DKT.BITEKO ATOA WITO VYOMBO VYA HABARI KUELIMISHA JAMII KUHUSU MASHUJAA

July 24, 2025 Add Comment

📌Rais Samia mgeni rasmi Maadhimisho ya Mashujaa kesho


📌Atoa wito kwa wananchi kushiriki Maadhimisho ya Mashujaa


Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ametoa wito kwa vyombo vya habari kushirikiana na Serikali katika kuelimisha jamii kuhusu historia ya mashujaa nchini.


Dkt. Biteko ametoa wito huo Julai 24, 2025 katika Uwanja na Mnara wa Mashujaa uliopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma mara baada ya kukagua maadalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa.

“ Ninatoa wito kwa wananchi wote kushiriki kwa wingi kwenye tukio hili adhimu. Hii ni siku yetu sote, siku ya kumkumbuka Mtanzania mwenzetu aliyesimama kwa ajili ya Taifa. Vivyo hivyo, nawaomba nyinyi waandishi wa habari, pamoja na vyombo vyenu na pia mitandao ya kijamii mshirikiane na Serikali katika kuelimisha jamii kuhusu historia ya mashujaa wetu, thamani ya mchango wao, na sababu ya sisi kuendelea kuwakumbuka kila mwaka,” amesema Dkt. Biteko.

Amezungumzia maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Mashujaa na kusema kuwa yanaendelea vizuri na mgeni rasmi katika tukio hilo anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, huku akisisitiza kuwa siku hiyo ni maalum kwa ajili ya kuwakumbuka, kuwaenzi na kuwaheshimu mashujaa wetu waliotoa maisha yao, nguvu zao, na sadaka zao kwa ajili ya uhuru, amani na maendeleo ya Taifa.



Amefafanua kuwa kwa heshima hiyo, saa 6:00 usiku wa tarehe 24 Julai, 2025 siku moja kabla ya kilele cha maadhimisho, Mwenge wa Kumbukumbu ya Mashujaa utawashwa rasmi na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule kwa niaba ya Rais kuashiria kuanza kwa maombolezo ya Mashujaa wetu. 



Ameongeza kuwa katika siku ya maadhimisho kesho tarehe 25 Julai, 2025 kuanzia saa 3:00 asubuhi kutakuwa na gwaride rasmi la heshima litakalofanywa na Vikosi vya Ulinzi na Usalama. Aidha, saa 6:00 usiku wa tarehe hiyohiyo mwenge wa Kumbukumbu ya Mashujaa utazimwa rasmi kuashiria hitimisho la maombolezo ya kumbukumbu Mashujaa kwa mwaka 2025.


Maadhimisho ya Kitaifa ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa hufanyika kila mwaka tarehe 25 Julai 2025 kwa lengo la kuwakumbuka mashujaa waliopoteza maisha yao katika uwanja wa vita, waliostaafu baada ya kulitumikia Taifa kwa uaminifu, na wale waliopata majeraha katika kuilinda nchi yetu.



Mwisho.

SERIKALI YAZINDUA NYARAKA ZA USIMAMIZI WA MAAFA WILAYA SUMBAWANGA

July 24, 2025 Add Comment


Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kushirikiana na UNDP, imezindua nyaraka tatu muhimu za usimamizi wa maafa katika Wilaya ya Sumbawanga, mkoani Rukwa.


✅ Nyaraka zilizozinduliwa:


Mpango wa Kujiandaa na kukabiliana na maafa ya Wilaya (D-EPRP)


Mkakati wa Kupunguza Vihatarishi vya Maafa (D-DRRS)


Ripoti ya Tathmini ya Vihatarishi, Uwezekano wa Kutokea na Uwezo wa kukbailian na maafa (RVCA)



📅 Uzinduzi umefanyika tarehe 23 Julai 2025 na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo na wananchi.

🎙️ Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Mhe. Nyakia Chirukile:


> "Hii ni hatua muhimu kujenga mfumo wa utayari dhidi ya majanga kama mafuriko."



🎙️ Brigedia Jenerali (Mstaafu) Hosea Ndagalla, Mkurugenzi wa Idara ya Maafa OWM:


> "Ni utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa Na. 6 ya 2022."



🎙️ UNDP Tanzania kupitia Bw. Godfrey Mulisa:


> "Mpango huu ni sehemu ya kusaidia jamii kujenga upya maisha yao na kuwa imara zaidi."

💬 Wadau wa maendeleo wametoa pongezi na kuahidi kushiriki kikamilifu kutekeleza mpango huu.



🟢 #Maafa2025 #Sumbawanga #UtayariDhidiYaMajanga #UNDP #OWM



VITUO VIWILI VYA KUPUNGUZA KASI YA MAFUTA GHAFI EACOP KUJENGWA NCHINI

July 24, 2025 Add Comment


*📌Vinalenga kupunguza kasi ya Mafuta kutoka Hoima Uganda hadi Chongoleani Tanzania*


*📌Ujenzi wafikia asilimia 50*


*📌 Mabomba ya kipenyo cha inchi 24 kutumika kusafirsha mafuta ghafi*


📌 *Wataalam wazawa waomba Serikali kuwa na data za kuwatambua pindi miradi inapotokea*


Na Neema Mbuja, Manyara


Jumla ya vituo viwili vya kupunguza kasi ya mafuta ghafi yanayotoka Hoima nchini  Uganda hadi Chongoleani- Tanga  vinatarajia kujengwa ili kusaidia upunguzaji wa kasi ya mafuta ghafi yanayosafirishwa sambamba na kulinda miundombinu ya bomba hilo la mafuta.


Hayo yamesemwa na Mtaalamu wa Ujenzi wa Miundombinu hiyo kutoka kituo namba moja (PRS-1) inayojengwa Kata ya Kibaya, Wilaya  ya Kiteto Mkoani Manyara. Mhandisi Damian Lasway, wakati alipokuwa akizungumzia maendeleo ya ujenzi wa miundombinu ya kituo hicho ambapo amesema ujenzi wa kituo  umefikia asilimia 50.

Amesema ujenzi wa vituo hivyo  utaenda sambamba na  wa nchini Uganda, ambapo kwa hapa nchini vituo hivyo viwili vitajengwa sambamba na vile vya kusukuma mafuta vitakavyojengwa  Muleba, Mbogwe, Igunga na Singida na vingine viwili vitakuwa nchini Uganda.



‘’ kazi hii ya ujenzi wa vituo hivi ni muhimu sana kwani mafuta yakiwa yanasafiri kutoka Uganda yanakuwa na kasi kubwa hivyo ni lazima kuwe na kituo cha kupunguza presha hiyo ya mafuta na baadae yaendelee kusafiri ‘’ ameisema Mha. Lasway

Amesema kituo cha kwanza kitajengwa mkoani Manyara, Kata ya Kibaya, Wilaya ya Kiteto na cha pili kitajengwa Kata ya Sindeni , Wilaya ya Handeni Mkoani Tanga .


Ameongeza kuwa,  Tanzania na Uganda zimefanya kazi kubwa kwenye utekelezaji wa mradi huo wa bomba la mafuta ghafi kwa kuhakikisha wazawa wananufaika na ujuzi kutoka kwa wataalamu mbalimbali wa kimataifa kutoka nchi tofauti.

Akizungmzia namna wanavyonufaika na ujuzi huo,  baadhi ya wazawa wanaofanyakazi kwenye eneo hilo akiwemo Rajab Rajab ambaye ni mhakiki ubora PRS-1 amesema kwa sasa uwezo wao umekua kwa kiasi kikubwa  tofauti na ilivyokuwa awali wakati wanaingia kwenye mradi

‘’Nina uhakika ukitokea mradi kama huu tena tutakuwa na uwezo mkubwa wa kutekeleza miradi jambo kubwa ni kwa Serikali kututambua na kuweka data za wataalamu ili zinapohitajika zipatikane kwa urahisi’’ Amesema Rajab

Naye Afisa Rasilimali Watu bi. Priscilla Baregu amesema licha ya wazawa kupewa kiqumbele kwenye utekelezaji wa mradi huu, tayari wameanza kuwatambua wafanyakazi wasio na ujuzi kwa kuwapeleka kwenye vyuo vinavyotambulika na kupatiwa mafunzo rasmi

‘’ Mpaka sasa tumeshawapeleka wafanyakazi takribani 4 kwenye mafunzo rasmi na tunawagharamia kila kitu ili kutoa motisha na kuwa na weledi mpindi mradi utakapomalizika’’ Amesema Bi. Priscilla




Mradi wa bomba la mafuta ghafi la Afrika Mashariki utatekelezwa kwa vipande 16 ambapo cha kwanza kinaanzia nchini Uganda kuelekea Chongoleani Tanga

JAB Yakabidhi Press Card kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Michuzi Media Group

July 24, 2025 Add Comment

 

●Waandishi Wengine Watakiwa Kuhakiki Viambatisho Katika Mfumo

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Patrick Kipangula, amemkabidhi rasmi Kitambulisho cha Uandishi wa Habari (Press Card) Mkurugenzi Mtendaji wa Michuzi Media Group, Muhidin Issa Michuzi, kwa niaba ya waandishi wengine wanaoendelea kukamilisha taratibu za kupata vitambulisho hivyo.

Hafla ya makabidhiano hayo imefanyika jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa jukumu la Bodi hiyo katika kuhakikisha kuwa waandishi wote nchini wanakuwa na vitambulisho halali kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari Na. 12 ya mwaka 2016.

Akizungumza baada ya kukabidhi kitambulisho hicho, Wakili Kipangula amempongeza Michuzi pamoja na waandishi wengine waliokwishapatiwa vitambulisho vyao kwa kufuata taratibu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa kisheria.

Amesisitiza kuwa mchakato wa utoaji wa vitambulisho bado unaendelea na ametoa wito kwa waandishi ambao maombi yao hayajakamilika kuingia katika mfumo rasmi wa Bodi ili kuhakiki viambatisho walivyowasilisha.

“Kuna baadhi ya waombaji ambao viambatisho vyao havifunguki, havisomeki, vimerudiwa au havikidhi matakwa ya kisheria kama vile vyeti visivyotambulika au kukosekana kwa barua za utambulisho kutoka kwa waajiri,” amesema Wakili Kipangula.

Ametoa rai kwa waandishi kuhakikisha wanafuata maelekezo yanayotolewa kupitia mfumo kabla ya kuwasiliana moja kwa moja na Bodi kuhusu hali ya maombi yao.
JAB imekuwa ikitekeleza jukumu la kuthibitisha na kusimamia maadili ya taaluma ya uandishi wa habari nchini, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanahabari wanatambulika rasmi na kuwa na vitambulisho halali vinavyotolewa kwa mujibu wa sheria.

Michuzi ameishukuru Bodi kwa mchakato huo na kuwataka waandishi wengine kuhakikisha wanazingatia taratibu ili kuimarisha tasnia ya habari kwa weledi na uwajibikaji.

WATENDAJI UCHAGUZI WATAKIWA KUFANYA VIKAO NA VYAMA VYA SIASA

July 24, 2025 Add Comment

 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jacobs Mwambegele akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku tatu kwa watendaji wa uchaguzi mkuu kutoka mikoa ya Shinyanga na Simiyu leo Julai 23, 2025. Mafunzo hayo yamefanyika mkoani Shinyanga kuanzia Julai 21 hadi 23 mwaka huu.  (Picha na INEC).
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jacobs Mwambegele akizungumza wakati akifunga mafunzo ya siku tatu kwa watendaji wa uchaguzi mkuu kutoka mikoa ya Shinyanga na Simiyu leo Julai 23, 2025. Mafunzo hayo yamefanyika mkoani Shinyanga kuanzia Julai 21 hadi 23 mwaka huu.  (Picha na INEC).
Mwenyekiti wa Mafunzo Ndg. Faustine Lagwen, akizungumza jambo. 

Washiriki wakifuatilia ufungaji wa mafunzo hayo. 

Washiriki kutoka mikoa ya Shinyanga na Simiyu wakifuatilia ufungaji wa mafunzo hayo.
Na. Mwandishi wetu.
Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imewaelekeza watendaji wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kufanya vikao na viongozi wa vyama vya siasa kujadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa uteuzi wa wagombea unafanyika kwa mujibu wa sheria.

Maelekezo hayo yametolewa na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani Jacobs Mwambegele wakati akifunga mafunzo kwa watendaji wa uchaguzi mkoani Shinyanga leo Julai 23, 2025.

Mtatakiwa kuyatafsiri mafunzo haya kwenye usimamizi wenu wa shughuli za kila siku za masuala ya uchaguzi kwa kuanza na vikao na vyama vya siasa, utoaji wa fomu za uteuzi na uteuzi wa wagombea wa nafasi za ubunge na kuhakikisha utoaji wa fomu za uteuzi na uteuzi wenyewe ngazi ya udiwani ufanyike kwa mujibu wa sheria,” amesema.

Amewaelekeza kuitisha na kuratibu kamati za upangaji wa ratiba za kampeni na kuitisha kamati za maadili iwapo kuna changamoto zitajitokeza wakati wa kampeni.

Jaji Mwambegele amewakumbusha watedaji hao kuhusu wajibu wao wa kutoa mafunzo kwa wasimamizi wa uchaguzi ngazi ya vituo na kuratibu na kusimamia vizuri na kwa weledi uchaguzi ngazi ya vituo.

Mafunzo mtakayowapa yatawawezesha kuratibu na kusimamia uchaguzi ngazi ya kata vizuri na kwa weledi. Hivyo, jukumu lenu ni kutoa mafunzo sahihi, kwa kuonesha kwa vitendo yote wanavyotakiwa kuyafanya wasimamizi wasaidizi ngazi ya Kata,” amesema.

Akifunga mafunzo kama hayo Kisiwani Pemba, Zanzibar, Makamu Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Jaji wa Rufani (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk amewakumbusha watendaji hao wajibu wao wa kubandika mabango, orodha ya majina ya wapiga kura na matangazo au taarifa zinazopaswa kuwafikia wapiga kura kwa kuwa ni takwa la kisheria na kanuni zinazosimamia uchaguzi.

“Ni wajibu wenu kuhakikisha mabango, matangazo, orodha ya majina ya wapiga kura na taarifa yoyote inayotakiwa kubandikwa kulingana na kalenda ya utekelezaji wa majukumu ya uchaguzi inabandikwa ili kuepusha malalamiko ya ukiukwaji wa masharti ya sheria na kanuni za uchaguzi,” amesema.

Amewasisitiza watendaji hao kutoa taarifa mbalimbali kwenye vyombo vya habari ili kuwajulisha wananchi na wadau mambo mbalimbali ya uchaguzi.

“Hakikisheni mnajiandaa kabla ya kukutana na vyombo vya habari. Pima taarifa yako unayotaka kuitoa kabla hujaitoa ili kuepuka kuleta taharuki badala ya utulivu katika eneo lako na Taifa kwa ujumla,” amesema.

Mafunzo hayo yamefanyika kwa siku tatu kwenye mikoa mbalimbali nchini na yanawajumuisha waratibu wa uchaguzi, wasimamizi wa uchaguzi na wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya jimbo.

Tume iliyagawa mafunzo hayo kwenye awamu mbili ambapo awamu hii ya pili ilihusisha mikoa ya Simiyu, Shinyanga, Kusini Pemba, Kaskazini Pemba, Mwanza, Mara, Dar es Salaam, Pwani, Rukwa, Katavi, Manyara, Arusha, Songwe na Mbeya.

Awamu ya kwanza ilifanyika tarehe 15 hadi 17 na ilihusisha watendaji kutoka mikoa ya Morogoro, Singida, Dodoma, Kaskazini Unguja, Kusini Unguja, Mjini Magharibi, Geita, Kagera, Mtwara, Lindi, Tabora, Kigoma, Tanga, Kilimanjaro, Ruvuma, Iringa na Njombe.
Mwisho.