SERIKALI YATOA MANENO YAKE KUHUSIANA NA SUALA LA SIMBA NA SINGANO

June 13, 2015



Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, imewataka wachezaji wa Ligi Kuu Bara kuwa na wanasheria wao wa kusimamia wakati wa kusaini mikataba yao.


Kauli hiyo ya serikali imekuja baada ya kiungo mshambuliaji Ramadhan Singano ‘Messi’ kuwa katika mgogoro wa kisheria na Klabu ya Simba kuhusu mkataba wake na timu hiyo.

Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Juma Nkamia, ameliambia Championi Jumamosi kuwa, kupitia mgogoro huo ni vizuri wachezaji wakatumia wanasheria katika kutazama mikataba yao ili kuzuia migogoro inayoweza kujitokeza siku za mbele.

“Hili sakata la Messi na Simba nalisikia juu juu tu, lakini ukitazama vizuri utagundua mchezaji hakuwa na msimamizi wa maana katika kusaini mkataba ule, ndiyo maana sasa wanapingana.

“Hivyo kuanzia sasa wachezaji wanapaswa kuwa na wanasheria wao binafsi ili wawasimamie katika mambo ya mikataba kwani wengi wanasaini mikataba bila kujua kilichomo ndani yake,” alisema Nkamia ambaye amewahi kuwa katibu mwenezi wa Simba.

“Siyo jambo jema kwa mchezaji kukimbilia fedha tu bila kujali kilichomo katika mkataba na kusaini akiwa haelewi kilichoandikwa au kukisoma na kukubaliana nacho.”

Katika madai ya msingi, Messi anasisitiza mkataba wake unaisha Julai Mosi, mwaka huu wakati Simba wanasema mkataba huo unaisha Julai Mosi, mwakani, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limewataka wawili hao kuketi upya kuzungumzia mkataba mpya huku likivunja mikataba ya awali kwa kuwa ina dosari.


Messi amejitangaza kuwa mchezaji huru na Simba inasisitiza kuwa kiungo huyo bado ni mali yao na hapaswi kuzungumzia mkataba wake kwenye vyombo ya habari.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »