Benki ya CRDB Yaadhimisha Miaka 30 kwa Kutoa Jumla ya Gawio Kubwa Zaidi Kuwahi Kutokea la Shilingi Bilioni 170

May 19, 2025 Add Comment

 

Arusha 17 Mei 2025 - Katika Mkutano Mkuu wa 30 wa Mwaka wa Wanahisa (AGM) uliofanyika katika kituo cha mikutano cha AICC, wanahisa walikubaliana kwa kauli moja kuidhinisha gawio la Shilingi 65 kwa kila hisa, kiwango cha juu zaidi kuwahi kutolewa katika historia ya benki hiyo.


Jumla ya gawio lililotangazwa kwa mwaka wa fedha wa 2024 ni Shilingi bilioni 170, ikionyesha uimara wa utendaji wa kifedha wa benki na dhamira yake ya kudumu ya kutoa thamani endelevu kwa wanahisa wake.
Akizungumza wakati wa mkutano huo, uliofanyika kwa mfumo wa mseto ambapo wanahisa wengine walishiriki kidijitali, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Dkt. Ally Laay, alielezea fahari yake juu ya safari ya mafanikio ya benki hiyo kwa kipindi cha miongo mitatu iliyopita.

"Tukiadhimisha miaka 30 ya ubora katika huduma za kibenki, gawio hili la kihistoria ni ishara ya uimara wetu wa kifedha na pia ni zawadi ya kipekee kwa wanahisa waliotuamini na kutembea nasi katika safari ya mabadiliko, ubunifu na ukuaji," alisema Dkt. Laay.

Alieleza kuwa gawio la Shilingi 65 kwa hisa, ambalo ni ongezeko la asilimia 30 kutoka mwaka uliopita, linaakisi ongezeko la faida kwa kila hisa hadi kufikia TZS 211.5 kwa mwaka 2024, likichochewa na muundo thabiti wa uendeshaji wa benki, uongozi wa kimkakati na wafanyakazi wenye moyo wa kujituma.

Faida ya Benki ya CRDB baada ya kodi ilikua kwa asilimia 30 hadi kufikia TZS bilioni 551, ikiashiria mafanikio ya mkakati wa muda mrefu wa benki na ufanisi wa uendeshaji. Dkt. Laay pia alizipongeza kampuni tanzu za benki kwa mchango wao unaoongezeka katika mafanikio ya kundi, ambapo kwa pamoja zimetoa mchango wa asilimia 6 katika Faida ya kundi.
CRDB Bank Burundi ilipata faida baada ya kodi ya Shilingi bilioni 40.3, huku CRDB Insurance ikiwa katika mwaka wake wa kwanza wa biashara, ilipata faida ya TZS milioni 343, na hivyo kuimarisha mapato yasiyotokana na riba.

Wakati huo huo, kampuni tanzu ya Benki ya CRDB DR Congo inaendelea kuonyesha mwelekeo mzuri wa ukuaji na inatarajiwa kufikia kiwango cha faida mapema kuliko ilivyotarajiwa.
Akiwasilisha ripoti yake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kundi la Benki ya CRDB, Abdulmajid Mussa Nsekela, alijivunia mafanikio ya miaka 30 ya benki hiyo na kueleza mwelekeo wa miaka ijayo: “Tukiadhimisha miongo mitatu ya kuboresha maisha na kujenga uchumi wa watu wetu na nchi zetu, mafanikio ya mwaka 2024 yanadhihirisha kuwa safari yetu ndio kwanza inaanza.

Hatua inayofuata ni ya kuleta ushirikishwaji mpana zaidi, mabadiliko ya kidijitali, na athari chanya katika ukanda wetu wa Afrika.”

Nsekela alieleza kuwa mali za benki zimeongezeka hadi kufikia Shilingi trilioni 16.7 (+25.3%), na mkopo wa jumla umefikia Shilingi trilioni 10.4 (+22.7%) kutokana na mikakati inayowalenga wateja na uwezeshaji kupitia mikopo. Benki pia iliongeza upatikanaji wa huduma kwa makundi yaliyosahaulika huduma shirikishi kama akaunti ya Sadaka na mikopo kwa wajasiriamali wadogo wadogo kupitia mifumo ya kidijitali.
Alitaja pia ushiriki wa benki katika miradi mikubwa ya kikanda kama vile uwezeshaji wa viwanda vya grafiti kwa kushirikiana na DBSA na IDC, jambo linaloifanya Benki ya CRDB kuwa kichocheo cha ongezeko la thamani na uanzishaji viwanda Afrika Mashariki na Kati.

Uwiano wa gharama na mapato wa benki uliimarika hadi kufikia asilimia 45.7, huku Uwiano wa Mikopo Chechefu (NPL) ukiendelea kuwa chini kwa asilimia 2.9, ikiashiria nidhamu madhubuti ya usimamizi wa gharama na ubora wa mikopo. Uwekezaji katika usanifu wa mfumo wa biashara, uhimilivu wa mtandao na miundombinu ya msingi ya kibenki, umehakikisha uendeshaji thabiti katika mazingira ya kidijitali yanayobadilika kwa kasi.
Nsekela alitoa shukrani kwa wanahisa kwa kuendelea kuiamini benki hiyo, huku akisisitiza maono ya muda mrefu ya benki: “Maadhimisho haya ya miaka 30 ni hatua ya kihistoria. Dira yetu haijabadilika, kuwa taasisi ya kifedha inayoaminika, yenye athari chanya, na tayari kwa siku zijazo kwa vizazi vijavyo.”

Kwa kuzingatia misingi ya utawala bora, wanahisa waliidhinisha kuteuliwa tena kwa Price Waterhouse Coopers (PwC) kuwa wakaguzi wa nje wa benki kwa mwaka wa fedha wa 2025. Aidha, wanahisa walikubaliana kwamba Mkutano Mkuu wa 31 wa Mwaka ufanyike tarehe 23 Mei 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC). Mkutano huo pia uliidhinisha kuchaguliwa kwa wajumbe katika makundi yafuatayo:

• Bw. Abdul Ally Mohamed, Bi. Grace Joachim na Dkt. Donald Mmari kuwakilisha wanahisa walio na umiliki chini ya asilimia 1,
• Dkt. Fred Msemwa aliteuliwa tena kuwakilisha wanahisa wenye umiliki kati ya asilimia 1–10
• Na Dkt. Judica King’ori aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Huru.
Akizungumza katika mkutano huo, Balozi wa Tanzania nchini Burundi, Mheshimiwa Gelasius Byakanwa, alisifu mageuzi ya benki hiyo: “Benki ya CRDB imekuwa mfano bora wa thamani kwa wanahisa na uadilifu wa kifedha. Rekodi yake ya kutoa gawio kila mwaka na utendaji wake mzuri katika soko la hisa ni ushahidi wa uongozi imara usio na kifani kwa kipindi cha miaka 30.”


WENYE VYETI FEKI VYA UANDISHI WA HABARI WAONYWA

May 19, 2025 Add Comment


Na Mwandishi Wetu, JAB

Wakati Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) ikiufungua rasmi mfumo wa usajili wa Waandishi wa Habari wa https://taihabari.go.tz ili kuomba kuthibitishwa na kupatiwa Kitambulisho cha Uandishi wa Habari (Press Cards) Mwenyekiti wa Bodi hiyo Ndg. Tido Mhando amewaonya wenye nia ya kutumia vyeti visivyo halali wakati wa kujaza taarifa zao.


Mhando alitoa tahadhali hiyo tarehe 19 Mei, 2025 wakati akizungumza na Wahariri na Waandishi wa Habari wa vyombo mbalimbali vya Habari katika ofisi za Bodi hiyo zilizopo Mtaa wa Jamhuri jijini Dar es Salaam.


“Ndugu zangu Waandishi wa Habari, Bodi hii itaanza kutoa ithibati kwa waandishi wa habari wote kupitia mtandao na kutoa vitambulisho vya kidijiitali (digital Press Card).  Maombi ya ithibati Press Cards yatafanyika kupitia Mfumo unaoitwa TAI-Habari”, alisema.


Mhando alisema mahitaji muhimu wakati wa kujaza taarifa katika mfumo huo kuwa ni pamoja na namba ya simu na barua pepe vinavyofanya kazi, picha ndogo (passport size) iliyoskaniwa barua ya utambulisho kutoka taasisi anayotoka au anakopeleka kazi zake ikiwa ni mwandishi wa kujitegemea (Freelancer), nakala ya Kitambulisho cha Taifa (NIDA) na ada ya ithibati shilingi Elfu Hamsini (50,000).

“Mahitaji mengine ni vyeti vya elimu vilivyoskaniwa kwa mfumo wa PDF na kuthibitishwa na Mamlaka husika (kama chuo kikuu vithibitishwe na TCU na kama ni vyuo vya kati vithibitishwe na NACTVET), na katika hili nisisitize tafadhali sana usiweke cheti ‘feki’ jambo hilo linakiuka siyo tu linakiuka maadili ya taaluma habari, bali pia ni makosa yanatakayodhibitiwa kwa mujibu wa Sheria za nchi,” alisema Mhando.

Mhando alisema mahitaji hayo ni muhimu ili kukamilisha mchakato wa maombi kwa mafanikio na kwamba ni hatua inayolenga kuboresha huduma, kuimarisha usimamizi wa taaluma ya Uandishi wa Habari na kurahisisha upatikanaji wa vitambulisho kwa waandishi waliothibitishwa.


Aliomba Wahariri, Waandishi na wadau wote wakiwemo waajiri kutambua umuhimu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari katika kuimarisha weledi, maadili, na uwajibikaji wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, na hivyo watoe ushirikiano wa hali ya juu katika kukuza na kuendeleza taaluma hiyo muhimu kwa taifa.



Akijibu maswali ya waandishi wa Habari kuhusu watu walio kwenye tasnia bila kuwa na vyeti vya Elimu ya Uandishi wa Habari, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo Wakili Patrick Kipangula alisema Sheria ilitoa muda wa miaka mitano kwa watu waliokuwa hawana sifa ili wakasome na kutimiza vigezo vya kisheria.


Alisema baada ya muda huo kuisha Waziri aliongeza muda wa mwaka mmoja na kwamba tangu Waziri aongeze mwaka mmoja ni miaka miwili imeshapita na kufanya jumla ya miaka nane na hivyo hakutakuwa na muda wa nyongeza tena.

RAIS SAMIA NA RAIS MSTAAFU KIKWETE WAPONGEZWA KWA KUFANIKISHA USHINDI WA PROFESA JANABI KATIKA UCHAGUZI WA MKURUGENZI WA WHO KANDA YA AFRIKA

May 19, 2025 Add Comment


Na Mwandishi `Maalumu


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa maono yake ya mbali na uamuzi wa busara wa kumpendekeza Profesa Mohamed Yakub Janabi kugombea nafasi ya Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

Wananchi mbalimbali waliohojiwa wametaja hatua hiyo ya Rais Samia kama ishara ya kujiamini kama taifa, na uthibitisho kuwa Watanzania wanao uwezo wa kushika nafasi nyeti katika taasisi kubwa za kimataifa, wakielezea faraja yao kwa jinsi Tanzania inavyozidi kung’ara kwenye majukwaa ya kidiplomasia duniani.

Aidha, Rais Samia amesifiwa kwa kuunda kikosi kazi maalum kilichoongozwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa ajili ya kuratibu na kusimamia kampeni ya kidiplomasia ya Profesa Janabi. 


Ushirikiano huo umeibuka na  matokeo chanya, ambapo Profesa Janabi ameibuka mshindi kwa kishindo kupitia mchakato wa uchaguzi uliopigiwa kura na nchi wanachama wa WHO Kanda ya Afrika.

Dkt. Kikwete, ambaye ana uzoefu mkubwa katika medani za kimataifa, amepongezwa kwa kutumia umahiri na uhusiano wake wa kidiplomasia kuhakikisha kampeni hiyo inafanikiwa. Mchango wake umetajwa kama kichocheo muhimu kilichowezesha Tanzania kupata ushindi dhidi ya wagombea kutoka Côte d’Ivoire, Guinea na Togo.


Katika picha iliyopigwa wakati wa harakati za kampeni hiyo, Dkt. Kikwete anaonekana akiongoza moja ya vikao vya kikosi kazi hicho, ambacho hatimaye kilitimiza azma yake mnamo Jumapili, Mei 18, 2025, kwa ushindi mkubwa wa Profesa Janabi. 

Mgombea huyo wa Tanzania alipata kura 32 kati ya 47 zilizopigwa kwa siri na wajumbe wa nchi wanachama wa WHO Afrika, kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu wa WHO.


Uchaguzi huo umefanyika kufuatia kifo cha ghafla cha aliyekuwa Mkurugenzi mteule, Dkt. Faustine Ndugulile, mnamo Novemba 2024. Nafasi hiyo ilivuta wagombea mahiri kutoka mataifa kadhaa, lakini Profesa Janabi alifanikiwa kuungwa mkono kwa wingi, akionesha kuwa jina la Tanzania bado lina nguvu katika diplomasia ya afya barani Afrika.


Kwa mujibu wa taratibu za Shirika la Afya Duniani, jina la Profesa Janabi sasa litawasilishwa kwa ajili ya kuthibitishwa rasmi na Bodi ya Utendaji ya WHO katika kikao chake cha 157 kitakachofanyika Mei 28–29, 2025, mjini Geneva, Uswisi.


Iwapo atathibitishwa, Profesa Janabi ataapishwa na kuanza kutekeleza rasmi majukumu yake kwa kipindi cha miaka mitano, huku akiwa na fursa ya kuongezewa muhula mmoja zaidi kulingana na kanuni za taasisi hiyo.

WAZIRI MKUU MAJALIWA : SERIKALI IMEJIPANGA KUDHIBITI MAGUGUMAJI ZIWA VICTORIA

May 19, 2025 Add Comment


_▪️Amshukuru Rais Dkt. Samia ununuzi wa mitambo ya uteketezaji wa magugumaji

 

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha changamoto ya uwepo wa magugumaji katika ziwa Victoria inapatiwa ufumbuzi ili kuwezesha shughuli za kijamii ziweze kuendelea katika maeneo hayo.

 



”Ninamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutoa fedha za ununuzi wa mitambo mikubwa ya kuteketeza magugumaji ndani ya ziwa Victoria ili kuwezesha shughuli za uvuvi, usafiri na usafirishaji kuendelea.”

 

Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu, Mei 19, 2025) wakati akizungumza na wananchi alipokagua shughuli ya udhibiti wa magugumaji katika eneo la Kigongo-Busisi akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza.

 


Mheshimiwa Majaliwa amesema magugumaji hayo yamekuwa yakiathiri kwa kiwango kikubwa shughuli mbalimbali za kijami na kiuchumi katika ziwa hilo, hivyo ununuzi wa mitambo hiyo utasaidia kuteketezwa kwa magugu hayo.

 

Aidha, Waziri Mkuu amewashukuru wananchi wa maeneo hayo wakiwemo wavuvi ambao wamejitolea kushirikiana na Serikali katika zoezi la kuyaondoa magugumaji hayo.

 

Wakati huo huo, Waziri Mkuu ameiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira iendelee na kazi ya kuyaondoa magugumaji hayo hadi pale yatakapomalizika ili kuhakikisha shughuli za kijami zinaendelea bila ya kikwazo chochote.

 

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Cyprian Luhemeja akitoa taarifa kuhusu shughuli ya kuteketeza magugumaji hayo kwa Waziri Mkuu amesema kwa sasa wanaendelea na kazi ya kuyaondoa magugumaji ya asili ambayo yamesambaa katika eneo la ukubwa wa ekari zaidi ya 300.

 

Amesema magugumaji hayo ambayo yamegawanyika katika aina tatu (salivinia molesta ambalo ni jipya, water hyacinth na gugumaji la asili aina ya Lutende) yameathiri mfumo wa ikolojia, shughuli za usafiri na usafirishaji na shughuli za uvuvi katika baadhi ya maeneo ndani ya Ziwa Victoria

 

Katibu Mkuu huyo amesema wanatarajia kumaliza kazi ya kuyateketeza magugumaji mwezi Julai, 2025 na hivyo kuwezesha shughuli za uvuvi, usafiri na usafirishaji kuendelea katika ziwa Victoria kama ilivyokuwa awali.

BIASHARA YA MAZAO YA MISITU NA NYUKI YAPAA – MAUZO NJE YA NCHI YAONGEZEKA KWA ASILIMIA 333%

BIASHARA YA MAZAO YA MISITU NA NYUKI YAPAA – MAUZO NJE YA NCHI YAONGEZEKA KWA ASILIMIA 333%

May 19, 2025 Add Comment

 MH CHANA.jpg

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana akiwasilisha akadirio ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
-----
WhatsApp Image 2025-05-19 at 10.42.45.jpeg

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Kutoka kushoto ni Kamishna wa Uhifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Prof. Dos Santos Silayo, akiwa na makamishna wengine wa uhifadhi wafuatilia kwa makini hoja mbalimbali, ikiwemo mafanikio makubwa ya TFS katika usimamizi endelevu wa rasilimali za misitu na nyuki Mei 19,2025—ikiwa ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kujenga uchumi shirikishi wa kijani.

Serikali imebainisha mafanikio makubwa katika biashara ya mazao ya misitu na nyuki nchini, ikiwemo ongezeko la uzalishaji, viwanda na mauzo nje ya nchi, ikiwa ni matokeo ya uwekezaji wa kimkakati unaofanywa kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Akizungumza leo Mei 19, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati wa kuwasilisha makadirio ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Balozi Dkt. Pindi Chana alisema kuwa ndani ya miaka mitano, sekta hizo mbili zimeonyesha ushahidi wa wazi wa kuimarika kwa msingi wa uchumi wa kijani nchini.

Aliongeza kuwa, katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2020/2021 hadi 2024/2025, uzalishaji wa mbao kutoka mashamba ya miti ya Serikali unaolimwa kibiashara umeongezeka kutoka mita za ujazo 1,108,791 hadi 1,264,535, ikiwa ni ongezeko la zaidi ya 155,000 m³.

Aidha, viwanda vya kati na vikubwa vya kuchakata na kuongeza thamani ya mazao ya misitu vimeongezeka kutoka 636 mwaka 2020 hadi 1,671 mwaka 2025, huku viwanda vidogo vidogo kama vya useremala vikifikia zaidi ya 7,000 kote nchini.

Waziri Chana alisema kuwa thamani ya mauzo ya mazao ya misitu nje ya nchi nayo imepanda kwa kasi, kufikia Shilingi 458.47 bilioni mwaka 2024/2025, kutoka Shilingi 105.68 bilioni mwaka 2020/2021. Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 333.8, jambo alilolieleza kuwa ni matokeo ya kuimarika kwa viwango vya usimamizi na ubora wa bidhaa zinazozalishwa.

Katika upande wa nyuki, Serikali imewezesha ujenzi wa viwanda nane (8) vya kati na vikubwa vya kuchakata na kuongeza thamani ya mazao ya nyuki, kutoka kiwanda kimoja (1) mwaka 2020. Viwanda hivyo vimejengwa katika mikoa ya Tabora, Kigoma, Singida, Iringa, Katavi na Geita.

Mpaka kufikia Aprili 2025, Tanzania imeuza nje ya nchi jumla ya tani 1,321.35 za asali zenye thamani ya Shilingi 15.86 bilioni, ikilinganishwa na tani 430.61 za mwaka 2020/2021 zenye thamani ya Shilingi 5.17 bilioni — ikiwa ni ongezeko la asilimia 206.9.

Kutokana na mafanikio haya, Shirika la Wafugaji Nyuki Duniani limeiteua Tanzania kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Dunia wa Wafugaji Nyuki (APIMONDIA) utakaofanyika mwaka 2027 na kuhudhuriwa na watu zaidi ya 4,000 kutoka mataifa mbalimbali duniani.
“Kuongezeka kwa uzalishaji na thamani ya mauzo ya mazao ya misitu na nyuki ni ushahidi wa mafanikio ya ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi. Tunajenga msingi wa uchumi wa kijani unaozingatia uhifadhi, maendeleo ya viwanda na ajira kwa vijana wetu,” alisisitiza Waziri Chana.

Katika hatua nyingine, Waziri Chana amewakaribisha wabunge wote na wadau wengine wa sekta ya maliasili kushiriki maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani ambayo yanaendelea jijini Dodoma, na kufikia kilele chake kesho Mei 20, 2025 katika katika viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.


--

Tulizo Henry Kilaga I A Brand Communication Strategist,

Located: Dodoma I Dar es Salaam - Tanzania. 

Call/WhatsApp: +255 765 888887

www.thestrategist.co.tz