Picha na Lusungu Helela- MNRT
…………………
NA LUSUNGU HELELA-DSM
Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imetaja idadi ya watalii walioingia nchini kuwa imeongezeka kutoka Milioni 1.2 Mwaka 2016 hadi kufikia watalii Milioni 1.3 mwaka 2017 huku watalii kutoka nchini Marekani wakiwa vinara.
Hatua hiyo inakuja ikiwa ni kukua kwa kasi ya uchumi huku ikisaidiwa na ujenzi wa miundombinu ya barabara katika hifadhi za Taifa.
Mbali na idadi hiyo, Serikali imetaja mapato yaliyopatikana kutokana na watalii hao kuwa yameongezeka kutoka wastani wa Dola za Kimarekani Milioni 2.1 Mwaka 2016 hadi kufikia Dola Milioni 2.2 Mwaka 2017.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Maj. Gen. Gaudance Milanzi amesema taarifa ya utafiti huo unaonesha kuwa Tanzania inazidi kufanya vizuri katika sekta ya utalii kwa vile kila mwaka idadi ya watalii na mapato yamekuwa yakiongezeka.
Awali, Milanzi alisema ripoti hiyo ya pamoja iliandaliwa kwa ushirikiano wa Benki Kuu Tanzania(BOT), Tume ya Taifa ya Takwimu(NBS), Idara ya Uhamiaji Zanzibar,
Kwa mujibu wa Milanzi, ripoti hiyo iliyopatikana kutokana na ‘survey’ iliyofanywa katika njia kuu za watalii, ikiwemo viwanja vya ndege pamoja na maeneo ya njia za mipaka ya kuingia nchini, pia imebaini idadi kubwa ya watalii wanaoingia nchini wanatoka katika nchi za Marekani, Uingereza, India, Uholanzi pamoja na Uswiswi.
Katika uzinduzi wa taarifa hiyo Milanzi amesema taarifa hizo zilikusanywa kupitia viwanja vya ndege vya Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), Kilimanjaro(KIA), Abeid Aman Karume(Zanzibar) pamoja na mipaka ya Namanga, Tunduma, Mtukula na kwingineko, kwa kiasi kikubwa imechangiwa na idadi ya watalii walioingia nchini na kutembelea fukwe pamoja wanyamapori
Alisema kimsingi ongezeko la watalii waliongia nchini, pia limetokana na kasi ya kuvitangaza vivutio mbalimbali vilivyopo nchini inayofanywa na Bodi ya Utalii Tanzania(TTB) kupitia mamlaka iliyopewa ya kuvitangaza vivutio hivyo, zikiwemo mbuga za wanyama, fukwe, mlima Kilimanjaro na vinginevyo.
Aidha alisema mbali na vivutio hivyo pia siku za hivi karibuni Tanzania imekuwa ikipata wageni wanaofika nchini kwa ajili ya kupata matibabu katika hospitali zetu mbalimbali, ambao pamoja na huitaji wao katika masuala ya tiba, wanapata fursa ya kufanya utalii na hivyo kuchangia ongezeko katika eneo hilo.
Alisema ujenzi wa miundombinu ya barabara katika Hifadhi za Taifa pia kwa kiasi kikubwa kumechangia kuongeza idadi ya watalii wanaoingia nchini, hatua aliyosema kuwa itazidi kuutangaza utalii wetu.
Naye, Kaimu Mkurugenzi wa Utalii kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii Deograsius Mdamu amesema kwa sasa idara imeanza kuwekeza nguvu katika utalii wa fukwe kwa vile ni aina ya utalii ambao unaonekana kupendwa na watalii wengi wanaongiana nchini.
Wakati huo huo , amesema wanataraji kushirikiana na mamlaka mbalimbali ikiwemo Mamlaka ya Uendelezaji Uchumi(EPZA) katika kutangaza utalii.
Aidha alitaja changamoto mbalimbali zilizokuwa zinazowakabili watalii, ikiwemo masuala ya viza pamoja na huduma za kifedha kupitia utaratibu kadi maalumu, ni maoneo yanayoendelea kufanyiwa kazi na Wizara hiyo ili kuzidi kuutangaza utali hapa nchini.