MAKAMU WA KWANZA WA RAIS ZANZIBAR AWAFAGILIA BAKIZA NA BAKITA KWA KUENEZA KISWAHILI DUNIANI

December 13, 2023



MAKAMU wa Rais Zanzibar, Othman Masoud Othman akikagua vitabu pamoja na kazi za sanaa za ufundi nje ya ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil

MAKAMU wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Othman Masoud Othman akihutubia katika Kongamano la Kimataifa la Saba la BAKIZA katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil- Kikwajuni , Unguja


KATIBU Mtendaji wa BAKIZA, Dk. Mwanahija Ali Juma




WAZIRI wa Habari, Vijana Utamaduni na Michezo Zanzibar, Mh. Tabia Maulid Mwita


****


NA. ELISANTE KINDULU, UNGUJA


MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mh. Othman Masoud Othman ameyapongeza mabaraza ya kiswahili kwa kueneza vema kiswahili ndani na nje ya nchi.


Mh. Othman alitoa pongezi hizo alipokuwa akifunga kongamano la Saba la kimataifa la baraza la kiswahili Zanzibar (BAKIZA) lililofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil, akimwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, mwanzoni mwa wiki hii Kikwajuni- Unguja.


"Napenda nitumie fursa hii kuzipongeza BAKIZA na BAKITA kwa kueneza kiswahili kitaifa na kimataifa ikiwa pamoja na kufundisha lugha hiyo kwa wageni ndani na nje ya nchi".


Amesema kiswahili kimekuwa na watumiaji wengi duniani ambapo takribani watu milioni 200 wanaitumia lugha hiyo, hivyo amewaasa wataalamu wa lugha hiyo kuendelea kuitumia katika nyanja mbalimbali ikiwemo kuandika vitabu na kuvisambaza.


Aidha Makamu huyo wa Kwanza wa Rais amewataka watumiaji wa lugha hiyo ikiwa pamoja na wanazuoni kuendelea kujifunza zaidi utaalamu katika lugha hiyo ili kuepuka mapungufu katika kuandika na kuzungumza.


" Hata kisu kikali lazima kinolewe. Mimi niliwahi kuwa mwalimu wa kiswahili kabla ya kuingia katika tasinia ya sheria. Lakini hadi leo bado mwanafunzi wa Kiswahili. Hivyo sote kwa pamoja licha ya kukieneza kiswahili lakini bado tunahitajika kujifunza zaidi.


Akimkaribisha mgeni rasmi kuzungumza, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Bi. Tabia Maulid Mwita alitoa wito kuwa vijana wanaotumika katika sanaa za maonyesho kwenye dhifa mbalimbali waendelezwe ili
kusasisha vipaji vyao.


Mapema akitoa taarifa za baraza hilo, Katibu Mtendaji wa BAKIZA Dk. Mwanahija Ali Juma alisema kongamano hilo limehudhuriwa na washiriki kutoka nchi za Sweden, India, Korea kusini, Uganda, Kenya, Komoro, Tanzania bara na Tanzania Visiwani.


Jumla ya maazimo 11 yaliwasishwa na washiriki wa kongamano ikiwemo wanaotafsiri tamthilia mbalimbali watafsiri kwa uhalisia wake ili kuepuka upotoshaji katika matumizi ya lugha.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »