MWENGE WA UHURU 2025 KUPITIA MIRADI YENYE THAMANI YA BILIONI 3 WILAYA YA TANGA

June 14, 2025 Add Comment










Na Paskal Mbunga,TANGA

MWENGE wa Uhuru unatarajiwa kuwasili katika wilaya ya Tanga Jumatatu June 16 mwaka huu na upitia katika miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya Sh.Bilioni 3,058,289,671.99.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati akitoa taarifa za ujio wa Mwenge huo,Mkuu wa wilaya ya Tanga Dadi Kolimba alisema wataupokea ukitokea wilayani Mkinga katika uwanja wa shule ya Msingi Mabambani Mtaa wa Mpirani Kata ya Chongoleani.

Aliitaja miradi ambayo itapitiwa na Mwenge ni ujenzi wa madarasa 4 ya Ghorofa ,matundu 13 ya vyoo na ofisi shule ya Msingi Mbuyuni yenye thamani ya Milioni 388,769,596.80 na Ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa ya awali ya mfano shule ya msingi Mwakidila yenye thamani ya Milioni 70,100,000.00.

Mkuu huyo alisema pia miradi mingine ni ujenzi wa ofisi ya mtendaji kata ya Tongoni uliogharimu kiasi cha sh.Milioni 85,000,000.00,ujenzi wa barabara ya Sahare awamu ya kwanza na ya pili yenye urefu wa mita 600 kwa kiwango cha lami uliogharimu Sh.Milioni 489,606,700.00.

“Lakini pia Mwenge utapita katika ujenzi wa Jengo la X-Ray kituo cha Afya Makorora wenye thamani ya Sh.Milioni 84,721,640.00 pamoja na mradi wa ufungaji wa dira za maji za malipo ya kabla awamu ya kwanza wenye thamani ya Sh. 1,872,091,735.00 “Alisema.

Hata hivyo alisema kwamba mradi mwengine ambao utapitiwa na mwenge ni mradi wa kikundi cha vijana cha kutengeneza gypsum wenye thamani ya Sh.Milioni 68,000,000.00

Alisema mbali na miradi hiyo saba mwenge wa uhuru utakagua shughuli za maandalizi ya uchaguzi,kongamano la vijana pamoja na maswala mtambuka.

Mwisho.

KAMPENI YA PIKA SMART INAYOHAMASISA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA YAZINDULIWA

June 13, 2025 Add Comment


*📌 Kamishna Luoga asisitiza matumizi ya umeme katika Nishati Safi ya Kupikia*


Kamishina wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga amezindua kampeni ya kitaifa ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia ya umeme inayokwenda na kaulimbiu ya PIKA SMART.


Mha. Luoga amezindua kampeni hiyo leo Juni 13, 2025 jijini Dar es Salaam akimwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi  Mramba. 


Kampeni hiyo imeandaliwa na Shirika la Modern Energy Cooking Services (MECS) chini ya ufadhili wa UKAID kwa kushirikiana na Serikali kupitia Wizara ya Nishati.


Mhandisi Luoga amesema kampeni hiyo imezinduliwa ikiwa ni mojawapo ya jitihada za Serikali kuhakikisha inawahamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ili kufikia lengo la asilimia 80 ya watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034. 

Luoga amewatoa hofu wananchi kuhusu kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme akitanabaisha kuwa ni salama na gharama nafuu na kuongeza kuwa Tanzania Ina Umeme mwingi na wa kutosheleza mahitaji.

"Kama tunavyofahamu bwawa la kufua umeme kwa maji la Julius Nyerere limekamilika na hivyo kupelekea umeme uliopo nchini hadi sasa kufikia takribani megawati 4,031,  umeme huu umeshafika  katika Vijiji vyote 12, 318 vya Tanzania  hivyo kuna kila sababu kwa wananchi kutumia nishati safi ya umeme kupikia." amesema Mha. Luoga



Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Mkurugenzi wa Mipango na uwekezaji TANESCO, Mhandisi Henryfried Byabato amesema Shirika hilo limekuwa likihamasisha wananchi kutumia nishati safi ya kupikia ya umeme kutokana na uwepo wa kutosha wa nishati hiyo nchini.

Ameongeza kuwa, teknolojia  zimeboreshwa hivyo majiko ya umeme yanatumia nishati kidogo na kwa ufanisi mkubwa.

Kampeni hii ya kuhamasisha matumizi ya pika smart imekuja wakati muafaka ambapo Wizara ya Nishati imezindua mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wenye lengo la kutoa mwongozo kwa wadau kuendeleza kampeni ya uhamasishaji matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan ambaye ni kinara wa nishati safi ya kupikia kuhakikisha watanzania wanahama kutoka kwenye matumizi ya nishati isiyo safi kwenda kwenye nishati safi



RC MTANDA AWATAKA WAKANDARASI REA KUHARAKISHA UTEKEZAJI MIRADI YA UMEME JUA VISIWANI

June 13, 2025 Add Comment


Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. Said Mtanda, amewataka wakandarasi wanaotekeleza mradi wa usambazaji wa mifumo midogo ya umeme jua katika maeneo ya visiwani kuhakikisha wanatumia muda vizuri na kukamilisha kazi kwa wakati, ili kuwaondolea wananchi wa maeneo hayo adha ya ukosefu wa nishati ya uhakika.


Akizungumza leo Juni 13, 2025 ofisini kwake jijini Mwanza, Mhe. Mtanda amewataka pia wataalamu kutoka Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kuhakikisha kuwa wakandarasi wanalipwa kwa wakati, jambo litakalowasaidia kuendelea na kazi bila kuchelewa.

“Ni muhimu kutumia muda vizuri na kukamilisha miradi hii kwa wakati. Serikali inatambua juhudi za kila mkandarasi anayefanya kazi kwa bidii na kwa ufanisi, na hao ndio wanaopewa kazi nyingine zaidi. Chema chajiuza, kibaya chajitembeza,” amesema RC Mtanda.


Mkuu huyo wa mkoa pia amewasisitizia wakandarasi umuhimu wa kujitambulisha kwa mamlaka za mikoa, wilaya, tarafa na vijiji ili jamii ziwe na uelewa wa mradi huo, kushirikishwa kikamilifu na kutoa maoni, taarifa au mapendekezo yatakayosaidia kufanikisha utekelezaji wake.

“Kwa kufanya hivyo, mtapata ushirikiano mkubwa kutoka kwa wananchi. Na pale changamoto zinapojitokeza, ni rahisi kupata msaada au taarifa muhimu kutoka kwao,” aliongeza.


Kwa upande wake, Msimamizi wa Miradi ya REA Kanda ya Ziwa, Mhandisi Ernest Makale, amesema mradi huo wa umeme wa jua unatekelezwa katika visiwa 78 vilivyopo wilaya tano za Mkoa wa Mwanza ambazo ni Sengerema, Buchosa, Ukerewe, Magu na Ilemela.

Mhandisi Makale Pia amebainisha  kuwa zaidi ya shilingi bilioni 4 tayari zimetengwa kwa ajili ya mradi huo, ambao unalenga kufikisha huduma ya umeme katika nyumba takribani 8,410 kwa bei ya ruzuku ya mpaka asilimia 75.


Lengo kuu la mradi huo ni kuhakikisha kuwa wakazi wa maeneo ya visiwani wanapata huduma ya nishati ya umeme ya uhakika, jambo litakaloboresha maisha yao na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika maeneo husika.


Mwisho.

CRDB Bank Foundation, StartHub Africa zaungana kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu

June 13, 2025 Add Comment

 

Meneja Uendelezaji Biashara Changa wa CRDB Bank Foundation, Sharron Nsule akitoa elimu ya ujasiriamali kwa wanafunzi walioshiriki semina katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Dar es Salaam, Tanzania – June 2025: Katika kuendeleza jitihada za kuinua ujasiriamali na kuwawezesha wanafunzi wabunifu, Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kushirikiana na StartHub Africa imevitembelea vyuo vikuu vitatu nchini na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanafunzi wanaopenda kumiliki biashara baada ya masomo yao.

Ushirikiano huo unaotekelezwa kupitia programu ya “Uni Launch and Scale” tayari umewafikia zaidi ya wanafunzi 1,000 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Kikuu cha Iringa na Taasisi ya Uhasibu Arusha (AIA) na kuwapa fursa ya kupata walezi wa kibiashara na mitaji wezeshi kutoka CRDB Bank Foundation.

Akizungumzia mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa amesema vyuo hivi vitatu ni mwanzo tu kwani lengo lililopo ni kuwafikia wanafunzi wengi zaidi na kuwawezesha ili wanapohitimu au wakai wanaendelea na masomo yao waanze kushiriki shughuli za kuujenga uchumi baada ya kuwapa elimu ya fedha, mafunzo ya ujasiriamali na uhakika wa kupata mtaji wezeshi.

“Lengo letu ni kuamsha ari ya ujasiriamali iliyomo ndani ya wanafunzi wetu wa vyuo vikuu na kutoa mazingia rafiki kwao kuanzisha biashara zitakazoajiri vijana wenzao badala ya wao wenyewe kuwa waombaji wa kazi wakihitimu. Kupitia ushirikiano huu tunajenga kizazi cha vijana waliowezeshwa kushiriki kuujenga uchumi wa taifa letu,” anasema Tully.

Katika vyuo vitatu ambako wataalamu wa CRDB Bank Foundation na StartHub Africa wamepita, jumla ya biashara 30 zinazomilikiwa na kuendeshwa na wanafunzi zitachaguliwa baada ya kukaguliwa ili kuingizwa kwenye mpango maalumu wa mafunzo ya usimamizi na uendeshaji biashara, utayari wa kifedha na utimamu wa bidhaa.

“Kwa kushirikiana na StartHub Africa pamoja na vyuo vikuu hivi, tunaamini tunaendeleza juhudi za kukuza ubunifu hasa wa kidijitali miongoni mwa wanafunzi wetu hivyo kujenga msingi imara wa biashara zinazoweza kukua na kuwanufaisha wananchi wengi,” amesema Tully.

Programu ya Uni Launch and Scale ambayo CRDB Bank Foundation inashirikiana na StartHub Africa kuitekeleza inalenga kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu kutekeleza uwekezaji wanaoukusudia kwa kuwapa mafunzo, ulezi wa kibiashara na uwezeshaji wa mitaji kupitia Programu ya Imbeju iliyojielekeza kuwainua vijana, wanawake na makundi maalumu.

Meneja Programu wa StartHub Africa, Zagaro Emanuel anasema katika ushirikiano huu wanakusudia kuwawezesha vijana wengi wabunifu kupitia mafunzo ya ujasiriamali na elimu ya fedha hivyo kuchangia kuujenga uchumi na kusukuma mbele maendeleo ya Tanzania.

“Tunawahamasisha wanafunzi na wahitimu wa vyuo vikuu, tunawandaa waanzilishi wapya wa biashara watakaosaidia kuleta mapinduzi ya kiuchumi na kuimarisha ujasiriamali nchini kwa kushirikiana na vyuo vikuu, wawekezaji na wawezeshaji. Tukiwa pamoja na Taasisi ya CRDB Bank Foundation, tunaamini tutafika mbali na kuwajumuisha wanafunzi wengi zaidi nchini,” anasema Emanuel.

Meneja huyo anaongeza kwamba programu hiyo inawapa wanafunzi jukwaa la kujitangaza katika soko la ndani, kitaifa na kimataifa na wanapowasilisha mawazo ya miradi yao, wanajiweka kwenye nafasi nzuri zaidi ya kuvutia mitaji huku vyombo vya habari vikiwarahisishia kujulikana kwa biashara zao hivyo kujiongezea umanifu kwa wadau ambalo ni jambo jema kwa kila biashara.

GCLA YAWAPA HAMASA VIJANA KUCHANGAMKIA MASOMO YA SAYANSI

June 12, 2025 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MAMLAKA ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imetoa zawadi kwa kuwatunuku vyeti wanafunzi wahitimu 48 na walimu 8 waliofanya vizuri zaidi kwenye masomo ya sayansi kidato cha nne 2023 na kidato cha sita 2024 kwa kutambua bidii na kujituma kwao katika kusoma masomo hayo.