MAKAMU WA RAIS DKT. BILAL AKUTANA NA UONGOZI WA CHAMA CHA WAFUGAJI LEO.

June 02, 2015

lib1

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akizungumza na wajumbe wa Kamati ya uongozi wa Chama cha Wafugaji Tanzania, wakati walipomtembelea Ofisini kwake Ikulu Dar es salaam leo Juni 02,2015.
………………………………………………………………….
Na Mwandishi Maalum
Asema :Jitahidini kuepusha migogoro-Dkt. Bilal awaasa wafugaji .
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Mohammed Gharib Bilal amewataka wafugaji nchini kuhakikisha wanafuata sheria na kuachana na tabia ya kuchukua sheria mkononi ili kuhakikisha usalama wao na watu wanaopakana nao unakuwepo wakati wote. Mheshimiwa Makamu wa Rais amezungumza hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kupokea ujumbe kutoka Chama cha Wafugaji Tanzania ulioongozwa na Mwernyekiti wao Ally Hamis Lumiye.
 
Makamu wa Rais alisema, si busara kwa wafugaji kujichukulia sheria mkononi na kwamba matatizo yanayowakabili wafugaji ni muhimu yakatatuliwa kwa kufuata sheria za nchi. “Jitahidini kuepusha migogoro hasa ile inayosababisha watu kupoteza maisha. Tusichukue sheria mkononi, sote lazima tuwe watii wa sheria,” Makamu wa Rais alisema.
 
Awali akizungumza kwa niaba ya Baraza la Wazee wa Chama cha Wafugaji Tanzania, Mwenyekiti wa Chama hicho Ally Hamis Lumiye alisema, chama cha wafugaji kwa sasa kinakabiliwa na changamopto kubwa hasa baada ya kuwepo mgawanyiko unaolenga kukimomonyoa chama hicho hasa kufuatia kujitokeza baadhi ya wafugaji kuamua kupora madaraka ya chama hicho na hivyo akaitaka serikali kuungana nao katika kuzima nguvu za waporaji hao.
 
“Mheshimiwa Makamu wa Rais leo hii tumekuja kwako kwa jambo moja nyeti. Wapo baadhi yetu wasiotaka kuona wafugaji tunajikomboa kwa kuwa na umoja kama huu. Wamefikia hatua ya kupora chama hiki na jitihada zetu za kutaka kuwadhibiti zinaonekana kuwa ngumu kufuatia baadhi ya viongozi wa serikali kuwatambua waporaji hao,” alisema mwenyekiti huyo.
 
Mheshimiwa Makamu wa Rais alisisitiza kuwa jambo la uporaji wa chama kamwe haliwezi kuachwa kimya kwa kuwa wafugaji na chama chao kimesajiliwa hivyo wafuate sheria hizo hizo ili kupata haki yao kama inaonekana kutokuwepo. Pili alisisitiza kuwa atalifanyia kazi suala hilo kupitia nafasi ziliozpo chini yake na kulipatia ufuimbuzi wa haraka.
 
“Mimi nami ni mfugaji, chama hiki ni muhimu kwa maslahi ya wafugaji. Kwa kuwa tuna katiba inayokiongoza na kwamba tunazo sheria ambazo zilifuatwa hadi kukipatia chama hiki usajili, basi hakuna haja ya kusikitika sana. Tutumie taratibu hizi hizi ili kuondokana na hao wanaotaka kupora mamlaka ya chama hiki,” alisema na kuongeza:
 
“Ni muhimu kiwepo chama imara kwa maslahi ya wafugaji wote. Chama hiki kinaweza kuwasaidia sana katika kukabiliana na changamoto mlizonazo maana kwa kuwa wamoja ni nguvu.”

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »