WANANCHI MIPAKANI WATAKIWA KUTUMIA TAASISI RASMI ZA FEDHA

January 30, 2024

Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akijibu swali la Mbunge wa Momba, Mhe. Josephat Kandege, aliyetaka kufahamu mpango wa Serikali wa kurasimisha na kurahisisha ubadilishaji wa fedha za kigeni kati ya Tanzania, Zambia, Malawi na Msumbiji, bungeni Jijini Dodoma.

Waziri wa Fedha Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akiteta jambo na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb), bungeni Jijini Dodoma.

 

 Na. Peter Haule, WF, Dodoma

Serikali imewataka Wananchi na wafanyabiashara katika mipaka ya Tanzania na nchi jirani kutumia taasisi rasmi za fedha zikiwemo benki za biashara na maduka ya kubadilisha fedha za kigeni ili kurahisisha miamala ya kibiashara.

Rai hiyo imetolewa bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), wakati akijibu swali la Mbunge wa Momba, Mhe. Josephat Kandege, aliyetaka kufahamu mpango wa Serikali wa kurasimisha na kurahisisha ubadilishaji wa fedha za Kigeni kati ya Tanzania, Zambia, Malawi na Msumbiji.

“Benki Kuu imeendelea kurahisha taratibu za usajili wa maduka ya kubadilisha fedha za kigeni nchini ili wananchi wenye uwezo waweze kufungua na kuendesha maduka hayo sehemu mbalimbali, ikiwemo sehemu za mipakani”, alisema Dkt. Nchemba.

Dkt. Nchemba alisema kuwa hadi kufikia Desemba 2023, huduma za kubadilisha fedha katika mipaka ya Tunduma, Mtwara, Mtukula na Namanga zinapatikana katika matawi 25 ya benki na maduka mawili (2) ya kubadilisha fedha.

 

Aidha alieleza kuwa Serikali kwa kushirikiana na jumuiya za kikanda, ikiwemo EAC na SADC zimetengeneza mifumo ya malipo ili kurahisha malipo kwa nchi wanachama kwa lengo la kupunguza matumizi ya fedha taslimu katika biashara.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »