TAKUKURU TANGA YABORESHA MFUMO WA HUDUMA ZA UDHIBITI TAKA NGUMU JIJINI TANGA

May 30, 2025 Add Comment


Na Oscar Assenga, TANGA

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoani Tanga (Takukuru) imesema kwamba moja ya mafanikio ya utendaji wake kazi katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari hadi Machi 2025 uboreshaji mfumo wa huduma za udhibiti Taka Ngumu Jijini Tanga.

Hayo yalisemwa leo na Kaimu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga Mariam Mayaya wakati akitoa taarifa kwa umma juu ya mafanikio ya utendaji kazi wa Taasisi hiyo kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025.

Alisema kwa upande wa uchambuzi wa mifumo katika kipindi hicho taasisi hiyo imefanikiwa kutekeleza matakwa ya sheria na kanuni za udhibiti taka ngumu nchini Tanzania kwa kutumia mfumo wa Punguza,Tumia Tena na Rejeleza taka (PTR) au Reduce,Re-use and Reycle (3R),

Aidha alisema katika mkoa wa Tanga mfumo huo ulianza katika kata ya Central,Chumbageni na Ngamiani Kati pamoja na utekelezaji wa sheria ya udhibiti wa taka ngumu,uchambuzi uliofanywa na Takukuru umesaidia mikakati na maazimio ya kulipwa kwa madeni ya wazabuni hivyo kufanya kazi ya uzoaji taka kuanza kutekelezwa kwa ufanisi.

Mariam alisema kwamba kwa ujumla zimefanyika chambuzi za mifumo 20 katika sekta za udhibiti take na usafi wa Mazingira,Afya,Kilimo na mapato ambapo wamefanikiwa kubaini mapungufu na kuwasilisha ripoti za chambuzi husika kwa wadau ambazo zimejadiliwa na maazimio yaliyofikiwa yametekelezwa na mengine yanaendelea kutekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumzia ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo,Mariam alisema kwamba katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025 walifanya kazi ya ufuatiliaji wa matumizi ya rasilimali za umma katika miradi 54 yenye thamani ya Bilioni 240,264,703,118.09.

Alisema katika ufuatiliaji wa miradi hiyo iliyopo katika sekta za Maji,Elimu na Afya ambapo miradi 12 yenye thamani ya Sh.Bilioni 5,468,760,058 ilibainika kuwa na mapungufu ambapo ushauri wa marekebisho yalitolewa na hatua za marekebisho ya mapungufu hayo zimechukuliwa na miradi ipo katika hali inayokidhi ubora kulingana na thamani ya fedha zilizowekezwa.

SAME KAYA SACCOS YARUDISHA KWA JAMII KWA KUTOA MSAADA WA VIFAA NA MAHITAJI MUHIMU

May 29, 2025 Add Comment

 



Na Ashrack Miraji Tanga Raha  

Katika kuendeleza uwajibikaji kwa jamii, taasisi ya kifedha ya SAME KAYA SACCOS imetoa msaada wa vifaa mbalimbali kwa makundi yenye uhitaji katika Wilaya ya Same, Mkoa wa Kilimanjaro. Msaada huo umetolewa kama sehemu ya kuadhimisha mchango wa jamii katika mafanikio ya SACCOS hiyo, ikiwa ni mfano bora wa taasisi za kifedha kurudisha kwa jamii wanakotoka.

Kwa mujibu wa Meneja wa SAME KAYA SACCOS, Bi Elvera Mdee, taasisi hiyo imetumia jumla ya Shilingi milioni tano (Tsh. Mil 5) katika kugharamia ununuzi wa bidhaa hizo, ambazo ni pamoja na vyakula, vinywaji, sare za shule (uniforms), vifaa vya usafi na vifaa vya shule (stationery).


Walengwa wa msaada huo ni pamoja na hospitali ya Wilaya ya Same, Shule ya Sekondari Chauka iliyopo Hedaru, pamoja na kituo cha kulelea yatima cha Rafiki Children Centre kilichopo mjini Same. Kila taasisi ilipokea msaada kulingana na mahitaji maalum yaliyobainishwa awali.

Katika hafla ya kukabidhi misaada hiyo, Bi Elvera Mdee alieleza kuwa SAME KAYA SACCOS inaamini katika kuijali jamii na kuwa karibu na wananchi, hasa wale walio katika mazingira magumu. Alisisitiza kuwa mafanikio ya taasisi hiyo hayawezi kufikiwa bila ushirikiano kutoka kwa wananchi wa Wilaya ya Same.

Aidha, alitoa wito kwa taasisi nyingine za kifedha na wafanyabiashara binafsi kujitokeza na kusaidia jamii, hususan katika kipindi hiki ambapo hali ya kiuchumi imekuwa changamoto kwa wengi. “Tunaamini kwamba kila mmoja wetu ana wajibu wa kusaidia kule tunakoweza. SAME KAYA SACCOS inatambua umuhimu wa mshikamano na upendo kwa jamii,” alisema.


Wazazi, walimu na walezi waliopokea msaada huo kwa niaba ya walengwa walitoa shukrani zao kwa taasisi hiyo, wakieleza kuwa msaada huo umekuja wakati muafaka na utaongeza ari ya watoto kuhudhuria shule, pamoja na kuboresha huduma za afya na mazingira ya usafi katika maeneo yao.

SAME KAYA SACCOS imekuwa mstari wa mbele si tu katika utoaji wa huduma za kifedha, bali pia katika kuhakikisha kuwa jamii inayowazunguka inanufaika moja kwa moja na mafanikio ya taasisi hiyo. Hii ni sehemu ya dira yao ya kuhakikisha maendeleo jumuishi na yenye uwiano kwa wote




 

NCAA YATOA MAFUNZO KWA WADAU WA UTALII KUHUSU MATUMIZI YA MFUMO MPYA WA SAFARI PORTAL V2

May 29, 2025 Add Comment


Na Kassim Nyaki, NCAA.


Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) imetoa mafunzo ya siku mbili kuanzia tarehe 29 hadi 30 Mei, 2025 kwa wadau wa Utalii kuhusiana na matumizi ya mfumo mpya wa *Safari Portal V2* ulioboreshwa kutoka mfumo wa zamani wa Safari Portal.


Akifungua Mafunzo hayo Kaimu Meneja wa Huduma za Utalii na masoko NCAA, Afisa Uhifadhi Mkuu Peter Makutian ameeleza kuwa mafunzo hayo yamelenga kuwajengea uwezo wadau wote wa Utalii kuhusu matumizi ya mfumo mpya wa makusanyo ya mapato yatokanayo na shughuli za Utalii ambao umeboreshwa ili kurahisisha utoaji huduma kwa wadau wote wanaofanya kazi na NCAA.

"Tumeboresha mfumo wetu wa makusanyo ya mapato ya Utalii na utaaanza kutumika kuanzia tarehe  31/05/2025, kwa hiyo ni muhimu wadau wetu wanaopata huduma kupitia mfumo huu wawe na uelewa ya maboresho yaliyofanyika na kuwasaidia namna ya kuhamisha taarifa zao kwenye mfumo mpya kabla ya tarehe ya kuanza mfumo huo" alilisitiza Makuatian.


Makutian ameongeza kuwa sababu zilizopelekea kuboresha mfumo huo ni kuendana na mabadiliko ya kukua kwa teknolojia ya habari na mawasiliano sambamba na kuzingatia mapendekezo ya Wadau wa utalii ambao ndio watumiaji wakuu wa mfumo huo.

Mafunzo hayo yameshirikisha makundi mbalimbali katika mnyororo wa sekta ya utalii ikiwemo Waongoza watalii, wamiliki wa kampuni za utalii, madereva wa utalii, wamiliki wa hoteli na wadau wengine wanaohusika na sekta ya Utalii.

Wadau wa utalii walioshiriki mafunzo hayo wametoa pongezi kwa uongozi wa NCAA kwa maboresho ya mfumo huo ambao umerahisisha taratibu za malipo bila kutumia mda mrefu wanapokuwa na shughuli za utalii na wageni ndani ya hifadhi ya Ngorongoro



DKT.BITEKO ATAJA MAENEO SITA YA VIPAUMBELE UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM 2020/2025

May 29, 2025 Add Comment


📌 CCM yajivunia kuimarisha upatikanaji wa huduma bora kwa jamii


📌 Rais Samia asema CCM kuzindua Ilani yake kesho


📌 CCM yazalisha ajira 800,000 kwa vijana 2020/2025


Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amesema kuwa mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita aliyowasilisha ni ya mwisho katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020. 


Amesema hayo Mei 29, 2025 wakati akiwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Mkutano Mkuu Maalum wa  CCM Taifa - 2025 jijini Dodoma kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa. 


Ametaja maeneo sita muhimu ya vipaumbele  katika utekelezaji wa Ilani hiyo ya CCM kuwa ni pamoja na kulinda  na kuimarisha misingi ya utu, usawa, haki na uongozi bora ili kudumisha amani, umoja na mshikamano wa Taifa.

Dkt. Biteko ameendelea kwa kusema kuwa eneo lingine ni kukuza  uchumi wa kisasa, fungamanishi, jumuishi na shindani  uliojengwa katika msingi wa viwanda, huduma za kiuchumi na miundombinu wezeshi.


Aidha, kipaumbele kingine “ Kuleta mageuzi ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kuwa na uhakika wa chakula na kujitegemea kwa chakula wakati wote na kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya uchumi na kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya, elimu, maji, umeme na makazi vijijini na mijini na kutengeneza ajira zisizopongua milioni nane katika sekta rasmi na isiyo rasmi kwa ajili ya vijana,”  ameongeza Dkt. Biteko.

Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesema kuwa kumekuwepo na mafanikio makubwa ikiwemo nchi kuendelea kuwa na amani, umoja na mshikamano pamoja na kuendelea kuenzi Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar na kudumisha Muungano wa Tanzania.


“ Vilevile, Serikali imeendelea kuimarisha demokrasia, utawala bora na haki za binadamu kwa kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kuondoa zuio la mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa na hivyo kuimarisha uhuru wa vyombo vya habari ili kuwezesha wananchi kupata habari kwa wakati,” amesema Dkt. Biteko.

Ameendelea kusema  kuwa mafanikio hayo  yamechagizwa na falsafa aliyoianzisha Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya 4R ambayo ni Maridhiano, Ustahimilivu, Mabadiliko na Kujenga Upya.


Amesisitiza “ Falsafa  hiyo imekuwa dira na nguzo muhimu ya kisera katika kuijenga upya Tanzania yenye mshikamano, haki na maendeleo endelevu kwa misingi ya demokrasia na ushirikishwaji wa wananchi katika masuala ya msingi ya Taifa.”



Kupitia mkutano huo Dkt. Biteko alielezea mafanikio ya Rais Samia kitaifa na kimataifa hususan katika sekta ya nishati kwa kuwa kinara wa nishati safi ya kupikia barani Afrika.


Akihutubia katika mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema kuwa Mkutano Mkuu huo ni sehemu muhimu ya maandalizi ya kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.


“ Kesho  tutafanya uzinduzi wa Ilani tutakayoinadi kwa wananchi ili kutupa nafasi nyingine ya kuongoza kwa miaka mitano,” amesema Dkt. Samia.


Amebainisha  kuwa Ilani hiyo imehusisha vipaumbele  vya Chama na kuwa kabla ya kuiwasilisha  kwa wajumbe wameona ni muhimu kupitia utekelezaji wa Ilani ya mwaka 2020 hadi 2025.


Akizungumza katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa CCM, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema  lengo la  mkutano huo ni kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa mwaka  2020 hadi 2025, kuzindua Ilani mpya 2025 hadi 2030 na kupitia maboresho machache ya Katiba ya CCM.


Aidha, Mkutano huo ulioongozwa  na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan umehudhuriwa na viongozi wa vyama vya siasa nchini, mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania pamoja wawakilishi wa vyama rafiki kutoka nchi mbalimbali za Afrika, China na Korea ya Kaskazini na Urusi.

 

MWISHO

DCEA YAIMARISHA MAPAMBANO DHIDI YA DAWA ZA KULEVYA KUPITIA MAFUNZO KWA VIONGOZI WA MITAA SAME

May 29, 2025 Add Comment

 



Na Ashrack Miraji Tanga Raha

Katika harakati za kitaifa za kuikomboa jamii dhidi ya janga la dawa za kulevya, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) Kanda ya Kaskazini imeendesha mafunzo maalum kwa viongozi wa serikali kuanzia ngazi ya wilaya hadi vitongoji, katika Wilaya ya Same, mkoani Kilimanjaro.

Mafunzo hayo yaliyofanyika leo, Mei 29, 2025, katika Ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, yamelenga kuwawezesha viongozi hao kutambua, kuzuia na kushughulikia changamoto zinazotokana na matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya. Viongozi hao pia wamehimizwa kuzingatia maadili, uwajibikaji na ushirikiano wa kijamii katika mapambano hayo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Same, Mheshimiwa Kasilda Mgeni, alisema kuwa dawa za kulevya si tu kwamba zina madhara ya kiafya kwa binadamu, bali pia zinachangia kudhoofisha uchumi, kuvuruga familia, kuporomosha maadili, kupunguza nguvu kazi ya taifa na kuongeza matukio ya uhalifu.


Alisema: “Hili ni janga linalohitaji nguvu ya pamoja kuanzia kwa viongozi, wazazi, walimu na vijana wenyewe ambao ndio waathirika wakuu wa dawa za kulevya. Hivyo nawahimiza kupitia mafunzo haya mkawe mabalozi na waelimishaji; muhamasishe na msimamie utekelezaji wa mikakati ya kupambana na dawa za kulevya katika maeneo yenu.”

Aidha, aliwataka viongozi wa serikali kuhakikisha kuwa wanakuwa wawajibikaji, waadilifu na kutojihusisha au kufumbia macho biashara haramu ya dawa za kulevya katika maeneo yao. Alibainisha kuwa serikali haitasita kuchukua hatua dhidi ya yeyote atakayebainika kujihusisha na vitendo hivyo.


Kwa upande wake, Afisa Elimu kutoka Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Kanda ya Kaskazini, Ndg. Shaban Miraji, alisema kuwa sababu kuu zinazochangia matumizi ya dawa za kulevya ni pamoja na malezi duni, ukosefu wa elimu sahihi kuhusu madhara ya dawa hizo, pamoja na hali ngumu ya kiuchumi.

Kwa upande wake Katibu tawala wa wilaya ya Same.  Bi. Upendo Wela akifunga Mafunzo hayo amesema kuwa ni wajibu wa kila mmoja aliyepata mafunzo hayo kuhakikisha wanapambana na kilimo cha mirungi na bangi ili kiweze kumalizika kabisa ndani ya wilaya ya Same kwa kushirikiana kwa pamoja

Kwa mujibu wa Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ya mwaka 2015, mtu yeyote atakayekutwa akilima bangi au mirungi, kufanya biashara, kusafirisha au kumiliki kiasi cha bangi au mirungi kisichozidi kilo 100, atahukumiwa kifungo kisichopungua miaka 30. Iwapo kiasi hicho kitazidi kilo 100, adhabu ni kifungo cha maisha.

Mafunzo hayo yaliambatana na mada mbalimbali, ambapo mada kuu ilikuwa kuhusu dawa za kulevya, huku nyingine zikihusu maadili kwa watumishi wa umma, mapambano dhidi ya rushwa, pamoja na kuhamasisha kilimo mbadala kama njia ya kujenga uchumi wa mtu mmoja mmoja na jamii kwa ujumla.