*📌Asema baada ya Vijiji vyote Meatu kupata umeme kasi inaelekea vitongojini*
📌 *Ataka umeme utumike kuongeza thamani ya mazao, kilimo na ufugaji*.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassani amesema Serikali imeendelea kupeleka maendeleo katika Wilaya ya Meatu ikiwemo ukamilishaji wa usambazaji umeme katika Vijiji vyote 109 vya Wilaya hiyo.
Dkt. Samia ameyasema hayo Juni 17, 2025 Wilayani Meatu Mkoa wa Simiyu akiwa kwenye ziara ya kikazi.
"Kama tulivyoahidi, hatujaishia hapo, kazi ya usambazaji umeme sasa inaendelea kwenye vitongoji lakini pamoja na jitihada hizi zote ninafahamu kuna changamoto ya umeme kutokuwa na nguvu ambayo inatatuliwa." Amesema Dkt. Samia
Ameeleza kuwa, Wizara ya Nishati inatatua changamoto hiyo ya umeme kutokuwa na nguvu kwa kujenga njia ya kusafirisha umeme kutoka Shinyanga hadi Simiyu na ujenzi wa kituo cha kupokea na kupoza umeme.
Amesema kukamilika kwa miradi hiyo kutapelekea uwepo wa umeme wenye nguvu na wa kutosha kwa ajili ya shughuli mbalimbali za uzalishaji ikiwemo Viwanda.
Amesisitiza kuwa, lengo la Serikali ni kuona wananchi wanatumia nishati ya umeme kwa shughuli mbalimbali ikiwemo kuongeza thamani ya mazao, kilimo na ufugaji.
EmoticonEmoticon