Waganga Wakuu wa Mikoa waagizwa kuhakiki takwimu za chanjo

September 15, 2016
Na Beatrice Lyimo
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amewaagiza Waganga Wakuu wa Mikoa kuhakiki takwimu za chanjo na kuzitawanya wilaya kwa wilaya ili kuhakikisha vituo vyote vinapata chanjo zilizopo.
Waziri Ummy ametoa agizo hilo leo mjini Dodoma alipokuwa akitoa taarifa kuhusu upungufu wa baadhi ya chanjo katika baadhi ya vituo vya kutolea huduma za afya nchini.
Waziri Ummy amesema kuwa licha ya kuwa na uhaba wa chanjo, kuna baadhi baadhi ya wilaya ambazoo chanjo ya aina moja haipo wakati wilaya nyingine chanjo hiyo ipo.
“Licha ya uhaba wa chanjo, kuna baadhi ya wilaya ambazo chanjo ya aina moja haipo ila wilaya nyingine chanjo hiyo ipo, kwa mfano chanjo ya kifua kikuu kwa manispaa ya Dodoma, kuna chanjo dozi 6540 wakati wilaya za Bahi, Chamwino na Chemba hakuna kabisa chanjo hiyo”, amefafanua Waziri Ummy..
Hata hivyo Waziri Ummy amewataka Waganga hao Wakuu wahakikishe wanapitia takwimu hizo ndani ya mikoa yao ili kuweza kuzitawanya chanjo hizo kwenye wilaya zote ambazo hazina au zenye  upungufu.
Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa ili kukabiliana na upungufu chanjo nchini, Wizara hiyo imenunua na inategemea kupokea chanjo kiasi cha dozi milioni mbili za kinga dhidi ya Kifua Kikuu (BCG) Septemba 28, mwaka huu, chanjo ya Polio dozi milioni mbili Septemba 19, 2016 na chanjo ya Pepopunda dozi 1,240,000 Septemba 26, mwaka huu.
Pia Waziri Ummy amesema kuwa Wizara imepokea fedha kutoka Hazina kwa ajili ya ununuzi wa chanjo nyingine za Surua na Rubella na zitategemewa kutumwa Shirika la Kimataifa la Kuhudumia Watoto Duniani (UNICEF) mbao ndio wanunuzi wa chanjo nchini.
Mbali na hayo Wizara hiyo inaendelea kuwahimiza wananchi hasa wazazi na walezi wenye watoto wa umri wa kupata chanjo, kuwa mara wapatapo taarifa ya uwepo wa chanjo zilizokosekana wawapeleke watoto wao ambao hawakupata chanjo au kukamilisha chanjo kulingana na ratiba ili kuweza kukamilisha chanjo zao na kuwahakikishia usalama wa afya watoto wao.  
Zaidi ya hayo, Serikali inawahakikishia wananchi wote kuwa huduma za afya ikiwemo chanjo zinaendelea kutolewa nchini bure, hivyo wananchi waendelee kutumia huduma hizo wakati wote kwani chanjo ni haki ya msingi kwa kila mtoto.
Chanjo ambazo zilikuwa na upungufu nchini ni pamoja na chanjo kwa ajili ya kukinga ugonjwa wa Surua na Rubella (MR) Kifua Kikuu (BCG), Polio (OPV) na Pepopunda (TT) ambazo hutumika kwa watoto kuanzia wanapozaliwa hadi miaka miwili na kina mama wajawazito kulingana na mwongozo wa chanjo uliotolewa na Wizara ya Afya ili kuwakinga na magonjwa hayo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »