Showing posts with label siasa. Show all posts
Showing posts with label siasa. Show all posts

DKT.SAMIA AMETENDA MAAJABU SEKTA YA NISHATI MIAKA MINNE YA UONGOZI -DKT.BITEKO

March 24, 2025 Add Comment


📌 Mashine ya 9 yakabidhiwa, yakamilisha MW 2115 - JNHPP


📌 Aitaka Jumuiya ya Wazazi ieleze Watanzania mafanikio ya Serikali


📌 Asema kuongezeka kwa mahitaji ya umeme nchini kunachochea ukuaji wa viwanda


📌 Atoa wito kwa Watanzania kuzingatia matumizi bora ya umeme


Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema katika kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan sekta ya nishati imepiga hatua kubwa nchini sambamba na kuzalisha umeme wa ziada dhidi ya mahitaji ya Watanzania.

Dkt. Biteko amesema hayo Machi 23, 2025 jijini Arusha wakati akitoa takwimu kuhusu  ongezeko la mahitaji  ya umeme nchini katika Kikao cha Baraza Kuu la Wazazi Taifa.


“ Rais Samia amefanya kazi kubwa katika sekta ya nishati nchini na hivi karibuni, tulikuwa nchini Barbados kueleza  mafanikio yetu katika sekta hii kwa kuwa Rais Samia amefanya jitihada kubwa sana katika ya nishati,” amesema Dkt. Biteko.

Ameongeza “Ili uchumi wa nchi yoyote duniani upatikane lazima kuwe na sekta ya nishati. Aidha, katika sekta ya nishati ili viwanda viweze kuendelea umeme unaohitajika ni asilimia 40 na katika sekta ya madini umeme unaohitajika ni asilimia 30,” 


Dkt. Biteko amesema mwaka 2017 hadi 2018 mahitaji ya juu ya umeme nchini yalikuwa megawati 1045, mwaka 2018 hadi 2019 mahitaji ya juu ya umeme yalikuwa megawati 1,116 mwaka 2021 hadi 2022 megawati 1,340.7.

“ Mwaka 2022 hadi 2023 mahitaji ya juu yaliyoongezeka na kufikia  megawati 1,470 na mwaka 2024 hadi kufikia sasa mwaka 2025 ni megawati 1,908 ikiwa ni sawa na megawati 262, ongezeko la mahitaji ya namna hii haliwezi kutokea kama hakuna uwekezaji katika sekta ya nishati,” amesema Dkt. Biteko.


Aidha, Dkt. Biteko amesema kuwa Mashine ya tisa ya mtambo wa kuzalisha umeme katika Bwawa la Julius Nyerere Machi 22, 2025 imekabidhiwa na kuunganishwa kwenye Grid ya Taifa. Amesisitiza kuwa kutokana na ongezeko hilo la megawati za umeme Bwawa la Kuzalisha Umeme la Julius Nyerere pekee linaweza kutosheleza mahitaji ya nchi licha ya kumalizika kwa muda uzalishaji wa umeme kwa kutumia mitambo ya Songas.

 “Katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan sekta ya nishati imefanya kazi kubwa, Rais Samia ametenda maajabu katika sekta hii na ameweza kuvutia wawekezaji wengi sana kuja kuwekeza nchini,” amesema Dkt. Biteko.

Aidha, amesema kuwa Jumuiya ya Wazazi nchini ina wajibu wa malezi na mazingira na kuwa nishati safi ni eneo mojawapo hivyo Wizara ya Nishati ina wajibu wa kushirikiana  na wadau mbalimbali ikiwemo Jumuiya hiyo, sambamba na kushirikiana nayo katika kampeni zake za kupeleka ujumbe kwa jamii.

Pamoja na hayo, Dkt. Biteko amewaasa Watanzania kuzingatia matumizi bora ya umeme kwa kuacha mazoea yanayosababisha upotevu wa umeme ikiwemo kuwashaa taa bila kuwa na matumizi nazo.


Ametolea mfano kuhusu matumizi mabaya ya umeme kupitia utafiti uliofanywa na Wakala wa Nishati wa Kimataifa (International Energy Agency) ambapo asilimia 30 ya umeme unapotea kutokana na mazoea.


Katika hatua nyingine, taasisi mbalimbali ikiwemo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) zimewasilisha mada mbalimbali katika semina hiyo.


Pia, Wizara ya Nishati kupitia taasisi zake za TPDC, REA na TANESCO zimetoa semina kwa wajumbe wa kikao hicho kuhusu Mkakati wa Taifa wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia 2024 hadi 2034, Matumizi Sahihi ya Nishati Safi ya Umeme.


Ambapo, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia, kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Ngeleja Mugejwa ameeleza faida mbalimbali za matumizi ya nishati safi ya kupikia hususan kwa watoto wa kike ambapo  kupitia matumizi ya nishati hiyo itawasaidia kupata muda mwingi wa kujisomea kuliko kuandaa na kupika chakula.

SHAMIRA AKABIDHI SHILINGI MILIONI 1 UJENZI WA NYUMBA YA KATIBU KASKAZINI UNGUJA

March 24, 2025 Add Comment

Mjumbe wa Baraza kuu UVCCM Viti vitatu Bara Ndg. Shamira Mshangama @shamiramshangama akiwa kwenye muendelezo wa ziara yake ya kuimarisha uhai wa Jumuiya ya Vijana CCM na kuhamasisha ushiriki wa vijana kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu 2025.

Shamira alitembelea ofisi ya UVCCM Mkoa wa Kaskazini Unguja, Zanzibar kufanya kikao kifupi cha ndani, na kukabidhi shilingi milioni moja kwa kamati ya Utekelezaji na viongozi wa Baraza la UVCCM Mkoa wa Kaskazini Unguja iliyopokelewa na Katibu wa UVCCM Mkoa huo Comrade Rished Khalfan pamoja na wajumbe wengine ngazi ya mkoa na Wilaya.


Shamira amewasisitiza kuwa pamoja na kazi zote tunazofanya lakini viongozi tunajukumu la kuzingatia ujenzi wa CCM na Jumuiya zake.

“Ujenzi wa Chama ni jukumu letu sote”.




DOYO HASSAN DOYO AMETANGAZA NIA YA KUGOMBEA URAIS WA TANZANIA KATIKA UCHAGUZI MKUU UJAO

March 15, 2025 Add Comment






Na Oscar Assenga,MOROGORO

Katibu Mkuu wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Doyo Hassan Doyo, ametangaza rasmi nia yake ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu ujao. Doyo alifanya tangazo hilo mbele ya waandishi wa habari jana mkoani Morogoro, na kusema kuwa kwa heshima kubwa anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjalia kuwa na afya njema.

Akizungumza kwa hisia, Doyo aliwashukuru Watanzania kwa mwitikio wao wa kuendelea kukuza demokrasia nchini, akisisitiza kuwa ni muhimu kwa kila Mtanzania mwenye sifa kupata haki ya kuchagua au kuchaguliwa. “Tanzania ni nchi ya kidemokrasia, ambapo kila Mtanzania mwenye sifa anayo haki ya kuchagua na kuchaguliwa,” alisema.



Doyo aliongeza kuwa, yeye mwenyewe ana sifa zote zinazohitajika kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akisisitiza kuwa amevuka umri wa miaka 45, umri wa kikatiba wa kugombea urais, na kwamba ana afya ya kuhimili majukumu makubwa ya urais.

Akizungumzia umuhimu wa uchaguzi mkuu ujao, Doyo alisisitiza kuwa huu utakuwa uchaguzi wa sita tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini, na kwamba ni muhimu kwa maendeleo ya taifa. “Kama Mtanzania mwenye haki ya kikatiba, nimemudu kujitathmini kifikra, kiuwezo, na kiuweledi, na kujiridhisha kuwa nina uwezo wa kumudu nafasi hii,” alisema Doyo.

Doyo alifafanua kuwa uamuzi wake wa kugombea urais haujaanza kwa mkupuo, bali ni baada ya kupata busara kutoka kwa wazee na familia yake, ambao walimshauri kuendelea mbele kwa faida ya taifa. “Si busara kuwataja hapa, lakini wanajua na wanasikia wakiwa pale walipo,” alieleza.

Doyo aligusia masuala muhimu ambayo bado hayajapata kipaumbele kikubwa katika taifa letu, na ambayo ataenda kuyashughulikia iwapo atachaguliwa kuwa Rais. Masuala hayo ni pamoja na: ajira, elimu, kilimo na ufugaji, rasilimali za maji, kupambana na ukwepaji wa kodi, na kupambana na rushwa. Aliongeza kuwa ataweka nguvu katika kuimarisha sekta ya madini, kuimarisha muungano, na kuendeleza jitihada za watoto wa kike katika elimu na teknolojia.

“Kwa hiyo, nimeona ni muhimu kutoa mchango wangu kwa taifa letu ili kuleta faraja kwa Watanzania. Hivyo, leo hapa mbele yenu, mimi Doyo Hassan Doyo, mwanachama wa Chama cha National League for Democracy (NLD), natangaza nia ya kugombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama chetu cha NLD. Dhamira yangu ni kubeba dhana ya Uzalendo, haki, na maendeleo kwa vitendo ili tuwakomboe Watanzania,” alisisitiza Doyo.

NLD: Ukombozi wa

NLD: Mtetezi wa Umma.

NLD: Moto Moto Motooo!



KUELEKEA SIKU YA WANAWAKE DUNIA MACHI 8 MBUNGE UMMY MBUNGE WA KWANZA MWANAMKE JIMBO LA TANGA

March 06, 2025 Add Comment


NA: MWANDISHI WETU, TANGA


Tarehe 08 Machi ya kila mwaka ni Siku ya Wanawake Duniani. Siku hii imebeba tafakuri ya kina juu ya mchango wa mwanamke katika kuchochea maendeleo ya nyanja zote; kijamii, kiuchumi na kisiasa. Pia, ni siku ya kujadili changamoto zinazowakabili wasichana na wanawake ili kuzitatua kama msingi wa kuharakisha maendeleo. Wanawake ni wadau muhimu wa maendeleo na bila ushiriki wao ipasavyo, juhudi hizo hazitazaa matunda yanayotarajiwa, ndiyo maana jamii inapaswa kuwashirikisha wasichana na wanawake kikamilifu.


Sambamba na hilo, wanawake wamekuwa wakihamasishwa kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kama Udiwani, Ubunge na hata Urais ili wapaze sauti zao wenyewe moja kwa moja badala ya kutegemea kusemewa na wanaume au kutegemea uwepo wa nafasi za viti maalum kwenye Udiwani na Ubunge. Ummy Mwalimu, Mbunge wa Tanga Mjini, ni mfano wa wabunge wanawake katika Bunge la Tanzania walioamua kugombea na kushinda ubunge mwaka 2020.

Ummy Mwalimu ambaye kitaaluma ni Mwanasheria, alianza kuwa Mbunge wa viti maalum mkoa wa Tanga  kwa vipindi viwili yaani mwaka 2010-2015 na baadaye 2015-2020. Mwaka 2020 aligombea rasmi Ubunge  kuwakilisha wananchi wa  Jimbo la Tanga Mjini ambapo aliibuka mshindi kwa kishindo kikubwa. Kwa hakika, Ummy Mwalimu ni kielelezo cha wanawake wenye uthubutu na kujiamini katika uongozi.


Kimsingi, Ummy Mwalimu amefanikiwa kuwa Mbunge wa mfano Bungeni kutoka na uchapakazi na uhodari wake wa kujenga hoja akiwasilisha vyema changamoto za wananchi wa Tanga Mjini ili viweze kufanyiwa kazi.  Hata Wizara mbalimbali alizohudumu kama Waziri, amekuwa kielelezo kizuri cha uchapakazi uliotukuka.


Kwa mfano, Ummy Mwalimu amewahi kuwa Waziri wa Afya kwa vipindi viwili (2015-2020 na 2022-2024). Vilevile, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) mwaka 2021. Pia, Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na  Watoto, Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira na Naibu Waziri Katiba na Sheria (2010-2015). Nafasi hizo zote amezitumikia kwa ufanisi na kuacha matokeo mazuri kote alipohudumu.


Sanjari na hilo, ni katika uongozi wake ambapo Jimbo la Tanga Mjini limepiga hatua kubwa za kimaendeleo hasa katika miradi mikubwa ya kimaendeleo na ya kimkakati. Mathalani,  uboreshaji wa huduma za afya, elimu, maji, umeme, barabara, bandari, masoko, kilimo cha mwani, utoaji wa mikopo kwa wanawake, vijana na wenye mahitaji maalum na huduma nyingine nyingi. Ummy Mwalimu amethibitisha uwezo mkubwa wa kiuongozi walionao wanawake katika kuwatumikia wananchi.  Huyu ndiye Ummy Mwalimu, kwa jina maarufu "Odo Ummy."

Ikumbukwe kuwa kilele cha Siku ya Wanawake Duniani ni Tarehe 08 Machi ya kila mwaka ambapo kwa mwaka huu 2025, maadhimisho hayo yatafanyika mkoani Arusha, yakichagizwa na kaulimbiu isemayo: Wanawake na Wasichana 2025: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji; huku Mgeni Rasmi akitarajiwa kuwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.