DC Mgaza awaasa vijana kupenda Michezo.

June 09, 2013

Na Oscar Assenga, Mkinga.
MKUU wa wilaya ya Mkinga, Mboni Mgaza amewataka vijana kupenda michezo na kuithamini kwa kuwa michezo ni ajira ambayo inaweza kuwainua kimaisha endapo wataizingatia na kucheza kwa umakini.

Mgaza alitoa wito huo jana wakati akifungua Mashindano ya Umoja wa Shule za Msingi wilayani humo (Umitashumta) ambapo alisema michezo pia huongeza upendo ushirikiano baina ya wachezaji wanaokuwa wakishiriki ikiwemo kujenga undugu miongoni mwao.

Amesema michezo pia inadumisha amani kwa kuwa watu wanaposhiriki katika michezo wanakuwa ndugu na kufikiria jinsi ya kupata mafanikio hivyo kupelekea kudumisha amani tulionayo.

Aidha amewataka washiriki kucheza vizuri ili kuweza kutengeneza timu nzuri ya wilaya ambayo itaanza kambi kwa ajili ya kuwakilisha wilaya hiyo katika mashindano hayo ngazi ya mkoa.

Awali akizungumza wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo, Afisa Elimu wilaya ya Mkinga Idara ya Elimu Msingi, Juma Mhina amesema mashindano hayo yanashirikisha timu kutoka tarafa mbili ambazo ni Mkinga na Maramba na inashirikisha idadi ya wanamichezo 190.

Mhina amesema michezo itakayochezwa ni Pete,Wavu, Mpira wa Miguu na Mpira wa mikono na kueleza kuwa lengo la serikali kurudisha michezo mashuleni ni kuibua vipaji vya wachezaji kuanzia mashuleni.

                        Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »