BENKI YA CRDB YANG'ARA KATIKA TUZO ZA AFRICAN BANKER 2025,YATWAA TUZO YA BENKI BORA KWA WAJASIRIAMALI

June 05, 2025 Add Comment

 


Dar es Salaam, 05 Juni 2025 – Benki ya CRDB imeandika ukurasa mpya wa mafanikio baada ya kutangazwa mshindi wa tuzo ya Benki Bora kwa Wajasiriamali Wadogo na wa Kati (SME) katika hafla ya tuzo za sekta ya benki barani Afrika ‘African Banker Awards 2025,’ iliyofanyika sambamba na Mkutano Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) jijini Abidjan, Côte d’Ivoire.

Kaulimbiu ya mwaka huu wa tuzo hizo ilikuwa “Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo Endelevu,” ikiakisi umuhimu wa sekta ya fedha katika kuchochea ukuaji wa kijani, ujumuishi wa kijinsia na uhimilivu wa kiuchumi barani Afrika.

Katika mwaka huu ambapo Benki ya CRDB inaadhimisha miaka 30 ya huduma ubunifu, ilipata heshima ya kutajwa katika vipengele vinne vikuu, vikiwemo: Benki Bora kwa Wajasiriamali (Mshindi), Banker of the Year – kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Benki, Abdulmajid Mussa Nsekela, Benki Bora kwa maendeleo endelevu, Benki Bora ya mwaka (AFAWA).

Tuzo hiyo ya Benki Bora kwa Wajasiriamali ilipokelewa na Afisa Mkuu wa Biashara, Boma Raballa, ambaye alieleza kuwa ushindi huo ni kielelezo cha dhamira ya Benki hiyo ya kuwapatia wateja na watanzania kwa ujumla wake huduma bunifu za fedha. Katika miaka 30 tokea kuanzishwa kwake, benki hiyo imeendelea kuwa nguzo ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa wajasiriamali, hususan vijana na wanawake. “Ushindi huu si wetu pekee, bali ni wa jamii nzima tunayoihudumia,” ameeleza Raballa.

Benki ya CRDB imejidhihirisha kuwa mshirika mkubwa wa wajasiriamali nchini ikitoa uwezeshaji wa hadi shilingi bilioni 5. Hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2024 mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 1.2 imetolewa kwa zaidi ya wajasiriamali 230,000 kutoka sekta mbalimbali.

Benki ya CRDB imekuwa kinara katika huduma bunifu kwa wajasiriamali nchini, ikiwa Benki ya kwanza kuanzisha kitengo maalum kwa ajili ya kuhudumia kundi hili la wateja mwaka 2000.

Mwaka 2024, Benki ya CRDB ilifanya maboresho makubwa ya akaunti ya wajasiriamali ‘Biashara Akaunti’, ikiboresha pia fursa za uwezeshaji kupitia mikopo, pamoja na kutoa suluhisho za kidijitali kwa ajili ya kuongeza ufanisi wa upokeaji malipo kwa wateja kupitia huduma za ‘LIPA HAPA’ na mashine za manunuzi (PoS).

Aidha, Benki hiyo pia inazo bidhaa mahususi kwa ajili ya kusaidia wafanyabiashra wanaogaiza bidhaa nje ya nchi kama ‘Mkopo wa Komboa,’ ukisaidia wateja kutoa mizigo yao bandarini kwa wakati. Hatua ambayo imeondoa ucheleweshaji katika uzalishaji na usambazaji wa bidhaa sokoni.

Sambamba na huduma, Benki pia inatoa huduma za ufadhili wa biashara (trade finance) na ufadhili wa rasilimali (asset financing), ambazo zimekuwa msaada mkubwa kwa wateja katika kukuza na kuimarisha biashara zao.

Benki ya CRDB pia imekuwa ikiwapatia wajasiriamali uzoefu wa biashara kimataifa kwa kuwapeleka nchi mbalimbali duniani ili kuwapa fursa za kujifunza na kuongeza thamani kwenye biashara wanazozifanya, huku ikiwajengea uwezo wa kushindana katika masoko ya kimataifa. Hii ni hatua muhimu katika kukuza ushindani wa bidhaa na huduma za Kitanzania.

Aidha Benki ya CRDB imekuwa ikishirikiana kimakakati na tasisi za kimataifa zinazolenga kuwasaidia wajasiriamali kama vile AGF, PROPARCO, DFC, GuarantCo na GCF pamoja na taasisi za hapa nchini kama vile PASS na TADB. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Benki hiyo imeweza kukusanya zaidi ya Dola za Marekani Milioni 700, ikionyesha imani ya washirika wa kimataifa katika uwezo na utayari wa benki katika kuwawezesha wajasiriamali nchini.

“Katika miaka 30 ya uwepo wetu, tumejifunza kuwa hakuna maendeleo ya kweli bila kuwainua wajasiriamali. Tunaendelea kujipanga kufikia wengi zaidi kupitia mikakati madhubuti ya ujumuishi, hasa kwa wanawake na vijana, kama sehemu ya kusaidia ajenda ya serikali ya maendeleo jumuishi,” aliongeza Raballa.
Tuzo hii ni ushahidi mwingine wa jinsi Benki ya CRDB imejikita kwa dhati katika kuwa daraja la mafanikio kwa maelfu ya wajasiriamali nchini. Kuelekea mbele, Benki hiyo imeendelea kuonyesha utayari wake katika kuwahudumia wajasiriamali kwa kutoa kipaumbele kikubwa kwa kundi hilo la wateja katika Mkakati wake wa Muda wa Kati wa Biashara wa 2023 – 2027.

UDSM yawaita Wadau wa Elimu kushiriki maadhimisho Wiki ya Utafiti na Ubunifu

June 05, 2025 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam.

CHUO  Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeutaarifu umma wa Watanzania na kuwaalika wadau wa elimu na maendeleo, kwa ujumla kushiriki katika Maadhimisho ya kumi ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya UDSM yatakayofanyika kuanzia Juni 9- 11, 2025 katika Viwanja ya Maktaba ya Chuo.

Akizungumza na Waandishi  wa Habari Kaimu Naibu Makamu Mkuu wa Chuo-Utafiti, Prof. Nelson Boniface (Pichani) amesema kuwa Maonesho hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 11, 2025 na mazungumzo ya mashirikiano ya kimkakati, kongamano, maonesho na mawasilisho ya watafiti na wabunifu likiwa ni jukwaa la washiriki kupata fursa ya kubadilishana maarifa na ushirikiano.

Aidha, Prof.  Boniface amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni: "Kutumia teknolojia ya Dijitali ili kukuza utafiti, ubunifu na ubiasharishaji,".

Ameongeza kuwa miradi mingi itakayooneshwa ni ile ya wanafunzi na Wanataaluma huku akitanabaisha kuwa mtoa Mada Mkuu ni Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), Mhandisi Peter Ulanga na Profesa Lilian Kaale Mkurugenzi katika masuala ya Ubunifu UDSM.

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinatumia fursa hiyo kujipambanua kwa jamii kwa kuonesha shughuli zake za utafiti, ubunifu, huduma kwa umma na ubadilishanaji maarifa kwa kuunga mkono Dira ya  Taifa ya  Maendeleo 2050.



Ukerewe yawashukuru wafanyakazi Benki ya CRDB ukarabati madarasa mawili, madawati 200

June 04, 2025 Add Comment

 


Mkuu wa Wiliya ya Ukerewe, Mheshimiwa Christopher Emily Ngubiagai amewashukuru wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwa kukarabati madarasa mawili na madawati 200 kwa ajili ya Shule ya Msingi Hamkoko.

Akipokea msaada huo kutoka kwa Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Benki ya CRDB, Godfrey Rutasingwa, mkuu huyo wa wilaya amesea mazingira mabovu ya madarasa yanasababisha utoro kwa watoto wengi jambo ambalo seriklai inashirikiana na wadau kulifanyia kazi ili watoto wote wasome kwa utulivu unaohitajika kufanikisha ndoto zao.

“Hakika leo wafanyakazi wa Benki ya CRDB mmetupa somo kwa kujitoa kwenu kuhakikisha mnaigusa jamii jamii yetu ya wana Ukerewe. Hakika huu ni upendo mkubwa sana kutoka kwa wafanyakazi ambao sio tu inatugusa jamii ya hapa Ukerewe bali Tanzania nzima kwa ujumla. Mmeonyesha kujali na alama hii ya upendo haitosahaulika. Asanteni sana kwa heshima hii kubwa mliyotupa,” amesema Mheshimiwa Ngubiagai.

Amesisitiza kuwa shule zikiwa na miundombinu mizuri huwafanya watoto wapende kusoma kutokana na kuvutiwa na mazingira mazuri na madarasa ya kisasa, madawati bora ya kukalia. Kwa kulitambua hilo, amesema serikali inafanya kila liwezekanalo kuhakikisha inajenga shule mpya popote inapohitajika nchini na kukarabati miundombinu ya hsule za miaka mingi.

Akizungumza na wazazi, walimu na wanafunzi waliokuwepo kwenye hafla ya kukabidhi madarasa na madawati hayo, Mheshimiwa Ngubiagai amesema ni muhimu kwa jamii kujitoa kuchangia kuboresha mazingira ya shule kwa ajili ya watoto wa Kitanzania kujifunza kwa umakini na akaitumia nafasi hiyo kuwapongeza wafanyakazi wa Benki ya CRDB kwa kuonyesha mfano katika kujitoa kwa jamii wanaoyoihudumia na inayowazunguka.

“Hii imekuwa bahati kwetu kwani mngeweza kwenda sehemu nyingine lakini mliona inafaa kuja Ukerewe kusaidia kutatua changamoto za madarasa na kutoa madawati haya 200. Kwa kweli mmetufundisha na kutupa deni kubwa mioyoni mwetu kwani Watanzania wengi huwa wepesi kuchangia harusi na sherehe nyingine ila wazito kujitoa kwenye elimu kama mlivyofanya wafanyakazi wa Benki ya CRDB,” amesema.

Kwa upande wake, Rutasingwa amesema msaada huo umetolewa kupitia Programu ya Employee Volunteering iliyoanzishwa mwaka 2020 ambapo wafanyakazi wa Benki ya CRDB huchanga fedha kutoka kwenye mishahara yao na kuielekeza kutatua kero iliyopo kwenye jamii katika sekta ya elimu, afya, mazingira na watu waishio katika mazingira magumu.

“Moyo huu wa kujitoa kwa wafanyakazi wetu ni mwendelezo wa jitihada zinazofanywa na Benki ya CRDB kurudisha na kuwekeza katika jamii inapotoa huduma. Benki yetu hutenga asilimia moja ya faida yake baada ya kodi kwa ajili ya kuiwezesha jamii. Tunachangia madarasa, madawati, na miundombinu mingine ya shule. tunatoa vifaatiba na kuhamasisha afya ya jamii. Kupitia kampeni ya Pendezesha Tanzania, tunashiriki kutunza mazingira ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na tupo mstari wa mbele katika kuwawezesha wanawake na vijana kujitegemea kiuchumi,” amesema Rutasingwa.

Mkurugenzi huyo amefafanua kuwa utekelezaji wa Programu ya Employee Volunterring unaanzia ngazi ya mfanyakazi mmoja mmoja, matawi, ofisi za kanda mpaka idara za makao makuu ya Benki ya CRDB.

“Katika ngazi ya kanda, tayari tumeratibu na kutekeleza miradi katika kanda za Pwani, Dar es Salaam, na Kaskazini. Leo tunafungua ukurasa mpya wa jitihada hizi katika Kanda hii ya Ziwa kwa kukabidhi rasmi madarasa mawili na madawati 200 kwa shule hii ya Hamukoko hapa wilayani Ukerewe,” ameeleza Rutasingwa.

Kwa wazazi, Rutasingwa amewakumbusha umuhimu wa kuandaa mazingira haya ya kiuchumi kugharimia elimu akieleza kwamb benki ya CRDB inayo Akaunti ya Junior Jumbo inayomwezesha mzazi kuweka fedha taratibu kwa ajili y amahitaji ya mwanaye huku ikimwandaa mtoto kuwajibika kiuchumi kwa kuanza kutumia huduma za benki tangu akiwa mdogo.

“Akaunti hii haina makato na inamwezesha mzazi kuweka akiba kidogo kidogo kwa ajili ya masomo ya mtoto wake, kuanzia elimu ya awali hadi chuo kikuu. Unachohitaji ni cheti cha kuzaliwa cha mtoto, kitambulisho cha mzazi au mlezi, na shilingi 5,000 ya kuanzia ili kufungua akaunti hii,” amesema.

MHE. MCHENGERWA AWAFUNDA WALIMU

June 04, 2025 Add Comment

Na John Mapepele

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa ametoa rai kwa walimu nchini kuwa wazalendo na kuzingatia weledi ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi.

WAZIRI MCHENGERWA AWAFUNDA WALIMU AWATAKA WAWE WAZALENDO KUZINGATIA MAADILI

June 04, 2025 Add Comment


Na John Mapepele 


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Mhe. Mohamed Mchengerwa ametoa rai kwa walimu nchini kuwa wazalendo na kuzingatia weledi ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi. 


Mhe. Mchengerwa ametoa rai hiyo kwenye mkutano wa walimu na wadau wa elimu  wa Wilaya ya Rufiji uliofanyika kwenye ukumbi wa shule ya Sekondari ya Wasichana Bibi Titi Mohamed, ambapo yeye mwenyewe pia alitunukiwa tuzo ya heshima ya kutambua mchango wake katika sekta ya elimu wilayani Rufiji.

"Katika hali ya kawaida  Serikali imeboresha mazingira na miundombinu ya sekta ya elimu kilichobaki ni kwa sisi walimu kutanguliza uzalendo ili kuinua kiwango cha elimu katika ngazi zote" . Amesisitiza Mhe. Mchengerwa 


Aidha, amesisitiza walimu kutambua wajibu wao na kwamba Serikali haitaweza kusita kuwachukulia hatua za kinidhamu  Walimu na Maafisa Elimu ambao watakuwa wazembe katika utekelezaji wa majukumu yao.

Katika taarifa ya Wilaya ya Rufiji kwa Mhe. Waziri, iliyoandaliwa na  Mkurugenzi Mtendaji  wa Rufiji, bwana Simon Berege, inaonyesha kuwa kumekuwa na ongezeko la wanafunzi wanaohitimu darasa la Saba kutoka 3135 mwaka 2020 hadi wanafunzi 3715 mwaka 2024.


Idadi ya shule za Awali na Msingi zimeongezeka  kutoka 48 mwaka 2021 Hadi 63 mwaka 2025 ikiwa ni ongezeko la shule 15 sawa na asilimia 31.3.


Pia vyumba vya madarasa  vimeongezeka  kutoka vyumba 377 mwaka2921 hadi vyumba566 mwaka 2025 ikiwa ni ongezeko la vyumba vya madarasa 189 sawa na asilimia 50. 1

Aidha, katika mashindano ya UMITASHUMTA ngazi ya mkoa, Halmashauri ya Mji wa Rufiji imefanikiwa kushinda kwa nafasi ya kwanza katika michezo ya mpira wa miguu, pete na riadha huku ikishika nafasi ya pili kwenye mpira wa mikono hivyo kushika nafasi ya pili ya ujumla katika mashindano hayo.

Katika mkutano huo Mhe.Waziri Mchengerwa alikabidhi makombe hayo kwa shule na baadaye kupokea msaada wa madawati 50 yaliyotolewa na Benki ya CRDB.