Mama Samia Suluhu Asimikwa Umalkia Wilayani Maswa, Wamwita ngole

October 03, 2015

New Picture (1)
Mgombea mwenza wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa nafasi ya urais, Mama Samia Suluhu Hassan (kulia) akisimikwa kuwa Malkia wa Wasukuma Wilaya ya Maswa na akinamama wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania ya CCM (UWT) alipowasili Jimbo la Maswa Mashariki kufanya mkutano wa hadhara wa kampeni kunadi ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa wanaMaswa.
………………………………………………………………………………….
Na Thehabari.com
MGOMBEA mwenza wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa nafasi ya urais, Mama Samia Suluhu Hassan leo amepewa heshima ya kusimikwa kuwa malkia wa Wasukuma Wilaya ya Maswa na kupewa jina jipya la Ng’walu Majura.
Mama Samia Suluhu amepewa heshima hiyo leo na Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania ya CCM (UWT) alipowasili Jimbo la Maswa Magharibi kufanya mkutano wa hadhara wa kampeni kunadi ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa wanaMaswa.
Mama Suluhu ambaye amepewa jina jipya la heshima hiyo la Ng’walu Majura alivishwa mavazi maalum ya kimila ya heshima ‘Ngole’ yaani malkia na kukabidhiwa mkuki maalum, ungo na usinge pamoja na kupewa zawadi anuai za vyakula vya kimila kwa kabila la Wasukuma eneo hilo.
Wakimpa heshima hiyo akinamama wa UWT walisema Mama Samia Suluhu amepewa heshima hiyo kwa kuwa ni mwanamke aliyekuja kuibua mambo mazuri kwa ushindi wa CCM na Tanzania kwa wanawake. Akinamama hao waliahidi kumuunga mkono ili kuhakikisha anashinda na kuwatoa kimasomaso Wanawakea wa Tanzania.
Kwa upande wake Mama Samia Suluhu amewashukuru akinamama hao kwa heshima na zawadi mbalimbali walizompa na kuwaahidi kupigania maslahi yao zaidi endapo chama chake kitafanikiwa kuunda Serikali katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25, 2015. Alisema licha ya kupigania maendeleo ya taifa zima yeye kama mwanamama ana ajenda maalum za kuwapigania akinamama kuanzia huduma za kijamii hadi uwezeshwaji kwao ili kuleta usawa na maendeleo kwa jamii hiyo.
Alisema amepokea kilio cha maji Maswa na kwa kuwa wanawake ndio waathirika wakubwa wa ukosefu wa maji atahakikisha Maji yanapatikana kupitia miradi anuai inayotekelezwa eneo hilo na kwa kuanzia watachimba visima 10 maeneo mbalimbali ya Maswa ili kuwapatia maji wakazi wa maeneo hayo.
Mapema majira ya asubuhi Mama Samia Suluhu alifanya mkutano wa kampeni katika Jimbo la Meatu akiinadi ilani ya CCM kwa wananchi, ambapo aliwaomba kuichagua CCM kwani imepanga kufanya mengi kwa wanaMeatu ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya barabara, ujenzi wa malambo na majosho kwa ajili ya kuhudumia mifugo yao.
Alisema ili kuondoa migogoro kwa wafugaji na wakulima safari hii Serikali itakayoundwa na CCM imepanga kupima ardhi yote ya vijiji na Wilaya na kisha kuainisha mipaka ya wakulima na wafugaji na kuwamilikisha jamii hizo kumaliza migogoro.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »