WAZIRI SITTA ATEMBELEA BANDAR YA TANGA,AFURAHISHWA NA UTENDAJI WAO

June 04, 2015
SERIKALI imesisitiza mpango wa ujenzi wa Bandari mpya ya Mwambani mkoani Tanga si kutokana na kuwepo kwa kina kirefu tu cha maji bali kuhakikisha kuwa inatumika kuwa kichocheo cha madaliko ya kiuchumi ndani ya mkoa huo kwa kuongeza Shehena za mizigo za ndani na nje ya nchi kutoka tani milioni moja za sasa hadi tani milioni 15 kwa mwaka.
Hayo yalibainishwa na Waziri wa Uchukuzi Samuel Sitta wakati akizungumza na wafanyakazi wa Mamlaka ya usimamizi wa Bandari(TPA)mkoani Tanga kufuatia ziara yake ya kikazi ya kukagua Bandari hiyo na eneo linalotakiwa kujengwa Bandari mpya ya Mwambani.
Sitta alisema mradi huo wa Bandari mpya ya Mwambani unaenda sambamba na ujenzi wa miundo mbinu ya Barabara kutoka Pangani,Bagamoyo hadi Dar es Salaam pamoja na njia ya reli ya kutoka Tanga Arusha,Musoma mpaka Ziwa Victoria kuelekea Uganda.
Alisema tayari serikali imeshaliagiza Shirika la Rahco ili kuwa na kituo kikubwa cha kuegeuzia treni na mabehewa, na kwamba mchakato wa  ujenzi wa njia hiyo ya reli kwa Kiwango cha Kimataifa (Standard Gage)  yenye spidi 100 ambayo inabeba kontena zaidi ya mbili kwa mtindo wa ghorofa mradi  unatarajiwa kukamilika katika kipindi cha miaka mitano kuanzia sasa.
“Rais Museven wa Uganda alitoa rai kwa Rais Jakaya Kikwete kujenga reli itakayokwamua uchumi wa Uganda na ukitazama ramani ya Afrika hususan Afrika Mashariki Bandari ya Tanga ndiyo njia fupi karibu kabisa kwa kuweza kusafirisha bidhaa za Jamhuri ya Uganda”,alisema Waziri huyo.
Sitta alisema fursa hiyo inachangiwa pia na ugunduzi wa madini aina ya Red Nicol katika mkoa wa Simiyu eneo la Dutwa pamoja na Soda Arsh katika Ziwa Natron  rasilimali ambazo zote zinatafutwa Duniani na zitasafirishwa kwa njia ya reli kupitia Tanga kuelekea kwenye soko la Kimataifa.
Kwa mujibu wa Kiongozi huyo ni kwamba mradi huo wa njia ya reli unatarajiwa kugharimu zaidi ya dola Bilioni 4 sawa na shilingi za kitanzania takriban Trilioni 8 na unatarajiwa kufanyika chini ya Mkandarasi wa Kampuni ya China Engineering Company ambaye atajenga kwa gharama zake mwenyewe.
“Kwa hali hii nakuja kwenu watumishi wa Bandari ya Tanga msijiinamie inamie kufikiria hatma zenu hatma ya bandari Tanga ni nzuri sana na itabidi kuongeza na watumishi zaidi kwa sababu mtatoka kwenye kiwango cha chini ya tani milioni moja kwenda kwenye tani milioni 15 kwa kipindi cha miaka 10 ijayo”,alisisitiza.
Kufuatia hatua hiyo aliiagiza Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha inajiandaa na mikakati hiyo katika suala zima la upanuzi wa maeneo yake ili na kutumia fursa hiyo kwa mabadiliko ya kiuchumi na maendeleo ya wakazi wa mkoa huo kwa jumla.
Awali akizungumza katika kikao hicho Meneja wa TPA mkoa wa Tanga Henry Arika aliishukuru serikali kwa kufikia uamuzi wa kupitisha mafuta katika bandari hiyo na kwamba mpaka kufikia Julai 2 hadi 4 mwaka huu Meli yenye shehena ya mafuta takribani tani 20,500 inatarajiwa kutia nanga kwenye Bandari ya Tanga.
Arika alisema hatua hiyo itasaidia kuongeza mapato kwa Bandari na serikali kwa ujumla na kwamba mpaka sasa tayari mamlaka hiyo imeshapata vifaa vya kisasa ikiwemo baji 3 zenye ukubwa wa tani 3500 zenye uwezo wa kupakua makontena ya futi 20 zaid ya makontena 120 na hivyo kuongeza ufanisi wa Bandari.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa TPA Awadh Massawe alisema kuwa aliishukuru serikali kwa kufanya mabadiliko ya dhati yenye lengo la kuboresha huduma za mamlaka hiyo ikiwa ni pamoja na Bandari ya Tanga ambayo ni ya pili katika utoaji wa huduma na utendaji kazi bora nchini.
WA TATU KUTOKA KUSHOTO NI WAZIRI WA UCHUKUZI SAMWEL SITTA KULIA NI KAIMU MKURUGENZI WA MAMLAKA YA TPA NCHINI,AWAZI MASSAWE NA MKUU WA MKOA WA TANGA,SAIDI MAGALULA WAKIPATA MAELEKEZI.



Waziri wa Uchukuzi,Samwel Sitta akisisitiza jambo kwa Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA)Awazi Massawe wakwanza kulia wakati alipofanya ziara ya kutembelea bandari ya Tanga juzi katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga,Said Magalula


 




Share this

Related Posts

Previous
Next Post »