Showing posts with label habari. Show all posts
Showing posts with label habari. Show all posts

DKT.BITEKO KUZINDUA MKAKATI WA TAIFA WA MAWASILIANO WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

May 30, 2025 Add Comment

 


 Imeelezwa kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko tarehe 2 Juni 2025 atazindua Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wa Nishati Safi ya Kupikia ambao ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha kuwa asilimia 80 ya Watanzania wanatumia Nishati Safi ya Kupikia ifikapo 2034.


Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba amesema uzinduzi wa Mkakati utaenda sambamba na uzinduzi wa Kampeni ya Kitaifa ya Uhamasishaji na  Uelimishaji wa matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.


Mramba ameeleza kuwa mkakati huo umeandaliwa na Wizara ya Nishati  kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Mitaji la Umoja wa Mataifa (UNCDF) chini ya ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU), ikiwa ni pamoja na Kampeni ya Kitaifa ya Uhamasishaji na Uelimishaji kuhusu Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia.


 Ameongeza kuwa  uzinduzi huo utaenda sambamba na Wizara ya Nishati  kukabidhiwa magari mawili kwa ajili ya  kuendesha Kampeni ya Kitaifa ya Uhamasishaji wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ili kuwafikia wananchi hasa sehemu za vijijini.


Mhandisi Mramba amesema Mkakati unalenga masuala mbalimbali ikiwemo kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu faida za nishati safi ya kupikia katika afya, mazingira na uchumi wa kaya, kuhamasisha mabadiliko ya tabia kutoka kwa matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia kama mkaa na kuni, kuhamasisha uwekezaji na ushiriki wa sekta binafsi katika soko la bidhaa za nishati safi ya kupikia na kujenga mazingira ya sera na udhibiti yanayosaidia upatikanaji na upatikanaji wa nishati safi kwa wote.


Amesema mbinu mbalimbali za mawasiliano zitatumika  ikiwemo  vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa,  viongozi wa kimila, kidini, na kisiasa, matumizi ya mitandao ya kijamii na mafunzo kwa watendaji wa Serikali na Waandishi wa Habari na kuyafikia makundi mbalimbali  ya wananchi wa mijini na vijijini, wanawake na vijana, watoa huduma za afya, viongozi wa serikali za mitaa, mashirika ya kiraia na sekta binafsi.


Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Marc Stalmans, Mkuu wa Ushirikiano wa  Umoja wa Ulaya upande wa Tanzania na Bw. Immanuel Muro, Mtaalam Mwandamizi wa fedha kutoka UNCDF ambao kwa pamoja wameeleza kuunga mkono juhudi za Serikali katika Uhamasishaji wa Nishati Safi ya Kupikia.




TAKUKURU TANGA YABORESHA MFUMO WA HUDUMA ZA UDHIBITI TAKA NGUMU JIJINI TANGA

May 30, 2025 Add Comment


Na Oscar Assenga, TANGA

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoani Tanga (Takukuru) imesema kwamba moja ya mafanikio ya utendaji wake kazi katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari hadi Machi 2025 uboreshaji mfumo wa huduma za udhibiti Taka Ngumu Jijini Tanga.

Hayo yalisemwa leo na Kaimu Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Tanga Mariam Mayaya wakati akitoa taarifa kwa umma juu ya mafanikio ya utendaji kazi wa Taasisi hiyo kwa kipindi cha Januari hadi Machi 2025.

Alisema kwa upande wa uchambuzi wa mifumo katika kipindi hicho taasisi hiyo imefanikiwa kutekeleza matakwa ya sheria na kanuni za udhibiti taka ngumu nchini Tanzania kwa kutumia mfumo wa Punguza,Tumia Tena na Rejeleza taka (PTR) au Reduce,Re-use and Reycle (3R),

Aidha alisema katika mkoa wa Tanga mfumo huo ulianza katika kata ya Central,Chumbageni na Ngamiani Kati pamoja na utekelezaji wa sheria ya udhibiti wa taka ngumu,uchambuzi uliofanywa na Takukuru umesaidia mikakati na maazimio ya kulipwa kwa madeni ya wazabuni hivyo kufanya kazi ya uzoaji taka kuanza kutekelezwa kwa ufanisi.

Mariam alisema kwamba kwa ujumla zimefanyika chambuzi za mifumo 20 katika sekta za udhibiti take na usafi wa Mazingira,Afya,Kilimo na mapato ambapo wamefanikiwa kubaini mapungufu na kuwasilisha ripoti za chambuzi husika kwa wadau ambazo zimejadiliwa na maazimio yaliyofikiwa yametekelezwa na mengine yanaendelea kutekelezwa kwa ufanisi.

Akizungumzia ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo,Mariam alisema kwamba katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025 walifanya kazi ya ufuatiliaji wa matumizi ya rasilimali za umma katika miradi 54 yenye thamani ya Bilioni 240,264,703,118.09.

Alisema katika ufuatiliaji wa miradi hiyo iliyopo katika sekta za Maji,Elimu na Afya ambapo miradi 12 yenye thamani ya Sh.Bilioni 5,468,760,058 ilibainika kuwa na mapungufu ambapo ushauri wa marekebisho yalitolewa na hatua za marekebisho ya mapungufu hayo zimechukuliwa na miradi ipo katika hali inayokidhi ubora kulingana na thamani ya fedha zilizowekezwa.

Mradi wa Miaka 13 wa Amend Wazidi Kutoa Matunda Tanzania

May 29, 2025 Add Comment

WADAU wa usalama wa barabarani wametoa wito wa kuanzishwa kwa mjadala wa kitaifa kuhusu namna ya kudhibiti ajali za barabarani, wakisisitiza kuwa vifo na majeruhi vinavyotokana na ajali hizo hususani kwa Watoto, haviwezi kuvumilika tena katika jamii ya Watanzania.

PROF. MUSHI: TUONDOE VIKWAZO VYA USAJILI KWA WANAFUNZI WA KIKE

May 29, 2025 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Daniel Mushi, ametoa wito kwa wadau wa elimu nchini kuunga mkono juhudi za serikali kwa kufadhili masomo ya elimu ya juu kwa wasichana hasa wanaoishi kwenye mazingira magumu.

KAPINGA ATAJA VIGEZO VYA ZIADA UPELEKAJI UMEME VITONGOJINI

May 29, 2025 Add Comment



*📌  Lengo ni kuhakikisha kila Jimbo linakuwa na vitongoji vingi vilivyofikiwa na umeme*


*📌 Vinahusisha mahitaji ya kiuchumi na Kijamii, ukubwa wa Jimbo na Kitongoji*


*📌  Mkurugenzi Mkuu REA atakiwa kumsimamia kwa karibu Mkandarasi wa miradi ya Vitongoji Ziwa Tanganyika*


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza miradi ya umeme katika Vitongoji kwa kuzingatia vigezo vya ziada ikiwemo ukubwa wa vitongoji, ukubwa wa Jimbo pamoja na mahitaji ya kiuchumi na kijamii.


Lengo la kuweka vigezo hivyo ni kuhakikisha kuwa kila jimbo linakuwa na vitongoji vingi vilivyofikiwa na nishati ya umeme.


Mhe. Kapinga ameyasema hayo leo Mei 29, 2025 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la la Mbunge wa Simanjiro, Mhe. Christopher Olesendeka aliyeuliza kwamba  Serikali imejipangaje kutekeleza miradi ya Vitongoji kulingana na jiografia ya Wilaya ya Simanjiro ambapo umbali kutoka Kitongoji kimoja hadi kingine ni zaidi ya kilometa kumi.


"Mheshimiwa Naibu Spika, tunatekeleza miradi hii ya Vitongoji kwa kuzingatia vigezo vya ziada, tumeangalia ukubwa wa jimbo husika, ukubwa wa Vitongoji na mahitaji ya kiuchumi na kijamii katika jimbo husika. Niwahakikishie Wabunge mtaona utofauti katika miradi hii tunayoitekeleza hivi sasa."  Amesema  Kapinga


Akijibu swali la Mbunge wa Nyasa Mhe. Stella Manyanya aliyeuliza kuhusu kitongoji cha  Songea Pori kilichopo katika Kijiji cha Lunyele  na Kitongoji cha Nindi kilichopo Kijiji cha Konganywita kufikishiwa nishati ya umeme, Mhe. Kapinga amesema Vitongoji hivyo vimefanyiwa upembuzi yakinifu na kubainika vinahitaji njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kati kwa umbali wa kilometa tatu.


Amesema  Serikali inatarajia kuvipelekea umeme vitongoji hivyo kupitia Mradi wa Kupeleka Umeme Vitongojini Awamu ya Pili B  (HEP IIB) ambao utekelezaji wake utaanza mwaka wa fedha 2025/2026. 


Kuhusiana na kasi ndogo ya Mkandarasi anayetekeleza miradi ya umeme katika Jimbo la Nyasa Mhe. Kapinga amesema tayari Serikali imeshakutana na Mkandarasa na kumuagiza kuweka Wakandarasi wadogo (sub contractors) katika miradi yake anayotekeleza.


Akijibu swali la Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Mhe. Aida Khenani aliyetaka  kauli ya Serikali kuhusu kusuasua kwa Mkandarasi ambaye amepewa kazi ya kupeleka umeme kwenye Vitongoji vilivyozunguka ziwa Tanganyika, Mhe. Kapinga amesema katika utekelezaji wa miradi ya Vitongoji Serikali imehakikisha inawapata wakandarasi wenye weledi.


Kuhusu Wakandarasi ambao wanasuasua,  Kapinga kwa niaba ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kumsimamia Mkandarasi anayetekeleza mradi huo wa umeme kwenye Vitongoji vilivyozunguka ziwa Tanganyika.


Aidha, amemuagiza kuchukua hatua za ziada kwa Mkandarasi huyo kuhakikisha anatekeleza mradi huo kwa haraka na kwa weledi.