KOZI YA MAKOCHA WA MCHEZO WA WAVU NGAZI YA MKOA WA TANGA KUANZA MEI 11 MWAKA HUU

May 10, 2018
CHAMA cha mchezo wa Wavu Mkoani Tanga (Tareva) kinatarajiwa kuendesha mafunzo ya waamuzi na makocha yatakayoshirikisha washiriki kutoa wilaya zote mkoani Tanga na kufanyika kwenye shule ya Sekondari Tanga School.
Mafunzo hayo yanatarajiwa kufanyika kuanzia Mei 11 hadi 15 mwaka huu yataendeshwa na Mwamuzi wa Kimataifa wa Mpira wa Wavu Saumu Agapa ambaye anatambuliwa na shirikisho la mpira wa wavu duniani (FIVB) ambaye atashirikiana na Salim Zuberi kocha mwenye levo ya pili.
Akizungumza jana na gazeti hili, Mwenyekiti wa chama hicho mkoani Tanga Augustino Agapa alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwapa ujuzi walimu wa shule za msingi na sekondari.
Alisema baada ya mafunzo hayo anaamini watafanya uamuzi sahihi kwenye shule zao kwa wale wa msingi na sekondari ambao wakati mwengine wanaweza kushindwa kufanya hivyo kutokana na kutokutambua sheria.
Hata hivyo alisema lengo la kutoa mafunzo hayo ni kuhakikisha mchezo huo unachezwa kuanzia ngazi za chini ili vijana waweze kukua nao na baadae waweze kupatikana wachezaji wazuri ambao watakuwa chachu ya mafanikio.
Mafunzo hayo yatawashirikisha walimu wa shule za msingi na sekondari wanaofundisha michezo vikiwamo vilabu,wachezaji wa zamani ambao wapo mkoani Tanga.
“Kama unavyojua tumeamua kuanzia mashuleni kwa sababu huko ndio kisima cha mchezo kutokana na kuwepo kwa vipaji ambavyo vinaweza kuwa hazina kubwa mkoani hapa kwa siku zijazo”Alisema

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »