Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mh.Luhaga Mpina (katikati) kitoa maamuzi ya kuitaka Kampuni ya Game
Tracking Safaris(TGTS) kuondoka katika eneo la hekta 20000 kwenye
vitalu tisa vilivyomo kwenye Ranchi ya Uvinza ifikapo tarehe 1/1/2018.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mh.Luhaga Mpina akizungumuza na Meneja wa Kampuni ya Game Tracking
Safaris(TGTS) Audax Kalulama katika simu alipotembelea Ranchi ya Uvinza
leo na kuamuru mwekezaji huyo kuondoka kabla ya Januari Mosi mwakani
kutokana na Mwekezaji huyo kukaa katika eneo hilo kinyume cha Sheria.
Sehemu ya Ranchi ya Uvinza.
.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi
Mh.Luhaga Mpina (katikati) akiwasikiliza walinzi wa Kampuni ya Game
Tracking Safaris(TGTS) hawapo pichani wakitoa maelezo alipotembelea
Ranchi ya Uvinza .
…………………………………………………………………….
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mh.
Luhaga Mpina ameutaka uongozi wa Kampuni ya Game Tracking
Safaris(TGTS) kuangalia na kupitia nyaraka walizonazo ili kuona
uhalali wa umiliki wa eneo la hekta 20000 kwenye vitalu tisa vilivyomo
kwenye Ranchi ya Uvinza inayomilikiwa na Kampuni ya Ranchi za za Mifugo
za Taifa (NARCO)kabla ya Selikali kuwatoa kwa nguvu ifikapo tarehe
1/1/2018.
Waziri Mpina ametoa maelekezo
hayo leo alipotembelea Ranchi ya Uvinza kuangalia shughuli mbalimbali
katika Ranchi hiyo ambapo ametoa muda wa hadi Januari mosi mwakani kwa
mwekezaji huyo kuondoka katika eneo hilo endapo atabaini kuwa amekuwa
akikaa kimakosa kuanzia katika vitalu namba 41 hadi 49.
Aidha Waziri Mpina amesema
endapo Mwekezaji huyo ataendelea kubaki baada ya tarehe Mosi Januari,
Serikali itamuondoa kwa nguvu na atatakiwa kulipa gharama zote za
fidia na usumbufu.
“Ninakuagiza angalia taarifa
mbalimbali ulizonazo kuhusu umiliki wa eneo hili kama utaona
umeendelea kukaa hapa bila kufuata taratibu tafadhali uondoke mara
mmoja ili kupisha Serikali kuendelea na shughuli zake” alisisitiza Mpina
Waziri Mpina amemuagiza Meneja
Mkuu wa NARCO, Profesa Philemoni Wambura kuwaandikia barua ya
kuwaondoa wawekezaji wote katika Ranchi hiyo ambao hawajaendeleza kwa
zaidi ya asilimia 40 na kwamba wawekezaji ambao wamewekeza kwa zaidi ya
asilimia arobaini wanatakiwa kukamilisha malipo yote kabla ya Januari
mosi mwakani.
Alionya wawekezaji kuacha tabia
ya kuidanganya serikali kwamba wanauwezo wa kuwekeza katika vitalu ili
wapewe lakini wanabadili matumizi baada ya kupewa. Aliongeza kwamba
Serikali imegundua baadhi ya wawekezaji wanaopewa vitalu wanawakodisha
wafugaji kutoka nchi jirani na kujipatia faida wakati Serikali haipati
chochote.
Awali, Meneja wa (TGTS) Audax
Kalulama akizungumza kwa simu na Waziri Mpina kutoka Arusha amesema
kwamba eneo hilo wanamiliki kihalali na kuomba muda ili wawasiliane na
Wizara ya Mifugo kuonyesha taarifa za umiliki wa eneo hilo.