Mgombea mwenza wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) wa nafasi ya urais, Mama Samia Suluhu Hassan (kulia)
akisimikwa kuwa Malkia wa Wasukuma Wilaya ya Maswa na akinamama wa
Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania ya CCM (UWT) alipowasili Jimbo la
Maswa Mashariki kufanya mkutano wa hadhara wa kampeni kunadi ilani ya
Chama Cha Mapinduzi kwa wanaMaswa.
………………………………………………………………………………….
Na Thehabari.com
MGOMBEA mwenza wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) wa nafasi ya urais, Mama Samia Suluhu Hassan leo amepewa
heshima ya kusimikwa kuwa malkia wa Wasukuma Wilaya ya Maswa na kupewa
jina jipya la Ng’walu Majura.
Mama Samia Suluhu amepewa heshima
hiyo leo na Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania ya CCM (UWT)
alipowasili Jimbo la Maswa Magharibi kufanya mkutano wa hadhara wa
kampeni kunadi ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa wanaMaswa.
Mama Suluhu ambaye amepewa jina
jipya la heshima hiyo la Ng’walu Majura alivishwa mavazi maalum ya
kimila ya heshima ‘Ngole’ yaani malkia na kukabidhiwa mkuki maalum, ungo
na usinge pamoja na kupewa zawadi anuai za vyakula vya kimila kwa
kabila la Wasukuma eneo hilo.
Wakimpa heshima hiyo akinamama wa
UWT walisema Mama Samia Suluhu amepewa heshima hiyo kwa kuwa ni mwanamke
aliyekuja kuibua mambo mazuri kwa ushindi wa CCM na Tanzania kwa
wanawake. Akinamama hao waliahidi kumuunga mkono ili kuhakikisha
anashinda na kuwatoa kimasomaso Wanawakea wa Tanzania.
Kwa upande wake Mama Samia Suluhu
amewashukuru akinamama hao kwa heshima na zawadi mbalimbali walizompa na
kuwaahidi kupigania maslahi yao zaidi endapo chama chake kitafanikiwa
kuunda Serikali katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 25, 2015.
Alisema licha ya kupigania maendeleo ya taifa zima yeye kama mwanamama
ana ajenda maalum za kuwapigania akinamama kuanzia huduma za kijamii
hadi uwezeshwaji kwao ili kuleta usawa na maendeleo kwa jamii hiyo.
Alisema amepokea kilio cha maji
Maswa na kwa kuwa wanawake ndio waathirika wakubwa wa ukosefu wa maji
atahakikisha Maji yanapatikana kupitia miradi anuai inayotekelezwa eneo
hilo na kwa kuanzia watachimba visima 10 maeneo mbalimbali ya Maswa ili
kuwapatia maji wakazi wa maeneo hayo.
Mapema majira ya asubuhi Mama
Samia Suluhu alifanya mkutano wa kampeni katika Jimbo la Meatu akiinadi
ilani ya CCM kwa wananchi, ambapo aliwaomba kuichagua CCM kwani imepanga
kufanya mengi kwa wanaMeatu ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya
barabara, ujenzi wa malambo na majosho kwa ajili ya kuhudumia mifugo
yao.
Alisema ili kuondoa migogoro kwa
wafugaji na wakulima safari hii Serikali itakayoundwa na CCM imepanga
kupima ardhi yote ya vijiji na Wilaya na kisha kuainisha mipaka ya
wakulima na wafugaji na kuwamilikisha jamii hizo kumaliza migogoro.
*Imeandaliwa na www.thehabari.com