

HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI
Na Mwandishi Wetu, JAB
Wakati Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) ikiufungua rasmi mfumo wa usajili wa Waandishi wa Habari wa https://taihabari.go.tz ili kuomba kuthibitishwa na kupatiwa Kitambulisho cha Uandishi wa Habari (Press Cards) Mwenyekiti wa Bodi hiyo Ndg. Tido Mhando amewaonya wenye nia ya kutumia vyeti visivyo halali wakati wa kujaza taarifa zao.
![]() |
Mhando alitoa tahadhali hiyo tarehe 19 Mei, 2025 wakati akizungumza na Wahariri na Waandishi wa Habari wa vyombo mbalimbali vya Habari katika ofisi za Bodi hiyo zilizopo Mtaa wa Jamhuri jijini Dar es Salaam.
“Ndugu zangu Waandishi wa Habari, Bodi hii itaanza kutoa ithibati kwa waandishi wa habari wote kupitia mtandao na kutoa vitambulisho vya kidijiitali (digital Press Card). Maombi ya ithibati Press Cards yatafanyika kupitia Mfumo unaoitwa TAI-Habari”, alisema.
Mhando alisema mahitaji muhimu wakati wa kujaza taarifa katika mfumo huo kuwa ni pamoja na namba ya simu na barua pepe vinavyofanya kazi, picha ndogo (passport size) iliyoskaniwa barua ya utambulisho kutoka taasisi anayotoka au anakopeleka kazi zake ikiwa ni mwandishi wa kujitegemea (Freelancer), nakala ya Kitambulisho cha Taifa (NIDA) na ada ya ithibati shilingi Elfu Hamsini (50,000).
“Mahitaji mengine ni vyeti vya elimu vilivyoskaniwa kwa mfumo wa PDF na kuthibitishwa na Mamlaka husika (kama chuo kikuu vithibitishwe na TCU na kama ni vyuo vya kati vithibitishwe na NACTVET), na katika hili nisisitize tafadhali sana usiweke cheti ‘feki’ jambo hilo linakiuka siyo tu linakiuka maadili ya taaluma habari, bali pia ni makosa yanatakayodhibitiwa kwa mujibu wa Sheria za nchi,” alisema Mhando.
Mhando alisema mahitaji hayo ni muhimu ili kukamilisha mchakato wa maombi kwa mafanikio na kwamba ni hatua inayolenga kuboresha huduma, kuimarisha usimamizi wa taaluma ya Uandishi wa Habari na kurahisisha upatikanaji wa vitambulisho kwa waandishi waliothibitishwa.
Aliomba Wahariri, Waandishi na wadau wote wakiwemo waajiri kutambua umuhimu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari katika kuimarisha weledi, maadili, na uwajibikaji wa taaluma ya uandishi wa habari nchini, na hivyo watoe ushirikiano wa hali ya juu katika kukuza na kuendeleza taaluma hiyo muhimu kwa taifa.
Akijibu maswali ya waandishi wa Habari kuhusu watu walio kwenye tasnia bila kuwa na vyeti vya Elimu ya Uandishi wa Habari, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi hiyo Wakili Patrick Kipangula alisema Sheria ilitoa muda wa miaka mitano kwa watu waliokuwa hawana sifa ili wakasome na kutimiza vigezo vya kisheria.
Alisema baada ya muda huo kuisha Waziri aliongeza muda wa mwaka mmoja na kwamba tangu Waziri aongeze mwaka mmoja ni miaka miwili imeshapita na kufanya jumla ya miaka nane na hivyo hakutakuwa na muda wa nyongeza tena.
Na Mwandishi `Maalumu
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepongezwa kwa maono yake ya mbali na uamuzi wa busara wa kumpendekeza Profesa Mohamed Yakub Janabi kugombea nafasi ya Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika wa Shirika la Afya Duniani (WHO).
Wananchi mbalimbali waliohojiwa wametaja hatua hiyo ya Rais Samia kama ishara ya kujiamini kama taifa, na uthibitisho kuwa Watanzania wanao uwezo wa kushika nafasi nyeti katika taasisi kubwa za kimataifa, wakielezea faraja yao kwa jinsi Tanzania inavyozidi kung’ara kwenye majukwaa ya kidiplomasia duniani.
Aidha, Rais Samia amesifiwa kwa kuunda kikosi kazi maalum kilichoongozwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa ajili ya kuratibu na kusimamia kampeni ya kidiplomasia ya Profesa Janabi.
Ushirikiano huo umeibuka na matokeo chanya, ambapo Profesa Janabi ameibuka mshindi kwa kishindo kupitia mchakato wa uchaguzi uliopigiwa kura na nchi wanachama wa WHO Kanda ya Afrika.
Dkt. Kikwete, ambaye ana uzoefu mkubwa katika medani za kimataifa, amepongezwa kwa kutumia umahiri na uhusiano wake wa kidiplomasia kuhakikisha kampeni hiyo inafanikiwa. Mchango wake umetajwa kama kichocheo muhimu kilichowezesha Tanzania kupata ushindi dhidi ya wagombea kutoka Côte d’Ivoire, Guinea na Togo.
Katika picha iliyopigwa wakati wa harakati za kampeni hiyo, Dkt. Kikwete anaonekana akiongoza moja ya vikao vya kikosi kazi hicho, ambacho hatimaye kilitimiza azma yake mnamo Jumapili, Mei 18, 2025, kwa ushindi mkubwa wa Profesa Janabi.
Mgombea huyo wa Tanzania alipata kura 32 kati ya 47 zilizopigwa kwa siri na wajumbe wa nchi wanachama wa WHO Afrika, kabla ya kuanza kwa Mkutano Mkuu wa WHO.
Uchaguzi huo umefanyika kufuatia kifo cha ghafla cha aliyekuwa Mkurugenzi mteule, Dkt. Faustine Ndugulile, mnamo Novemba 2024. Nafasi hiyo ilivuta wagombea mahiri kutoka mataifa kadhaa, lakini Profesa Janabi alifanikiwa kuungwa mkono kwa wingi, akionesha kuwa jina la Tanzania bado lina nguvu katika diplomasia ya afya barani Afrika.
Kwa mujibu wa taratibu za Shirika la Afya Duniani, jina la Profesa Janabi sasa litawasilishwa kwa ajili ya kuthibitishwa rasmi na Bodi ya Utendaji ya WHO katika kikao chake cha 157 kitakachofanyika Mei 28–29, 2025, mjini Geneva, Uswisi.
Iwapo atathibitishwa, Profesa Janabi ataapishwa na kuanza kutekeleza rasmi majukumu yake kwa kipindi cha miaka mitano, huku akiwa na fursa ya kuongezewa muhula mmoja zaidi kulingana na kanuni za taasisi hiyo.
_▪️Amshukuru Rais Dkt. Samia ununuzi wa mitambo ya uteketezaji wa magugumaji
WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha changamoto ya uwepo wa magugumaji katika ziwa Victoria inapatiwa ufumbuzi ili kuwezesha shughuli za kijamii ziweze kuendelea katika maeneo hayo.
”Ninamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kutoa fedha za ununuzi wa mitambo mikubwa ya kuteketeza magugumaji ndani ya ziwa Victoria ili kuwezesha shughuli za uvuvi, usafiri na usafirishaji kuendelea.”
Waziri Mkuu ameyasema hayo leo (Jumatatu, Mei 19, 2025) wakati akizungumza na wananchi alipokagua shughuli ya udhibiti wa magugumaji katika eneo la Kigongo-Busisi akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Mwanza.
Mheshimiwa Majaliwa amesema magugumaji hayo yamekuwa yakiathiri kwa kiwango kikubwa shughuli mbalimbali za kijami na kiuchumi katika ziwa hilo, hivyo ununuzi wa mitambo hiyo utasaidia kuteketezwa kwa magugu hayo.
Aidha, Waziri Mkuu amewashukuru wananchi wa maeneo hayo wakiwemo wavuvi ambao wamejitolea kushirikiana na Serikali katika zoezi la kuyaondoa magugumaji hayo.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu ameiagiza Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira iendelee na kazi ya kuyaondoa magugumaji hayo hadi pale yatakapomalizika ili kuhakikisha shughuli za kijami zinaendelea bila ya kikwazo chochote.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Cyprian Luhemeja akitoa taarifa kuhusu shughuli ya kuteketeza magugumaji hayo kwa Waziri Mkuu amesema kwa sasa wanaendelea na kazi ya kuyaondoa magugumaji ya asili ambayo yamesambaa katika eneo la ukubwa wa ekari zaidi ya 300.
Amesema magugumaji hayo ambayo yamegawanyika katika aina tatu (salivinia molesta ambalo ni jipya, water hyacinth na gugumaji la asili aina ya Lutende) yameathiri mfumo wa ikolojia, shughuli za usafiri na usafirishaji na shughuli za uvuvi katika baadhi ya maeneo ndani ya Ziwa Victoria
Katibu Mkuu huyo amesema wanatarajia kumaliza kazi ya kuyateketeza magugumaji mwezi Julai, 2025 na hivyo kuwezesha shughuli za uvuvi, usafiri na usafirishaji kuendelea katika ziwa Victoria kama ilivyokuwa awali.
Tulizo Henry Kilaga I A Brand Communication Strategist,
Located: Dodoma I Dar es Salaam - Tanzania.
Call/WhatsApp: +255 765 888887