Showing posts with label habari. Show all posts
Showing posts with label habari. Show all posts

WAZIRI ULEGA AUNDA TIMU KUCHUNGUZA KIVUKO CHA MV TANGA

May 13, 2025 Add Comment

 



Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega ameunda timu ya wataalamu na kuipa siku saba kuchunguza changamoto zinazojitokeza mara kwa mara katika Kivuko cha MV TANGA kilichopo wilayani Pangani, mkoani Tanga baada ya kupokea malalamiko ya wananchi kuhusu kusuasua kwa utendaji wake.

Pia, katika ziara yake mkoani Tanga, Ulega pia amemtaka mkandarasi aliyepewa kazi ya kujenga barabara ya Tanga - Pangani - Mkwaja - Bagamoyo (Makurunge) sehemu ya Tungamaa - Mkwaja – Mkange, kuilipa serikali fidia kutokana na uzembe uliofanya ujenzi usikamilike kwa wakati ilhali tayari serikali imetimiza upande wake wa mkataba ikiwamo kumlipa mkandarasi huyo.

Akizungumza kwa nyakati tofauti mkoani humo, Ulega alisema serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inafanya jitihada kubwa za ukarabati na ununuzi wa vivuko ili kurahisisha maisha ya wananchi na kwamba wananchi hawapaswi kupata shida wakati miundombinu ipo.

Kivuko aambacho kimeundiwa tume ni ya uchunguzi kinatoa huduma kati ya Pangani na Bweni na Ulega alisema lengo ni kuhakikisha kuwa kivuko hicho kinafanya kazi kwa wakati wote kama ilivyokusudiwa.

Naunda timu ya watu watatu, mmoja kutoka Ofisi ya Rais wa kutoka hapa na wawili Katibu Mkuu wa Ujenzi atawateua kutoka wizarani ili iniambie ni nini hasa kinaendelea hapa Pangani, haiwezi ikawa kila siku wananchi wanapata usumbufu”, amesisitiza Ulega.

Ulega amefanya maamuzi hayo kutokana na Kivuko hicho cha MV TANGA kushindwa kufanya kazi kwa siku nne huku watendaji na wasimamizi wakishindwa kufanya maamuzi ya haraka ya upatikanaji wa vipuri vya kufungwa katika kivuko hicho na kusisitiza kuwa endapo itabainika kuna hujuma zinafanyika katika kivuko hicho atachukua hatua za kinidhamu.

Akizungumza kabla ya Ulega, Mbunge wa Jimbo la Pangani ambaye pia ni Waziri wa Maji, Jumaa Aweso alimuomba waziri huyo kushughulikia changamoto ya usafiri wa Kivuko cha MV TANGA ambacho ni muhimu na msaada kwa wananchi wa Pangani.

Katika hatua nyingine, Waziri Ulega amekagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Pangani lenye urefu wa mita 525 na kuridhishwa na hatua zilizofikiwa.






MAWAZIRI WA SADC WAKUTANA KUJADILI USIMAMIZI WA MAAFA

May 13, 2025 Add Comment

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Mhe. Ummy Nderiananga, ameshiriki mkutano wa dharura wa Kamati ya Mawaziri wanaohusika na Usimamizi wa Maafa kwa Nchi Wanachama wa SADC, uliofanyika leo tarehe 13 Mei 2025 kwa njia ya mtandao.

Mkutano huo wa dharura umelenga kujadili hatua za kuimarisha mfumo wa usimamizi wa maafa na huduma za kibinadamu kwa nchi wanachama wa SADC.

Pia Mkutano huo umelenga kujadili hatua za kuimarisha usimamizi wa maafa na kuunga mkono ushirikiano wa kikanda katika kukabiliana na maafa na kuendelea kujenga usalama wa watu na mali, Aidha Waziri wa Serikali za Mitaa na Kazi za Umma wa Zimbabwe, Bw. Daniel Garwe, ameongoza mkutano huo kama Mwenyekiti.

Pamoja na hayo Mhe. Ummy Nderiananga ameutumia mkutano huo kutoa pongezi kwa Sekretarieti ya SADC kwa kuanzisha kituo cha huduma za kibinadamu na operesheni za dharura kilichopo Msumbiji, akisisitiza umuhimu wa kituo hicho katika kuimarisha ushirikiano na kukabiliana na maafa. Pia, amekubaliana na ongezeko la wataalamu 35 katika timu ya SADC ya utayari wa kukabiliana na dharura. 

Mkutano huu umeonesha mshikamano wa kikanda katika kuimarisha usalama na kukuza uchumi wa nchi za SADC kupitia usimamizi bora wa maafa.



TBS Yaweka Mikakati Nishati Safi ya Kupikia

May 13, 2025 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limechukua hatua ya kuandaa viwango vya ubora kwa bidhaa za nishati safi ya kupikia, ikiwa ni sehemu ya jitihada za serikali kuhakikisha usalama wa afya ya wananchi na kuhifadhi mazingira.

BUNGE LAPITISHA KWA KISHINDO BAJETI YA WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA YA TRILIONI 2.4

May 13, 2025 Add Comment
Kwa kauli moja leo tarehe 13 Mei 2025 Bunge la Tanzania limepitisha kwa kishindo bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi zake kwa mwaka 2025/2026 yenye jumla ya shilingi Trilioni 2.439.

Bajeti hiyo imepitishwa kwa asilimia 100 na wabunge ili kuwezesha utekelezaji wa malengo yaliyoanishwa kwa mwaka wa fedha 2025/26, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Taasisi zake.

Kati ya fedha hizo zilizopitishwa jumla ya shilingi Bilioni 688.6 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida ya Wizara ambapo Shilingi Bilioni 635.2 ni kwa ajili ya Mishahara na Shilingi Bilioni 53.3 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo.

Utekelezaji wa bajeti hiyo utajikita zaidi katika maeneo matano ya vipaumbele ambayo ni i) kuendelea na utekelezaji wa Sera na Mitaala, Mapitio ya sheria, Uandaaji wa miongozo, na utoaji wa mafunzo, ii) Kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa mafunzo ya Amali katika shule za sekondari na vyuo vya Amali, iii) Kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa elimu ya Amali, Msingi, Sekondari na Ualimu, iv) Kuongeza na kuimarisha ubora wa elimu ya juu na v) Kuimarisha uwezo wa nchi katika utafiti, Matumizi ya Sanyansi, Teknolojia na Ubunifu ili kuchangia upatikanaji wa maendeleo endelevu.

Wabunge wamempongeza Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Prof Adolf Mkenda (Mb) kwa utulivu wa kiutendaji katika wizara yake na mshikamano alionao na watendaji wote wa Wizara na kumsihi kusimamia kwa weledi mkubwa wizara hiyo ambayo ni msingi wa maendeleo ya nchi.

Kati ya fedha zilizopitishwa, zaidi ya shilingi Trilioni 1.7 ni kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo ambapo Shilingi 1.186 ni fedha za ndani na Shilingi 560.8 ni fedha kutoka kwa Washirika wa Maendeleo.

Kwa mujibu wa Waziri Mkenda, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO imeidhinishiwa jumla ya Shilingi Bilioni 3.2 kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida ambapo Mishahara ni Shilingi Bilioni 1.5 na Matumizi Mengineyo ni Shilingi Bilioni 1.7

Waziri Mkenda amesema kuwa jumla ya wabunge 36 wamechangia moja kwa moja huku wengine wakichangia kwa maandishi ambapo wote kwa pamoja wameshauri na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa mageuzi makubwa ya pili ya elimu sambamba na ongezeko kubwa la bajeti.

Pia Waziri Mkenda amesema kuwa wabunge wote waliochangia pia wamempongeza Rais Samia kwa kuongeza mikopo elimu ya juu, ongezeko la Vyuo vya Ufundi stadi-VETA, Ujenzi na ongezeko la shule za Amali pamoja na Ujenzi wa kampasi mpya za vyuo vikuu.

ULEGA AVUNJA MKATABA WA MKANDARASI MZEMBE

May 13, 2025 Add Comment

 



Na Mwandishi Wetu, Tanga

Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega ametangaza kuvunjwa kwa mkataba wa ujenzi wa barabara Mkoani Tanga baada ya Mkandarasi kutoka China kushindwa kutimiza masharti ya mkataba. 

Mkandarasi huyo, kampuni ya China Railway 15 Bureua Group anayejenga barabara ya Tanga - Pangani - Mkwaja - Bagamoyo (Makurunge) sehemu ya Tungamaa - Mkwaja - Mkange (km 95.2) wilayani Pangani anadaiwa kushindwa kufanya kazi aliyotakiwa kuifanya kwa wakati ingawa tayari amelipwa fedha yote na serikali. 

Baada ya kuvunja mkataba wa awali, Waziri Ulega amemuagiza Katibu Mkuu wa Ujenzi, Balozi Mhandisi Aisha Amour, kuondoa kilometa 25 za barabara hiyo ambazo hajazifanyiwa kazi na badala yake itangazwe zabuni mpya ili wenye uwezo wa kufanya kazi hiyo wapewe kazi na waanze haraka. 

Kufuatia agizo hilo, sasa kilometa 25 za barabara hiyo na kilometa 70 za barabara inayoanzia Mkange hadi Bagamoyo (Makurunge) zitaunganishwa kwenye zabuni ili apatikane Mkandarasi wa kuijenga.

Ulega ametoa maelekezo hayo leo Mei 12, 2025 kwenye ziara yake Mkoani Tanga ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa sehemu ya barabara hiyo ambayo Serikali imekwishamlipa Mkandarasi kiasi cha shilingi Bilioni 47 ingawa hadi sasa utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 48 tu.

“Mkandarasi huyu ametuangusha na hapa sisi hadai hata senti kwani tushamlipa zaidi ya bilioni 40, yupo nyuma ya muda, vifaa hajavileta vyote, wafanyakazi hawajawaleta wote, hivyo nimechukua maamuzi ya kumnyang’anya sehemu ya kazi ya mradi ili mradi huu ukamilike kwani ni wa muda mrefu na ni kilio cha wananchi wa Pangani na Mkoa wa Tanga kiujumla”, amesisitiza Ulega.

Ulega ameendelea kusisitiza kuwa maamuzi hayo ya kumyang’anya mkandarasi sehemu ya kazi ni kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi kwasababu Serikali ingeamua kuvunja mkataba wote ingechukua zaidi ya miezi 6 hadi mwaka mzima mpaka Mkandarasi mpya aanze kazi na hasara yake mradi kuendelea kuchelewa.

Vilevile, Ulega amemtaka Mkandarasi huyo kuilipa fidia Serikali kwa kuchelewesha mradi huo ambapo ameielekeza timu wa wataalam kuendelea kuchambua kimkataba juu ya hatua zitakazochukuliwa. 

Ulega amemwagiza Katibu Mkuu huyo kumweka mkandarasi huyo katika orodha ya Wakandarasi wasiofanya kazi vizuri katika miradi ya ujenzi kwa siku za usoni ili iweze kusadia wakati wa kupata Makandarasi wengine katika miradi mbalimbali ya ujenzi hapa nchini.

Kuhusu kilometa 70 ambazo Mkandarasi atatakiwa kuzimalizia, Ulega ameagiza Wakala wa Barabara (TANROADS) kuisimamia kampuni hiyo ya China Railway 15 Bureua Group kufanya kazi usiku na mchana ili azikamilishe kuzijenga kwa kiwango cha lami ifikapo mwezi Oktoba mwaka huu na ikiwa Wataalamu hao watashindwa kuwasimamia kikamilifu na wao watabadilishwa.

Kwa upande wake Msimamizi wa Mradi kutoka TANROADS, Mhandisi Julius Msofe ameeleza kuwa hadi sasa ujenzi wa mradi huo umefikia asilimia 47.82 ikilinganishwa na mpango kazi wa asilimia 100 na kuongeza kuwa muda wa mkataba wa miezi 36 sawa na asilimia 100 umeisha tangu tarehe 31 Machi 2025.