Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu),Jenista
Mhagama,akizungumza katika katika uzinduzi wa matokeo ya utafiti wa watu
wenye uwezo wa kufanya kazi wa mwaka 2014. Uzinduzi huo ulifanyika
katika Viwanja vya Karimjee,Dar es Salaam, jana. Kulia ni Mkurugenzi wa
Sensa ya watu na Takwimu za Jamii,Ephraim Kwesigabo na Mkurugenzi Mkuu
wa Takwimu nchini,Dk.Albina Chuwa.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
(Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu),Jenista
Mhagama,akionesha ripoti ya matokeo ya utafiti wa watu wenye uwezo wa
kufanya kazi wa mwaka 2014 katika Viwanja vya Karimjee,Dar es Salaam,
jana. Wengine wanaoshuhudia ni kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa
Takwimu nchini,Dk.Albina Chuwa, Mkurugenzi wa Sensa ya watu na Takwimu
za Jamii,Ephraim Kwesigabo na Mwakilishi kutoka Shirika la Kazi
Duniani,Marry Kawar.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu (Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu),Jenista
Mhagama,akizindua ripoti ya matokeo ya utafiti wa watu wenye uwezo wa
kufanya kazi wa mwaka 2014 katika Viwanja vya Karimjee,Dar es Salaam, .
Wengine wanaoshuhudia ni kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Takwimu
nchini,Dk.Albina Chuwa, Mkurugenzi wa Sensa ya watu na Takwimu za
Jamii,Ephraim Kwesigabo na Mwakilishi kutoka Shirika la Kazi
Duniani,Marry Kawar.
………………………………………………………………………………………………………………..
Na Raymond Mushumbusi – MAELEZO
Utafiti uliofanyika hivi
karibuni na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) umebaini kwamba asilimia 71
ya watanzania wanatumia muda mwingi kufanya shughuli zisizokuwa za
uzalishaji mali wala tija binafsi kwao na Taifa kwa ujumla
Akizundua taarifa ya utafiti
huo leo jijini Dar es salaam Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
Sera,Bunge,Kazi,Ajira,Vijana na watu wenye ulemavu Mhe. Jenista Mhagama
amesema kuwa idadi hiyo hufanya kazi zisizoleta tija kwao na taifa na
muda mwingi huutumia kujihudumia binafsi kwa kulala na starehe nyingine.
Ameeleza kuwa takwimu hizo
zinaonesha wazi ni kwa namna gani watanzania wanashindwa kujishughulisha
katika kufanya kazi zenye kuwaingizia kipato na badala yake wanatumia
muda wao mwingi kufanya shughuli zisizo za uzalishaji hasa kufanya
starehe mbalimbali.
“ Ndugu zangu watanzania
unakuta mtu amekaa baa au anacheza “poll table” kuanzia asubuhi mpaka
jioni na hujui anafanya kazi gani ya uzalishaji, ndugu zangu tuone aibu
basi tujishugulishe tulijenge taifa letu ili kujiletea maendeleo yetu na
nchi yetu.”
Aidha, matokeo hayo
yamebainisha kuwa asilimia 18.5 ya wananchi wanafanya kazi za uzalishaji
na asilimia 10.6 ni wale wanaofanya shughuli za nyumbani zisizo na
malipo huku uchambuzi wa kijinsia ukionesha kuwa wanaume asilimia 23.8,
wanatumia muda mwingi kwenye shughuli za kiuchumi ikilinganishwa na
asilimia 13.5 ya wanawake.
Amefafanua kuwa wanawake ambao
ni asilimia 16.5 katika utafiti huo wanatumia muda mwingi kufanya kazi
za nyumbani zisizo na malipo ikilinganishwa na asilimia 4.4 ya wanaume.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu
wa Ofisa ya Taifa ya Takwimu (NBS) Dkt. Albina Chuwa amesema kuwa
upatikanaji wa Takwimu hizo utaisaidia Serikali kupata mbinu sahihi za
kuondokana na tatizo la ajira nchini kwa kuunganisha nguvu kutoka sekta
isiyo rasmi ili kuleta changamoto katika soko la ajira nchini.
Amesema kuwa hii ni mara ya
tano Tanzania inafanya utafiti huo na kubainisha kuwa ulianza mwezi
Januari hadi Desemba, 2015 ukitumia sampuli ya Sensa ya Watu na Makazi
ya mwaka 2012 iliyotumika kupata taarifa sahihi ya takwimu hizo.
Aidha, amebainisha kuwa ili
kufanikisha utafiti huo NBS imeshirikiana na wadau mbalimbali ikwemo
Wizara ya kazi na Ajira,Shirika la Kazi Duniani (ILO),Benki ya Dunia
(WB),Benki ya Maendeleo ya Afrika(ADB) na Asasi zisizo za Kiseikali.