TIMU ya Coastal Union “Wagosi wa Kaya”kesho wanatarajia kucheza mechi ya kirafiki na timu ya Mombasa Combain ikiwa ni kukipa makali kikosi hicho kabla ya kucheza mechi zake zinazofuata za Ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara.
Mechi hiyo inatarajiwa kuchezwa kwenye uwanja wa CCM Mkwakwani kuanzia
saa kumi jioni ikiwemo wadau mbalimbali wa soka kutakiwa kujitokeza ili
kuweza kushuhudia mchezo huo.
Ofisa Habari wa Coastal Union, Oscar Assenga amesema kuwa mechi hiyo ni
sehemu ya kuhakikisha kikosi hicho kinajiimarisha zaidi kila idara kabla
ya mchezo wake na Polisi Morogoro.
Assenga amesema kuwa maandalizi ya kuelekea mchezo huo yamekamilika kwa
asilimia kubwa na Mombasa Combain wanatarajiwa kutua leo jijini hapa
tayari kwa ajili ya mechi hiyo itayochezwa kesho kuanzia saa kumi
jioni.
Hata hivyo aliwataka wapenzi wanachama na mashabiki wa soka kuhakikisha
hawakosi fursa hii adimu kuja kuishuhudia timu yao ikicheza kwenye
uwanja wake wa nyumbani kabla ya kuanza mechi za Ligi kuu zinazofuata.
Wakati huo huo,Kikosi cha timu ya Coastal Union kinaendelea na mazoezi
kila siku kwenye viwanja vya shule ya sekondari Popatlaly na sasa kipo
tayari kuweza kuikabili timu yoyote ile itakayokutana nayo na kuweza
kupata matokeo mazuri.