NHIF kuwekeza Vituo vya mfano Kigoma, Mtwara

October 22, 2015

1 2
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Michael Mhando (meza kuu katikati) akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mikakati ya Mfuko huo ya ujenzi wa Vituo vya mfano vya matibabu.
……………………………………………………………………..
Na Mwandishi wetu. MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) unatarajia kuanza ujenzi wa vituo vya matibabu vya mfano katika mikoa ya Mtwara na Kigoma katika mwaka huu wa fedha wa 2015/2016.
Mikakati hiyo imesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Michael Mhando wakati akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana kuhusiana na mikakati ya Mfuko katika uboreshaji wa miundombinu ya Matibabu.
“Tunatarajia kuwanza ujenzi wa Kituo cha matibabu cha mfano mkoani Mtwara na hasa kwa kuzingatia kuwa Wizara yetu ya afya pia inao mpango wa kujenga Hospitali mkoani humo. Tunawasiliana na Wizara ili tuunganishe nguvu zetu. Eneo tayari lipo na Mfuko umetenga kiasi cha Tsh bilioni 3 kwa mwaka 2015/16, lakini pia ujenzi Kituo cha Matibabu cha Mfano Mkoani Kigoma ambacho kitatoa huduma kwa wanachama na wananchi wa mkoa huo na mikoa ya jirani,” alisema Bw. Mhando.
Aidha Mfuko umejipanga kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Mkoa wa Dar es Salaam ambapo umeanza kushirikiana na Uongozi wa mkoa ili kuziwezesha hospitali za Amana, Mwananyamala na Temeke kuwa na vifaa vya kisasa zaidi ili kuhudumia wanachama wengi kupitia huduma za matibabu na kliniki maalum zitakazokuwa zinaendeshwa na madaktari bingwa wa hospitali hizo.
“Katika Jiji la Dar es Salaam mfuko utajenga kituo cha madaktari bingwa (Doctors Plaza) katika eneo la Ubungo Maziwa ambako mfuko utaweka pia miundo mbinu kwa ajili ya huduma mbalimbali. Kituo hicho kitawawezesha wanachama na wananchi kupata huduma za kuwaona madaktari bingwa wa fani mbalimbali kwa urahisi na katika eneo moja, hali ambayo itapunguza msongamano wa wagonjwa katika baadhi ya vituo na kuboresha huduma jijini.
Bw. Mhando alisema kuwa mbali na juhudi za uboreshaji wa huduma za afya zilizotajwa hapo juu, Mfuko pia umewekeza katika ujenzi wa Ofisi zake katika Mikoa ya Mbeya, Dodoma na Tabora ambapo majengo hayo yatawezesha upatikanaji wa nafasi kwa huduma za Hospitali za Doctors Plaza ambazo zimekuwa zikihudumia wanachama wengi wa Mfuko.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »