TAARIFA KUTOKA NDANI YA SHIRIKISHO LA SOKA TANZANIA (TFF)

July 20, 2017
TAARIFA YA KAMATI YA UCHAGUZI TAFCA

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA), Ramadhani Mambosasa ametangaza majina manane ya wagombea waliopitishwa katika usaili katika mchakato uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Agosti 10, mwaka huu mjini Dodoma.

Waliopitishwa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi - ngazi ya taifa ni pamoja na Kidao Wilfred, Lisiter Manyara, Michael Bundala, Dismas Haonga, Jamhuri Kihwelo, George Komba, Samuel Moja na Mwalwasi.

Nafasi zinazowaniwa ni Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Katibu Mkuu, Katibu Msaidizi, Mweka Hazina, Wajumbe wa Mkutano Mkuu TFF na Wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

WAGANDA KUWACHEZESHA RWANDA, TANZANIA

Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), limewateua waamuzi wa Uganda kuchezesha mchezo wa marudiano kati ya Amavubi ya Rwanda na Taifa Stars ya Tanzania. Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza timu hizo zilitoka sare ya 1-1.

Mchezo huo utakaofanyika Uwanja wa Nyamirambo, Jumamosi saa 10.00 jioni kwa saa za Rwanda sawa na saa 9.00 alasiri kwa saa za Tanzania, utachezeshwa na Brian Nsubuga Miiro ambaye atakuwa na jukumu la kupiliza kipenga.

Waamuzi wasaidizi watakuwa Ronald Katenya (Line 1) na Dick Okello (Line 2) wakati Mwamuzi wa akiba atakuwa Chelanget Ali Sabila huku Kamishna wa mchezo atakuwa Ali Mohamed Ahmed kutoka Somalia.

Mchezo huo ni wa kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani (CHAN). Timu hiyo kwa mwaka huu imecheza mechi 10 za kimataifa na kushinda mitano; kutoka sare minne na kufungwa mmoja wa nusu fainali za Cosafa.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »