SERIKALI ITAENDELEA KUSIMAMIA HAKI ZA MTOTO WA KIKE

May 04, 2016

download 
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO, Dodoma
…………………………………………..
Serikali itaendelea kusimamia haki ya mtoto wa kike ya kupata elimu na kuwachukulia hatua kali za kisheria ikiwemo kuwapeleka mahakamani wale wote wanaowapa ujauzito wanafunzi na kuwakosesha kupata elimu ambayo ni haki yao ya msingi.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Seriklali za Mitaa (TAMISEMI) Seleman Jafo alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Janeth Mbene wa Ileje baada ya kujibu swali la msingi lililohoji kuhusu kushuka kwa kiwango cha elimu nchini.
“Serikali haitamvumilia mwanaume yeyote atakayempa ujauzito mwananfunzi na kukwamisha kupata elimu kwa wakati na kumharibia malengo ya maisha yake” alisema Naibu Waziri Jafo.
Hatua hiyo ya Serikali itawahakikishia na kuwawezesha watoto wa kike nchini kusoma na kumaliza masomo yao hatua ambayo itakuwa msaada kwa watoto hao wa kike, familia zao na taifa kwa ujumla.
Akisistiza msimamo wa Serikali kuhusu wanaume wanaowapa ujauzito wanafunzi, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu alisema kuwa Serikali haipo tayari kuwavumilia wanaume wenye tabia ya kuwakwamisha watoto wa kike kupata elimu kwa kuwapa ujauzito na itahakikisha sheria inachukua mkondo wake ili kukomesha tabia hiyo.
Akizungumzia tatizo hilo la wanafunzi kupata ujauzito wakiwa shuleni, Mbunge wa Jimbo la Igunga Seif Khamis Gulamali alisema kuwa tatizo hilo lipo sehemu mbalimbali nchini ambapo watoto hubebeshwa mimba wakiwa katika umri mdogo wa kuwa shuleni na tatizo hilo linaendelea kuleta hasara kubwa kwa wanafunzi wenyewe, familia zao na taifa kwa ujumla.
Gulamali alisema kuwa hali hiyo inatokana na hulka ya makabila mengi nchini hasa ya wafugaji hali inayosababishwa na tabia ya kuhama hama kutafuta malisho na maji kwa ajili ya mifugo yao.
“Wapo wazazi wanaowapa maelekezo watoto wao wasifaulu mitihani yao ili waweze kuolewa na wamegeuzwa kuwa sehemu ya kipato cha familia zao kwa kupata mahari” alisema Gulamali.
Ili kukomesha tabia hiyo ya kuwapa ujauzito watoto wenye umri mdogo hasa kwa wafugaji, Gulamali alisema kuwa ipo haja ya Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi pamoja na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuweka mazingira mazuri ambayo yatawapa wananchi wengi fursa ya  kuwekeza kwenye sekta ya kilimo na mifugo kwa kuwahakikishia upatikanaji wa maji kwa wingi ili wananchi wazalishe na kuondokana na tabia ya kuhama hama kwa wazazi wao ambayo imekuwa kikwazo kikubwa kwa watoto kupata elimu.
Kuhusu shilingi milioni 50 zilizoahidiwa na Serikali kwa kila kijiji hapa nchini, Gulamali alisema kuwa ni vema ufikiriwe mfumo wa kupeleka hizo fedha ambao utakuwa wa tija kwa wananchi na taifa kwa ujumla utakaohkikisha fedha hizo zitakuwa endelevu na kuwarahisishia wananchi kazi na kuongeza uzalishaji wa mazao yatakayowaongezea kipato.
Hatua hiyo itasaidia taifa kuwa na matumizi bora ya rasilimali fedha zinazotolewa na Serikali kwa kuwekeza kwenye sekta za viwanda, mifugo, uvuvi na kilimo ambapo Tanzania kuna mvua ya kutosha, mabonde yenye rutuba, mito, maziwa, bahari pamoja na watu ambao ndio msingi wa maendeleo kwa taifa kwa kuongozwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa ifikapo 2025 Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »