TANZANIA NA CUBA KUENDELEZA USHIRIKIANO

October 03, 2016
mao1
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mgeni wake Makamu wa Rais wa Cuba Mh. Salvador Valdes Mesa wakati alipokutana naye Ikuu leo kwa mazungumzo ambapo wamezungumzia  jitihada za Serikali hizi mbili ya Cuba na Tanzania katika kuendelea kuimarisha na kudumisha mahusiano mazuri yaliyopo kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizi mbili.(PICHA KWA HISANI YA OFISI YA MAKAMU WA RAIS)
mao2
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Samia Suluhu Hassan  na Mgeni wake Makamu wa Rais wa Cuba Mh. Salvador Valdes Mesa wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya  viongozi wa Tanzania na Cuba.
mao3
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Samia Suluhu Hassan akimkabidhi zawadi ya picha ya mnyama Chui anayepatikana  katika mbuga za wanyama za Tanzania Mgeni wake Makamu wa Rais wa Cuba Mh. Salvador Valdes Mesa.
mao4
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokea zawadi ya picha kutoka kwa  Mgeni wake Makamu wa Rais wa Cuba Mh. Salvador Valdes Mesa , Kulia ni Mhe. Balozi Dkt. Augustine Mahiga Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Kikanda na Kimataifa.
……………………………………………………………………………………
Na. Immaculate Makilika- MAELEZO
Serikali ya  Tanzania na Cuba zimeahidi kuendeleza ushirikiano  uliopo, ambao umeasisiwa na viongozi wa mataifa hayo Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wa Tanzania pamoja na Fidel Castro  Rais  mstaafu wa Cuba.
Akizungumza na waandishi wa habari,  Ikulu leo jijini Dar es salaam, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Mhe. Samia Suluhu, amesema kuwa  Makamu wa Rais wa Cuba,  Mhe. Salvador Valdes Mesa ameitikia mwaliko huo wa kuja nchini kwa vile nchi  hizo mbili zimekua na ushirikiano na mahusiano mazuri kwa muda mrefu.
“Ziara hii ni moja ya jitihada za Serikali hizi mbili ya Cuba na Tanzania katika kuendelea kuimarisha na kudumisha mahusiano mazuri yaliyopo kwa manufaa ya wananchi wa nchi hizi mbili ili kuhakikisha mahusiano yaliyopo yanaimarika zaidi” alisema Makamu wa Rais
Katika ziara  hiyo ya Makamu wa Rais wa Cuba nchini, mambo mbalimbali yalijadiliwa ikiwemo masuala ya Afya, Elimu, Michezo, na Utamaduni, ambapo katika sekta ya afya nchi ya Cuba  imepiga hatua na kuahidi  kushirikiana na Tanzania  ili kujenga kiwanda cha kisasa  cha kutengeneza madawa ya binadamu.
Aliongeza kuwa Tanzania imeomba Serikali ya |Cuba kuendelea kusaidia sekta hiyo kwa kufundisha wataalamu wa afya, ambapo tayari madaktari 24 kutoka Cuba wako nchini kwa ajili ya kusaidia kutoa huduma  za kitabibu na mafunzo katika mikoa mbalimbali  ya Tanzania Bara na Visiwani.
Masuala mengine yaliyojadiliwa katika ziara hiyo ni pamoja na ushirikiano katika sekta ya elimu, biashara, utalii na uwekezaji.
Ambapo pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Suluhu amesisitiza nia ya Serikali ya Tanzania kudumisha ushirikiano huo ikiwa ni pamoja kupongeza jitihada za kuboresha uhusiano wa Cuba na Marekani.
Kwa upande wake, Makamu wa Rais  wa Cuba, Mhe. Salvador Antonio Valdes Mesa ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea kuonesha ushirikiano kwa nchi yake na kuahidi kuendelea kutoa msaada kwa Tanzania.
“Tumeamua kuendelea kuboresha mahusiano yetu na Tanzania kwa kuongeza ushirikiano wetu katika sekta nyingine ambazo hatukuwa tunashirikiana hapo awali kama vile sekta ya utalii” alisema Makamu wa Rais wa Cuba
Aidha, Mhe. Mesa ameiomba Tanzania kuendelea kuiunga mkono Cuba katika masuala ya kimataifa ili kuendeleza ushirikiano na kukuza uchumi kwa nchi zote mbili.
Makamu wa Rais wa Cuba aliwasili nchini jana jioni kwa ziara ya siku tatu  ambapo alipata fursa ya kuonana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa John Magufuli .

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »