DC MKINGA AHIMIZA VIJANA KUJIKITA KWENYE KILIMO

April 15, 2016


VIJANA wilayani Mkinga Mkoani Tanga wametakiwa kujikita kwenye kilimo ili waweze kupata mafanikio makubwa badala ya kukaa vijiweni ambapo hutumia muda mwingi kufikiria kufanya vitendo viovu badala yake wahakikisha wanashiriki katika shughuli za uzalishaji ili waweze kuchangia ukuaji wa maendeleo yao.

 Mkuu wa wilaya ya Mkinga,Mboni Mgaza aliyasema hayo juzi wakati ziara yake iliyolenga kuhamasisha shughuli za kilimo ambapo alisema endapo vijana hao watatumia muda wao kwenye kilimo itawasaidia kuweza kujikwamua kiuchumi.

Alisema kuwa vijana hao wanapaswa kubadilika na kuona umuhimu wa kuwajibika hasa wakati huu ambao wananchi wilayani humo wanaweka msukumo kwenye kilimo kwa kushiriki shughuli hizo kwa umakini mkubwa.

  “Unajua vijana ndio nguvu kazi kubwa kwa Taifa letu hivyo niwaase badala ya kukaa vijiweni na kucheza pool table wakati wa kazi watumie nafasi hiyo kwenye kilimo ambacho ndio ute wa mgongo kwa maendeleo ya nchi “Alisema

Aidha ili kuhakikisha jambo hilo linapata mafanikio makubwa aliwaagiza maafisa ugani kuacha kukaa maofisini badala yake wawafuate wakulima kwa ajili ya kuwapa utaalamu wa kilimo ili waweze kulima kisasa.

Sambamba na hayo mkuu huyo wa wilaya aliwataka maafisa ugani kuona umuhimu wa kwenda vijijini na kuacha kukaa maofisini ili waweze kutoa mbinu kwa wakulima waweze kulima kilimo chenye tija kwao.

Hata hivyo pia aliwataka wananchi kubadilika na kulima kilimo cha kisasa ikiwemo kuandaa mashamba yao sambamba na kupanda kisasa ili kupata mavuno mengi hali itakayowasaidia kukuza vipato vyao.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »