwa iliamua kutumia Bandari ya Tanga kupitisha mizigo yake kupitia Kampuni Seafront Shipping Services (SSS) ambapo meli hiyo ikitokea nchini China ikitumia siku 21 kufika kwenye Bandari ya Tanga

Ujio wa Meli hiyo ambayo kwa mara ya kwanza imeingiza idadi kubwa ya Magari ambayo yatashushwa katika Bandari ya Tanga ulishuhudiwa na Naibu Waziri wa Uchukuzi Mhandisi David Kihenzile.

Akizungumza mara baada ya kuipokea meli hiyo Mhandisi Kihenzile ujio wa meli hiyo katika Bandari ya Tanga ni kutokana na juhudi zilizofanywa na Serikali katika kuboresha Bandari hiyo ambapo kiasi cha Bilioni 429 zilitumika

Alisema uwekezaji huo umekuwa ni chachu kubwa ya kuifungua Bandari hiyo huku akiwashauri wadau mbalimbali kutumia bandari ya Tanga kwa ajili ya kusafirisha mizigo yao na kuleta ameli za abiria kutokana na maboresho makubwa yaliyofanywa kwenye Bandari.

“Ujio wa Meli hii ni matunda makubwa ya uwekezaji ambayo yamefanywa na Serikali kwani katika Bandari hii kumefanyika uwekezaji wa Bilioni 429 katika maboresho ya Bandari hiyo leo tumeshuhudia meli kubwa kutoka China ikiwa imetumia siku 21 kutua Tanga ikiwa imebeba magari 300”Alisema

Alisema katika uwekezaji huo fedha hizo zilisaidia kuongeza kina kutoka mita 3 mpaka 13 zamani meli hiyo isingeweza kupaki hapo ilipo lakini pia imewasaidia kufanya upanuzi na eneo la kuingilia na kutokea meli kwa takribani Upana mita 73.

Aidha alisema pia fedha hizo zimesaidia kuongeza eneo la kugeuzia meli kwenye kipenyo cha takribani mita 800.

“Nitumia nafasi hii kutoa rai kwa sababu bado mzigo unaohudumiwa hapa hautoshi idadi ya meli hazitoshi wanajikuta sehemu ya mzigo mwengine tunavizia kwenye bandari za majirani zetu zikishusha ndio zije hapa tunataka meli za aina hii zitoke moja kwa moja ulaya, china na maeneo ya mbalimbali zije hapa kwetu moja kwa moja”Alisema.

Awali akizungumza Mkuu wa Mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian aliwataka wafanyabiashara kuitumia Bandari hiyo kwa sababu wakiitumia mizigo yao itatoka kwa haraka hakuna usumbufu wa kuambiwa subiri meli nyengine zinapakua.

Hii ni kwa mara ya kwanza wamefanikiwa kuleta meli hiyo yenye shehena ya mizigo mchanganyiko inayokadiriwa kuwa na tani 14,000 kutoka chini moja kwa moja hadi Bandari ya Tanga.

Ambapo inaweka alama ya kipekee kuwahi kutokea kwa meli ya mizigo mchanganyiko kuweza kushusha kiwango kikubwa cha mizigo mchanganyiko, zaidi ya magari 500 na aina nyingine ya mizigo mchanganyiko kuweza kushushwa katika bandari ya Tanga.

Baadhi ya mizigo itaelekea katika nchi Jirani kama Zambia,Zimbabwe,Jamhuri ya watu wa kongo (D.R.C) ,Malawi ,Rwanda na kadhalika. Pia mizigo mingine itabaki hapa nchini kwa maana ya (Local goods).

“Kimsingi haya ni mafanikio makubwa na muhimu kwa maendeleo ya Bandari ya Tanga. Bandari ya Tanga inatarajia pia kupokea aina nyingi ya mizigo kuelekea nchi za Jirani, na hii itafanya wafanyabiashara, watoa huduma za usafiri, mawakala wa forodha, jamii za wafanyabiashara wa ndani, kwa pamoja kunufaika kwa kiwango cha juu kutokana na meli zitakazokuwa zinatia nanga bandari ya Tanga moja kwa moja kutoka bandari za Kimataifa

Awali akizungumza Meneja Mkuu wa Kampuni ya Uwakala wa Meli Seafront Shipping Services (SSS) Neelakandan CJ alisema kutakuwa na meli za mizigo mchanganyiko kuanzia 3 mpaka 4 kipindi cha hivi karibuni, ambazo tayari zimepangwa kuingia bandari ya Tanga mwezi wa nane(8).


Share this

Related Posts

Previous
Next Post »