CANACO YAPEWA SIKU SABA KUWASILISHA MKATABA SERIKALINI

May 06, 2018

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Handeni kwa ajili ya ziara ya siku mbili ya mkoa wa Tanga yenye lengo la kukagua shughuli za madini pamoja na kuzungumza na wananchi tarehe 05 Mei, 2018. Kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe.



Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati mbele) akiendelea na ziara katika eneo la kampuni inayojishughulisha na utafiti wa madini ya dhahabu katika eneo la Magambasi wilayani Handeni ya CANACO Tanzania Limited.



Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ( wa pili kutoka kulia) akitoa maelekezo kwa uongozi wa kampuni inayojishughulisha na utafiti wa madini ya dhahabu katika eneo la Magambasi wilayani Handeni ya CANACO Tanzania Limited.



Mmoja wa watendaji wa kampuni ya Tanzania Gold Field Limited, Robert Slavik (kulia) akielezea namna kampuni yake ilivyoingia makubaliano na kampuni ya CANACO Tanzania Limited kwenye shughuli za uchimbaji madini kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ( wa pili kutoka kulia)



Sehemu wa wananchi wa kijiji cha Nyasa kilichopo wilayani Handeni mkoani Tanga wakifuatilia maelezo yaliyokuwa yanatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara.



Mmoja wa wakazi wa kijiji cha Nyasa kilichopo wilayani Handeni mkoani Tanga, Mhina Kaoneka akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko(hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara.



Mmoja wa wakazi wa kijiji cha Nyasa kilichopo wilayani Handeni mkoani Tanga, Michael Andrea akiwasilisha kero yake kwa Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko(hayupo pichani) kwenye mkutano wa hadhara.



Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akifafanua jambo mbele ya wananchi wa kijiji cha Nyasa kilichopo wilayani Handeni mkoani Tanga (hawapo pichani) kwenye mkutano wa hadhara.



Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe (kushoto) akielezea mchango wa sekta ya madini kwenye wilaya yake mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia).

…………………..

Na Greyson Mwase, Tanga

Mei 05, 2018

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ameipa siku saba kampuni inayojishughulisha na utafiti wa madini ya dhahabu katika eneo la Magambasi wilayani Handeni ya CANACO Tanzania Limited, kuwasilisha mikataba na nyaraka zote kati yake na kampuni ya Tanzania Gold Field Limited ili kubaini namna makubaliano ya mkataba yalivyofanyika ikiwa ni pamoja na ulipaji kodi serikalini,

Biteko aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi wa kijiji cha Nyasa kilichopo wilayani Handeni mkoani Tanga mara baada ya kufanya ziara katika kampuni ya CANACO Tanzania Limited na kutoridhishwa na utendaji wa kampuni hiyo.

Waziri Biteko yupo katika ziara ya siku mbili mkoani Tanga kwa ajili ya kukagua shughuli za madini pamoja na kuzungumza na wananchi na kutatua changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo katika shughuli za madini.

Alisema mara baada ya kufanya ziara katika kampuni ya CANACO Tanzania Limited, amebaini kuwa kampuni hiyo mara baada ya kukamilisha shughuli zake za utafiti wa madini ya dhahabu, kampuni hiyo iliikaribisha kampuni nyingine ijulikanayo kama Tanzania Gold Field Limited ya Canada kwa ajili ya kufanya shughuli za uchimbaji wa madini katika eneo la Magambasi wilayani Handeni mkoani Tanga pasipo kufuata taratibu za kisheria.

Aliendelea kusema kuwa, kampuni ya Tanzania Gold Field Limited iliwataka wachimbaji wadogo waliokuwa wanaendelea na shughuli za uchimbaji madini katika eneo hilo kuondoka ili waanze uchimbaji madini jambo ambalo lilitekelezwa.

Alieleza kuwa, kampuni ya Tanzania Gold Field Limited ilianza shughuli zake bila kuwasilisha makubaliano ya kimaandishi kati yake na kampuni ya CANACO Tanzania Limited Serikalini pamoja na kodi jambo ambalo ni kinyume na sheria za nchi.

Biteko aliendelea kusema kuwa kampuni inayotambulika mpaka sasa kisheria ni ya CANACO Tanzania Limited ambapo shughuli za madini katika eneo la Magambasi zimekuwa zikifanyika bila kufuata sheria na kanuni za mazingira.

“Haiwezekani wachimbaji wadogo ambao ndio wamiliki wa madini ya dhahabu katika eneo la Magambasi wakaondolewa halafu akapewa mwekezaji mkubwa ambaye mpaka sasa hakuna kilichofanyika zaidi ya kuchejua mabaki wa udongo wenye dhahabu na kuuza na kuharibu mazingira huku wachimbaji wadogo wenye uwezo wa kuchimba dhahabu wakihangaika na kuishi katika lindi la umaskini,” alisema Biteko.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Biteko alimtaka Kaimu Afisa Madini Mkazi wa Handeni, Idrissa Yahya kuanza kazi mara moja ya uchambuzi wa vipengele vyote vya sheria na kanuni za madini ili kuangalia namna vilivyokiukwa na kuwasilisha ripoti ofisini kwake.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Godwin Gondwe alimpongeza Naibu Waziri Biteko kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuhakikisha kuwa sekta ya madini inakuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi na kuahidi kuendelea kushirikiana na Wizara ya Madini ili kuimarisha sekta ya madini katika wilaya yake.(Chanzo Fullshangwe Blog)

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »