Katibu
Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa(TAMISEMI), Jumanne Sagini wakati akizungumza na watendaji
mbalimbali wa ofisi hiyo leo katika mkutano wa kikazi uliofanyika kwenye
ukumbi wa mikutano wa Karimjee jijini Dares Salaam , ambapo lengo kuu
lilikuwa ni kutoa maelekezo ya utendaji kazi kama ilivyoagizwa na Waziri
Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa.Kulia ni Naibu Katibu Mkuu Afya -TAMISEMI
,Dkt .Deo Mutasiwa .
Baadhi
ya watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za
Mitaa(TAMISEMI) wakimsilikiza Katibu Mkuu wa ofisi ambaye hayupo
pichani.
Na Magreth Kinabo – maelezo
SERIKALI
imewataka watendaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini kuhakikisha
kwamba wanafanyakazi kwa uadilifu weledi wa taaluma zao na kufuata
sheria zilizopo katika kusimimia suala la usafi wa mazingira, likiwemo
la kudhibiti biashara holela, gereji bubu,uegeshaji wa magari holela.
Pamoja
na hayo wasimamie, upigaji holela wa muziki katika vilabu, baa na kumbi
zaidi ya saa zilizopangwa na kuzuia bodaboda zinazosafirisha abiria
hadi maeneo ya miji katikati, pia kuzuia ujenzi holela.
Kauli
hiyo imetolewa leo na Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), Jumanne Sagini wakati akizungumza
na watendaji mbalimbali wa ofisi hiyo katika mkutano wa kikazi
uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Karimjee, jijini Dar es Salaam
ambapo lengo kuu lilikuwa ni kutoa maelekezo ya utendaji kazi kama
ilivyoagizwa na Waziri Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa.
Akizungumzia
kuhusu suala la usafi wa mazingira kufuatia ziara iliyofanyika hivi
karibuni imeonekana kuwa na changamoto mbalimbali alisema;
“Kazi
zetu haziendi vizuri kwa sababu hatusimamii sheria zilizopo ndio
kumekuwa na malalamiko katika utendaji wa kazi zetu, mfano katika suala
la gharama za usimamizi wa usafi wa mazingira ni kubwa . Lakini
kinachofanyika ni kweli kinalinganishwa na gharama hizi?” alihoji Katibu
Mkuu huyo.
Akitolea
mifano gharama zinazotumika katika suala hilo, kwa kipindi cha mwaka wa
fedha wa 2014/2015 alisema kwa upande wa manispaa ya Kindondoni
wanatumia Sh. bilioni 2.6, Ilala ni Sh. bilioni 2.6, wakati Temeke
wanatumia Sh. bilioni 1.2 .
“Kilichobainika
ni kwamba mikataba ya watu wanaojishughulisha na usimamizi wa usafi wa
mazingira ni ya mwaka mmoja na wanaopewa mikataba hiyo ni watu ambao
hawana uwezo wa kutosha wa kutekeleza jukumu hilo.
“ Ama
watu wasio na uwezo ama mnaofahamiana nao. Au kampuni zenye mahusiano na
baadhi ya watumishi wa mamlaka za serikali za mitaa au wenye uhusiano
na viongozi wenu, Jiepusheni na kuwapa watu hawa kwa sababu kutokana na
hali hiyo hamtaweza kukabiliana nao. Kama kuna kiongozi ambaye mmepatia
nafasi hii lazima athibitishe kuwa na uwezo. Na kama pia ni miongoni
mwenu hakikisheni kuwa ni mtu mwenye uwezo. Kazi zetu haziendi vizuri
kwa sababu ya nasaba au viongozi wenu,” alisisitiza Katibu Mkuu huyo,
huku akisema lazima wabadilike na kuangalia kama hawana uwezo wajitoe au
wafukuzwe.
Aliongeza
kwamba katika suala hilo kumekuwa na migongano ya watumishi wa
halmashauri ambao wanatakiwa kufanya kazi kama timu; mfano maafisa afya,
mazingira na usafishaji, lakini akasema wanaonana kama maadui.
“ Hawa
wangepaswa kufanya kazi kwa kushirikiana ,lakini ni maadui kwa sababu
ya maslahi … hili ni lenu wakurugenzi kwani hata watoto wako
wakisambaratika ni lazima huwaketishe chini ili mambo yaende,
asiyekubali unamwajibisha,” alisema.
Sagini
alisema watendaji hao , wote ni wadau wa usafi, hivyo wanapaswa kufanya
kazi kwa ushirikiano, hivyo aliwataka wapeane mikono katika kikao
hicho, ambapo walifanya hivyo ikiwa ni hatua ya kuonesha ushirikiano.
Pia
alisema watu wanaosafirisha bidhaa za vyakula kwa kutumia majani ya
migomba au matenga wasiruhusiwe kufanya hivyo wapewa muda wa wiki moja
au mbili kutumia utaratibu mwingine.
Aliwataka
pia watendaji mbalimbali wa TAMISEMI kuwa na ushirikishwaji katika
ngazi za chini kwenye halmashauri kwa kuwa haliko vizuri.
Sagini
alisema ni vizuri kukawekwa mfumo wa TAMISEMI wa kushirikisha ngazi za
chini kama ilivyo kwa mjumbe wa nyumba kumi kwenye masuala ya vyama.
“ Ni
lazima tuingie katika mfumo huu wa kuwa na watendaji wa kaya 30 ambao
watakuwa chini ya TAMISEMI . Suala hili lina faida ya ulinzi na usalama
na kuwatambua wageni… tunaangalia jinsi ya kulitekeleza,” alisema.
Aliwataka
wakurugenzi wasikae maofisini kwenye madawati bali watembelee maeneo
mbalimbali ili kutatua kero za wananchi na kuangalia mipangilio ya miji
na majiji.
Katika
suala hilo la usafi wa mazingira alisema mtu mwenye uwezo wa kusafisha
jiji liwe safi apewe nafasi huku akisisitiza suala la kushirikisha sekta
binafsi ni muhimu katika mambo mbalimbali likiwemo la ujengaji wa
maegesho ya magari, ambapo sasa yanahitajika kwa ajili ya mradi wa
mabasi yaendayo haraka(DART).
“
Kwenye eneo hili la DART lazima mbadilike tunataka barabara za DART ziwe
nyeupe yaani watu wasifanye biashara,” alisisitiza huku akitaka kuanzia
Jumatatu wiki ijayo yatekelezwe.
Aliwataka watu wanaohusika na vyombo vya usafiri na usafirishaji kutovunja sheria, akatolea mfano boda boda.