Showing posts with label Nishati. Show all posts
Showing posts with label Nishati. Show all posts

TANZANIA NA JAPAN KUFUNGUA MILANGO MIPYA YA UWEKEZAJI KATIKA SEKTA YA NISHATI

April 30, 2026 Add Comment


Ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika sekta ya nishati unaingia hatua mpya, huku juhudi zikielekezwa zaidi katika kuvutia uwekezaji wa sekta binafsi na teknolojia za kisasa za uzalishaji umeme.

Hatua hiyo imebainishwa jijini Dar es Salaam leo tarehe 30 Aprili,2026 wakati Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia,Dkt.  James Mataragio alipokutana na Mwakilishi Mkuu mpya wa Japan International Cooperation Agency, Dkt. Kuge Katsuya.

Katika kikao hicho Dkt. Mataragio ameweka wazi Mkakati wa Serikali kuifanya sekta ya nishati kuwa kivutio kikubwa cha mitaji ya kimataifa hususan kutoka Japan.

Amesema  kuwa pamoja na historia ndefu ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili, hatua inayofuata inapaswa kulenga uwekezaji mkubwa zaidi unaoweza kuongeza uzalishaji na upatikanaji wa nishati nchini.

“Huu ni wakati wa kuhamasisha kampuni binafsi na taasisi za kifedha kutoka Japan kuja kuwekeza moja kwa moja katika miradi ya nishati Tanzania,” amesisitiza.

Akizungumzia ushirikiano wa Tanzania na Japan Dkt. Mataragio amesema JICA imekuwa mdau wa muda mrefu katika sekta ya nishati nchini na wameshiriki katika miradi ya  Uandaaji wa Mpango kabambe wa Matumizi ya Gesi Asilia Nchini (Natural Gas Utilization Master Plan -NGUMP),  wametoa fursa za kuwajengea uwezo wataalamu katika Matumizi ya gesi asili pamoja na utekelezaji wa Miradi mbalimbali ya umeme.

Aidha Dkt. Mataragio amembushia ahadi ya muda mrefu ya Japan ya kuwezesha Mradi wa umeme wa megawati 300 mkoani Mtwara.

Kwa upande wake, Dkt. Kuge ameashiria mwelekeo mpya wa ushirikiano utakaojikita katika Mafunzo ya teknolojia ya nishati ya nyuklia, Uzalishaji wa umeme kupitia gesi asilia kwa ufanisi mkubwa zaidi na Kuunganisha Tanzania na wawekezaji binafsi kutoka Japan

Ahadi hiyo inaashiria uwezekano wa Tanzania kunufaika na teknolojia za kisasa zaidi za nishati kutoka Japan, moja ya nchi zinazoongoza duniani katika ubunifu wa nishati.

Mkutano huo umeonesha wazi kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Japan hauishii katika misaada, bali sasa unaelekea kwenye uwekezaji mkubwa na ubadilishanaji wa teknolojia  hatua inayoweza kubadilisha kabisa sekta ya nishati nchini

RAIS SAMIA ATAMBULIWA KUWA KINARA WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA AFRIKA

April 30, 2026 Add Comment




📌 Mawaziri wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika wapendekeza Rais Samia kutangazwa rasmi

Umoja wa Afrika umetambua juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuendeleza na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ndani na nje ya nchi, na kumpendekeza kutangazwa rasmi kuwa kinara wa Umoja wa Afrika wa ajenda hiyo.

Hatua hiyo imefikiwa katika Mkutano wa 5 wa Mawaziri wa Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika wanaoshughulikia Nishati na Uchukuzi uliofanyika jijini Johannesburg, Afrika Kusini, tarehe 30 Aprili 2026. Katika mkutano huo Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameongoza ujumbe wa Tanzania katika ngazi ya Mawaziri.

Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ametambuliwa na kupendekezwa kuwa kinara wa Afrika kutokana na mchango wake mkubwa katika kusukuma sera, mikakati na ushirikiano wa kimataifa unaolenga kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia, kupunguza athari za kiafya na kimazingira, pamoja na kuboresha maisha ya waafrika, hususan wanawake na watoto.

Akizungumza katika mjadala kuhusu Programu ya Nishati Safi ya Kupikia Afrika, Waziri Ndejembi amesema kuwa mafanikio ya Tanzania katika sekta hiyo yametokana na uongozi madhubuti wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kusukuma ajenda ya nishati safi ya kupikia ndani na nje ya nchi.

Amesema kuwa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, nishati safi ya kupikia imepewa kipaumbele cha kitaifa na kuingizwa katika Dira ya Taifa ya 2050, ikiwa ni sehemu muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Katika juhudi za kimataifa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kuhamasisha agenda ya nishati safi ya kupikia kupewa kipaumbele katika mipango ya mataifa mbalimbali kupitia majukwaa ya kimataifa ikiwemo mkutano wa COP28 mwaka 2023, pamoja na Mkutano wa Nishati Safi ya Kupikia Barani Afrika uliofanyika Paris mwaka 2024, ambapo zaidi ya dola za Marekani bilioni 2.2 ziliahidiwa kusaidia sekta hiyo.

Kutokana na hatua hiyo ya mapendekezo ya Mawaziri yaliyoanzia katika ngazi ya wataalamu wa Umoja wa Afrika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuthibitishwa na kutangazwa rasmi kuwa Kinara wa Umoja wa Afrika wa Nishati Safi ya Kupikia katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika utakaofanyika.




MHE. SALOME ASHIRIKI MKUTANO WA 21 WA MAWAZIRI WA NISHATI AFRIKA MASHARIKI

MHE. SALOME ASHIRIKI MKUTANO WA 21 WA MAWAZIRI WA NISHATI AFRIKA MASHARIKI

April 30, 2026 Add Comment

 





Na Mwandishi Wetu, Cairo

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ameiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa 21 wa Baraza la Mawaziri wa Nishati wa Ukanda wa Mashariki mwa Afrika, uliofanyika Aprili 29, 2026 jijini Cairo, Misri, ukiwa na lengo la kuimarisha ushirikiano wa kikanda katika sekta ya umeme.

Katika mkutano huo wa nchi wanachama wa Umoja wa Nishati Mashariki mwa Afrika (EAPP), uamuzi muhimu umefikiwa wa kuichagua rasmi Jamhuri ya Kiarabu ya Misri kuwa mwenyeji wa kudumu wa kituo cha uendeshaji wa soko la umeme la pamoja kwa nchi wanachama.

Mkutano huo uliongozwa na Waziri wa Umeme na Nishati Jadidifu wa Misri, Mhe. Dkt. Mahmoud Esmat, ambaye pia ni mwenyekiti anayemaliza muda wake, uliwakutanisha Mawaziri wa Nishati kutoka nchi 13 wanachama kwa lengo la kukamilisha mfumo wa kiutawala na kiuendeshaji wa soko la umeme la pamoja na endelevu.

Mbali na kuichagua Misri, Baraza hilo pia limepitisha nyongeza ya muda wa miezi miwili kwa nchi wanachama kukamilisha mchakato wa kuridhia hati za makubaliano ya ushirikiano baina ya serikali na mashirika ya umeme.

Aidha, mkutano huo umeridhia Jamhuri ya Shirikisho la Kidemokrasi ya Ethiopia kuchukua nafasi ya uenyekiti wa Baraza la Mawaziri, kufuatia kumalizika kwa muda wa uongozi wa sasa, kwa mujibu wa katiba ya umoja huo inayotaka uongozi kuzunguka kwa wanachama kila mwaka.

Akihitimisha mkutano huo, Mwenyekiti wa EAPP, Mhe. Dkt. Esmat, amesisitiza umuhimu wa kuendeleza umoja, ushirikiano, uwazi na kuheshimiana miongoni mwa nchi wanachama ili kufikia malengo ya kuwa na soko la umeme la kikanda lenye tija.

Akizungumza kuhusu mkutano, Mhe. Salome amesema maazimio yaliyofikiwa ni hatua muhimu katika kuleta mageuzi makubwa katika biashara ya umeme na kuimarisha soko la nishati la pamoja kwa nchi za ukanda huo.

Katika mkutano huo, Mhe. Makamba ameambatana na Balozi wa Tanzania nchini Misri, Meja Jenerali Richard Makanzo, Kamishna Msaidizi wa Maendeleo ya Umeme kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO anayeshughulikia uzalishaji umeme, Mhandisi Anthony Mbushi, pamoja na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati, TANESCO na EWURA.
Shar

DC MKUDE AKABIDHI VYOMBO VYA USAFIRI TANESCO MKOA WA ARUSHA KUIMARISHA UTOAJI HUDUMA

DC MKUDE AKABIDHI VYOMBO VYA USAFIRI TANESCO MKOA WA ARUSHA KUIMARISHA UTOAJI HUDUMA

April 14, 2026 Add Comment






*Ni katika muendelezo wa mkakati wa TANESCO wa kuwahudumia wananchi kwa ufanisi zaidi.

*Awataka kutumia vyombo hivyo kwa kazi husika za TANESCO.

Na Mwandishi Wetu, Arusha

Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mkoani Arusha Mhe. Joseph Mkude amekabidhi vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO Mkoa wa Arusha ili kuimarisha utoaji wa huduma mbalimbali za Shirika kwa wananchi.

Akizungumza tarehe 13, Aprili 2026 wakati wa hafla ya kukakabidhi vitendea kazi hivyo iliyofanyika katika Ofisi za TANESCO Mkoa wa Arusha amesema hatua hiyo ya kukabidhi vitendea kazi hivyo ni hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za umeme wa uhakika bila vikwazo vyoyote.

Amesema vitendea kazi hivyo vinakwenda kuongeza ufanisi katika utendaji kazi kwa watumishi wa TANESCO katika wilaya za Mkoa wa Arusha na kuwawezesha kutatua changamoto za wateja kwa wakati kwani Magari pamoja na Bajaji zitawawezesha kuyafikia maeno mengi zaidi ili kufikisha huduma ya umeme.

Amewataka Watumishi wa TANESCO Mkoa wa Arusha kuhakikisha wanatumia vyema vitendea kazi hivyo kwa malengo yaliyokusudiwa na Shirika na wala sio kwa matumizi yao binafisi ambayo hayana faida wala mchango wowote kwa Shirika hasa katika kutoa huduma kwa wananchi.

“Haya Magari tuliyopatiwa katika Mkoa wetu yanakwenda kugawiwa katika kila wilaya naomba yakatumike ipasavyo kwa malengo yaliyokusudiwa, tusitumie Magari haya kwa mambo yetu binafsi yasiyo na tija katika kutoa huduma kwa wananchi”.

Kwa upande wake Meneja wa Huduma za Usalama TANESCO Bw. Lenin Kiobya amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan iliwezesha kununuliwa kwa Magari Makubwa na Madogo zaidi ya 500 kwa mwaka wa fedha 2025/2026 ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Bw. Kiobya amesema kati ya Magari hayo zaidi ya 500, Malori ya ukubwa mbalimbali ikiwemo tani 10 na tani 7 yapo 215 ambayo yanakwenda kuwa msaada Mkubwa zaidi katika huduma za matengenezo ya umeme kwa wakati hali itakayochangia kuongeza ufanisi wa kazi ndani ya Shirika.

Aidha, amesema kwa Mwaka wa Fedha ujao 2026/2027 Serikali imetenga zaidi ya bilioni 200 ili kununua vitendea kazi hivyo lengo likiwa ni kumaliza kabisa upungufu wa vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO katika maeneo yote nchini.

“Serikali iliwezesha TANESCO kuweza kunua Magari 556 kwa mwaka huu wa fedha 2025/2026 ili kurahisisha utoaji wa huduma ya umeme kwa wananchi, na kwa mwaka ujao wa fedha 2026/ 2027 Serikali imetenga zaidi ya bilioni 200 ili kununua vitendea kazi hivyo lengo likiwa ni kumaliza kabisa upungufu wa vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO”

Meneja wa TANESCO Mkoa wa Arusha Mhandisi Kisika Kisika amesema TANESCO katika Mkoa huo wamepokea vitendea kazi mbalimbali ikiwemo Magari makubwa 2, Gari aina ya Landcruser (4), Bajaji moja (1) vitakavyokwenda kuboresha zaidi huduma kwa wateja katika Mkoa huo.

“Tunaishukuru Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa kutupatia vitendea kazi hivi ambavyo kwa sasa tunakwenda kuvitumia kufikisha huduma kwa wananchi kwa haraka zaidi.

WATENGENEZA MAUDHUI MTANDAONI WATAKIWA KUWA NGUVU YA KUBADILISHA JAMII KATIKA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

April 08, 2026 Add Comment




📌 Kupitia uelimishaji na uhamasishaji wa jamii


Katika mwendelezo wa mafunzo kwa watengeneza maudhui mtandaoni (Content Creators), awamu ya kwanza inayoendelea Jijini Arusha leo Aprili 8, 2026, Wizara ya Nishati imewahimiza washiriki kutumia majukwaa yao ya kidijitali kama chachu ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii.


Akitoa wito huo, Mhandisi Benezeth Kabunduguru kutoka Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia amesema watengeneza maudhui wana nafasi kubwa ya kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia, pamoja na kuhamasisha jamii wanayoizunguka na wafuasi wao kubadili mitazamo na kuanza kutumia nishati hizo.

Akiwasilisha mada yake, Mhandisi Kabunduguru ameeleza kuwa watengeneza maudhui wanaweza kutumia mbinu mbalimbali zenye mvuto kama vile picha za video fupi, vichekesho, hadithi na simulizi za maisha halisi ili kufikisha ujumbe kwa ufanisi na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia.

Aidha, amesisitiza kuwa nishati safi ya kupikia si aina moja tu, bali ipo katika mfumo mbalimbali ikiwemo gesi, umeme, mkaa mbadala na nyinginezo, ambazo zimeidhinishwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuwa salama kwa afya ya binadamu na rafiki kwa mazingira.

Katika hatua nyingine, alibainisha kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kinara wa ajenda ya nishati safi ya kupikia barani Afrika. Hivyo amewataka watengeneza maudhui kumuunga mkono kwa vitendo ili kufanikisha lengo la kitaifa la kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Ameongeza kuwa watengeneza maudhui wanapaswa kutumia ushawishi wao kubadilisha mitazamo hasi ya jamii kwa kutumia lugha sahihi, ubunifu na maudhui yenye kugusa maisha ya watu.

Kwa mujibu wa takwimu, takribani vifo 33,000 hutokea kila mwaka kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia. Hivyo, kuna umuhimu mkubwa wa kuifikisha elimu hii kwa wananchi wengi zaidi kupitia majukwaa ya kidijitali yanayotumiwa na watengeneza maudhui.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na Mfuko wa Utamaduni na Sanaa Tanzania, huku Wizara ya Nishati ikiwa miongoni mwa wadhamini wakuu.