WATU WANAOISHI NA MAAMBUKIZI YA VIRUSI VYA UKIMWI MKOANI TANGA WATAKIWA KUACHA KWENDA KWA WAGANGA WA KIENYEJI

December 21, 2017
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga,Dkt Asha Mahita
akizungumza wakati akifungua semina ya kuwajengea uwezo WAVIU washauri   ili waweze kuwaunganisha wateja kutoka kwenye Jamii kwenda kwenye vituo vya Afya iliyoratibuwa na Shirika la  Ariel Glaser Pediatric AIDS Health Care Initiative (AGPAHI) mkoani Tanga juzi kushoto ni Kaimu Mratibu wa Ukimwi mkoa wa Tanga,Anita Temu na kulia ni Afisa
Mradi wa Huduma Unganishi wa Shirika hilo,Madina Paulo
Watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (VVU) mkoani Tanga wametakiwa kuachana na kasumba za kukimbia kwa waganga wa kienyeji na  kuendelea na utaratibu walipangiwa na wahudumu wa afya wa kutumia dawa  kwani hali hiyo inaweza kuwasababishia matatizo makubwa.
Hayo yalisemwa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt Asha Mahita wakati akifungua warsha ya kuwajengea uwezo Waviu washauri ili waweze kuunganisha jamii kwenda katika vituo vya afya. Warsha hiyo inaratibiwa na Shirika la AGPAHI mkoani hapa.
Alisema vitendo vya wagonjwa kuacha dawa vinaweza kuwaweka kwenye wakati mgumu ikiwemo kupata usugu ambao unaweza kupelekea kupoteza maisha kutokana na kushindwa kufuata utaratibu uliowekwa na kuwataka kuondokana na tabia za namna hiyo.
“Kuna tabia ambayo imejengeka baadhi ya wagonjwa kuacha kutumia dawa na kukimbilia kwa waganga wa kienyeji kwani wanapoacha kutumia dozi na kutumia dawa nyingine.. virusi vinakuwa na usugu hali inayowasababishia hali mbaya zaidi na hata uwezekano wa kupoteza maisha “Alisema.
“Mpaka watu watambue kuwa hakuna dawa iliyothibitishwa kutibu VVU hivyo waendelea kuzitumia dawa za kupunguza makali ya VUU (ARV) ikiwemo kuacha kwenda kwa waganga wa kinyeji kwani wanaweza kukumbana na matatizo makubwa sana “Alisema.
Aidha alisema pia katika mpango wa mkoa wa Tanga wataendelea kuhamasisha wananchi kwenda kwenye vituo vya afya ili waweze kujua afya zao ikiwemo kuweza kuchukua hatua iwapo watabainika wameathirika.
“Lakini pia kwa watoto maana upimaji wao upo chini ikiwemo kuhakikisha watoto wanaopata maambuzi wanaanzishiwa dawa mapema kwani zitawasaidia kuongeza maisha yao na kuishi na afya njema”Alisema. 
Awali akizungumza katika semina hiyo,Afisa Mradi Huduma Unganishi wa Jamii wa Shirika la AGPAHI mkoani Geita Richard Kambarangwe alisema warsha hiyo ni kuwapa elimu zaidi Waviu washauri wanaosaidia kutoa huduma katika vituo vya tiba na matunzo (CTC) kwa watu wanaoishi na VVU.
Alisema pia kuweza kuwasaidia kupata ujuzi zaidi ili kujifunza mbinu za kuwatafuta na kuwaunganisha wateja wa CTC na vituo kwa jamii kuweza kupunguza idadi ya kupotea kwa wateja.
“Lakini pia takwimu za Tanzania na mkoa inaonyesha watu wengi wanaotumia dawa za kupunguza makali ya VVU wanaweza kupotea kwenye huduma hivyo shirika la AGPAHI mara kwa mara linazingatia kutoa elimu  itakayowasaidia watu kupata uelewa wa lishe na matumizi sahihi ya dawa “Alisema.
Kaimu Mratibu wa Ukimwi Mkoa wa Tanga,Anita Temu akizungumza wakati wa semina hiyo kulia ni Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga,Dkt Asha Mahita na kulia ni  Afisa Mradi wa Huduma Unganishi wa shirika la AGPAHI,Madina Paulo

Mganga M kuu wa Mkoa wa Tanga,Dkt Asha Mahita katika akiteta jambo na Mratibu wa Ukimwi wa Jiji la Tanga,Moses Kisibo mara baada ya kufungua semina hiyo
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga,Dkt Asha Mahita akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa semina hiyo mara baada ya kuifungua



Share this

Related Posts

Previous
Next Post »