PINDA ATETA NA WAZIRI MKUU WA UGANDA

August 21, 2015

download (6)
*Asema Tanzania kuadhimisha miaka 100 ya Maskauti mwaka 2017
……………………………………………………………
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amekutana na Waziri Mkuu wa Uganda, Dk. Ruhakana Rugunda na kufanya naye mazungumzo kuhusiana na masuala mbalimbali yahusuyo nchi hizi mbili.
Akizungumza na mwenyeji wake jana jioni (Alhamisi, Agosti 20, 2015), kwenye kikao kilichofanyika Ofisi ya Waziri Mkuu wa Uganda jijini Kampala, Waziri Mkuu alisema amefurahishwa na juhudi zinazofanywa kwenye mipaka ya nchi hizo mbili na hasa mpaka wa Mutukula.
“Nimearifiwa kwamba juhudi za ujenzi wa one-border-post pale Mtukula zinaendelea vizuri. Tunachotakiwa kufanya kwa sasa ni kuangalia kwa kiasi gani tunaweza kutumia kituo hiki kama fursa ya kukuza biashara baina ya nchi zetu mbili,” alisema.
Alisema masuala ya kuimarisha uchumi ni ya msingi na hayana budi kupewa kipaumbele katika kipindi hiki cha sasa. “Kikubwa ni kwa nchi zetu kuendelea kuimarisha amani iliyopo kwa faida ya wananchi wake, maana bila amani hakuna kitakachofanyika,” alisema.
Waziri Mkuu Pinda alitumia fursa hiyo kumtakia heri yeye na wananchi wa Uganda wakati wakijiandaa kufanya Uchaguzi Mkuu ujao unaotarajiwa kufanyika Februari, 2016.
Pia alimwalika Waziri Mkuu wa Uganda aje kutembelea Tanzania pindi apatapo nafasi ya kufanya hivyo.
Naye Waziri Mkuu wa Uganda, Dk. Rugunda alisema nchi yake bado inatambua na inathamini mchango wa Tanzania katika kuleta amani nchini mwao.
“Tanzania itaendelea kukumbukwa na Waganda kwa mchango mlioutoa katika harakati za kuikomboa Uganda kutoka kwenye makucha ya Iddi Amin Dada. Maneno aliyokuwa akiyasema mwalimu Nyerere bado yamo akilini mwetu na yanaendelea kuishi mioyoni mwa Waganda wengi,” alisema.
“Waganda wengi wanaiona Tanzania kama ni nyumba yao ya pili (second home) na wanafurahia wanapokuja huko akiwemo Rais wetu, Mheshimiwa Yoweri Kaguta Museveni. Sote tunathamini mchango wa Tanzania na tutaendelea kuuezi,” alisema Dk. Rugunda.
Alisema yeye binafsi anafurahi kwamba Tanzania na Uganda zimeunganishwa kwa njia ya kieletroniki (mtandao na mawasiliano ya simu); lakini akaongeza kuwa kiasili, nchi hizo zimeunganishwa kwa njia ya barabara na maji kupitia Ziwa Victoria na kwamba ana imani uhusiano uliopo utaendelea kudumu vizazi na vizazi.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema Tanzania itaadhimisha miaka 100 ya Chama cha Maskauti cha Tanzania ifikapo Agosti, 2017. “Hivi sasa tunao maskauti wapatao 800,000 nchi nzima lakini lengo letu ni kufikisha maskauti milioni moja ifikapo mwaka 2017 kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 100 nchini kwetu,” alisema.
Waziri Mkuu Pinda aliwasili nchini Uganda Jumatano usiku kwa ziara ya siku moja akimwakilisha Rais Jakaya Kikwete kwenye maadhimisho ya miaka 100 ya Chama cha Maskauti cha Uganda (Uganda Scouts Association – USA). Amerejea nchini jana usiku.
Rais Yoweri Museveni ndiye mlezi wa chama hicho na alikuwa amemwalika Rais Kikwete kwenye maadhimisho hayo.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »